Makala

Sekunde za mwisho kabla ya kifo Ojwang

Na SAMWEL OWINO June 14th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

KIKAO cha faragha kati ya Mamlaka Huru ya Kuchunguza Utendakazi wa Polisi (IPOA) na Kamati ya Bunge la Taifa kuhusu Usalama kilifichua maelezo ya kushtua kuhusu jinsi mwanablogu Albert Ojwang’ alivyouawa na polisi.

Duru kutoka ndani ya kikao hicho ziliambia Taifa Leo kuwa, IPOA imepiga hatua kubwa katika kuwasaka wauaji wa Bw Ojwang’.

Mamlaka hiyo iliambia kamati inayoongozwa na Gabriel Tongoyo kuwa, tangu mwanzo, Ojwang’ alikuwa amepangiwa kuuawa kwani mara tu safari ya kumleta Nairobi ilipoanza, mahabusu walihamishwa kutoka seli na wauaji wakaachwa nyuma kusaidia kutekeleza mauaji hayo.

Wahalifu wa makosa madogo walihamishiwa vituo vingine ili kutoa nafasi kwa Bw Ojwang’.

Inaripotiwa kuwa, wauaji hao kwa kushirikiana na maafisa wa polisi, walimuua Bw Ojwang’ usiku wa manane Juni 8, 2025.

IPOA ilieleza kuwa afisa mmoja mkuu wa polisi ambaye zamu yake ilifaa kuisha saa mbili usiku alikataa kwenda nyumbani kwa makusudi na akaendelea kufanya kazi hadi saa tisa usiku.

Mamlaka hiyo, inayoongozwa na Issac Hassan, iliwaambia wabunge kuwa afisa huyo (ambaye tayari amerekodi taarifa) alisema kuwa ‘alikuwa na kazi ya kufanya’.

Baada ya mauaji hayo kukamilika, alijaribu kukabidhi zamu kwa afisa aitwaye Kimani, ambaye alikataa kupokea zamu baada ya kugundua kuwa Bw Ojwang’ alikuwa amefariki.

“Kimani alienda na kumgusa Ojwang’ na akagundua alikuwa amekufa kwani moyo haukuwa ukipiga. Alikataa kuchukua zamu maiti ikiwa ndani ya seli,” IPOA iliripotiwa ilivyofahamisha kamati.

IPOA pia imeelekeza uchunguzi kwa OCS wa Kituo cha Polisi cha Central, ambaye inadaiwa aliagiza fundi wa kamera za CCTV afike kuvuruga vifaa hivyo ili kuficha tukio hilo la mauaji.

Mamlaka hiyo iliambia kamati kuwa iwapo itaweza kubaini aliyeagiza OCS kuwasiliana na fundi wa CCTV kuzima kamera, basi mtu huyo atatoa ushahidi muhimu.

Jana jioni, Mkuu wa Kituo cha Polisi cha Central Bw Samson Talaam alikamatwa na makachero mjini Eldoret ambapo inadaiwa alitorokea.

Kabla ya waandishi wa habari kuondolewa kwenye kikao, Bw Hassan alisema mtu alitumwa mahsusi kufuta sehemu ya video ya CCTV ambayo ingeweza kufichua yaliyojiri kwa Bw Ojwang’ akiwa mikononi mwa polisi.

“Kwa hakika mtu alikuja na kufuta sehemu fulani ya rekodi ya CCTV,” alisema Bw Hassan.

IPOA iliambia kamati kuwa kwa msaada wa Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) na Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI), wanaweza kulazimisha kurejeshwa kwa diski ya CCTV iliyochukuliwa, jambo ambalo litasaidia kuwafichua wauaji wa Ojwang’.

Imefichuka kuwa OCS alimpigia simu mwanamke raia, ambaye naye alimwita fundi wa CCTV kwenda kuzima kamera.

Pia, IPOA inamtafuta mwanamume kutoka Kaunti ya Homa Bay ambaye alikuwa ndani ya seli na aliona jinsi Bw Ojwang’ alipigwa, na anaweza kuwa shahidi muhimu wa serikali katika kesi hiyo.

Chanzo hicho kilieleza kuwa mamlaka tayari imepata taarifa muhimu kutoka kwa mshukiwa mmoja aliyerekodi taarifa, akieleza jinsi maafisa wanne wa polisi walijaribu kumfanya Ojwang’ ambaye alikuwa tayari amefariki aonekane kama anaondoka akiwa hai, kwa kumbeba kwa mabega yake.

Hata hivyo, Mkurugenzi wa Upelelezi wa Jinai (DCI) Mohamed Amin aliambia kamati kuwa Bw Ojwang’ alifariki akiwa ndani ya seli, na si hospitalini kama ilivyodaiwa awali.

Kwa mujibu wa barua kutoka Hospitali ya Mbagathi iliyowasilishwa kwa DCI, maafisa wa polisi wa Kituo cha Central walimpeleka Bw Ojwang’ akiwa tayari amekufa.

Barua hiyo, iliyotiwa saini na Dkt Shah Mitari, inasema kwa sehemu: “Wakati wa uchunguzi, hakuwa na fahamu, mwili wote ulikuwa baridi na alikuwa na michubuko kwenye viungo.”

Bw Amin alisema kuwa mnamo Juni 8 saa saba na dakika 35 usiku, Bw Ojwang’ alisikika akilia kwa sauti na kupiga ukuta wa seli yake, alipokuwa peke yake.

Kulingana na taarifa kutoka kitabu cha kidijitali cha kurekodi matukio (OB) cha Kituo cha Polisi cha Central, ambayo iliwasilishwa kwa kamati na DCI, Ojwang’ alipatikana akipiga kelele wakati wa ukaguzi wa kawaida.

“Wakati huo, afisa wa zamu alitembelea seli na kupata seli zote zikiwa sawa isipokuwa ya mwisho, ambapo mshukiwa aliyekuwa peke yake alikuwa akipiga kelele sana na kupiga ukuta,” ilisema taarifa ya OB ya saa saa saba na dakika 35 iliyorekodiwa na Konstebo Mohamed Rashid Abdullahi.

Bw Amin alieleza kamati kuwa Konstebo James Mukhwana, aliyekamatwa Alhamisi, alikuwa miongoni mwa maafisa waliokuwa wakifanya ukaguzi wa seli na dakika 25 baadaye Ojwang’ alikuwa amekufa.

Jana, IPOA ilimfikisha James Mukhwana mahakamani ikiomba azuiliwe kwa siku 21 huku uchunguzi wa kifo cha mwalimu Albert Ojwang’ ukiendelea.

Mamlaka hiyo iliambia Hakimu Mkuu Mwandamizi Robinson Ondieki kwamba, Bw Mukhwana alikuwa mlinzi wa seli usiku ambao Ojwang’ alipatikana akiwa amefariki ndani ya seli ya kituo cha polisi cha Central, Nairobi.

Katika hati ya kiapo, Bw Abdirahman Jibril, mkurugenzi msaidizi anayehusika na uchunguzi katika IPOA, alisema masaibu ya Ojwang’ yaonekana yalipangwa kwa sababu Bw Mukhwana alikuwa akiwasiliana mara kwa mara na watu waliokuwa ndani na nje ya kituo cha polisi.

Aliongeza kuwa Bw Mukhwana alikuwa akiwapa taarifa watu hao, na kuna uwezekano mkubwa kwamba, yeye pamoja na wengine walio huru walihusika kumpiga Bw Ojwang’.

“Uchunguzi wa awali umebaini kuwa kuna uwezekano mkubwa kwamba mshukiwa (Mukhwana), pamoja na watu wengine ambao bado hawajakamatwa, walipanga kuharibu ushahidi wa CCTV ili kuficha kilichotokea usiku Juni 8 2025 ambapo marehemu alishambuliwa kikatili hadi kufa, kwa lengo la kuvuruga uchunguzi,” alisema Bw Jibril.

Bw Mukhwana, kupitia kwa mawakili wake Danstan Omari na Stanley Kinyanjui, alipinga ombi hilo akisema hakuna sababu za msingi za kumnyima dhamana.Mahakama itatoa uamuzi kuhusu ombi hilo Juni 20.