• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 6:55 PM
SHANGAZI AKUJIBU: Nahisi mapenzi yake kwangu yameingia baridi

SHANGAZI AKUJIBU: Nahisi mapenzi yake kwangu yameingia baridi

Na SHANGAZI SIZARINA

Mwanaume mpenzi wangu amenichanganya kwa tabia zake, sijui iwapo ananipenda au la. Siku za mwanzo za uhusiano wetu alikuwa akinipigia simu na kunitumia SMS karibu kila siku. Lakini siku za hivi majuzi ni mimi nimekuwa nikimtafuta kwa simu na mara nyingine hata anapuuza. Nimeanza kuhisi hanipendi na ni kama ninajipendekeza kwake. Nafikiria kumuacha. Naomba ushauri wako shangazi.
Kupitia SMS

Mapenzi yanapoonekana kutoka upande mmoja kamwe huwa hayana raha. Ni jambo la kushangaza kwamba awali ndiye alikuwa akikutafuta lakini sasa amekuachia mzigo huo. Inawezekana kuwa hisia zake kwako zimepungua na amekosa jinsi ya kukwambia. Ushauri wangu ni kuwa umwelezee unavyohisi kabla ya kukata kauli kuwa hakupendi.

 

Jirani amenizuzua
Shikamoo shangazi. Nina umri wa miaka 22 na nina uhusiano na msichana jirani yetu mtaani. Nampenda sana naye pia ameungama kuwa hapati usingizi kwa sababu yangu. Ajabu ni kwamba amekataa kabisa kunionyesha kwa vitendo mahaba aliyo nayo kwangu. Nifanyeje?
Kupitia SMS

Masuala ya mahaba ni kuelewana wala hayalazimishwi. Mwenzako ameungama mwenyewe kuwa anakupenda na huna shaka kuhusu hilo. Kwa sababu hiyo itakuwa vyema kwako umuelewe akikwambia hayuko tayari kwa jambo hili au lile iwapo unathamini uhusiano wenu na unataka kuudumisha. Kuwa na imani kwamba siku atakayokuwa tayari atakutimizia ombi lako.

 

Anakuja kwangu tu anapotaka pesa
Nina mpenzi lakini ninashuku kuwa hana mapenzi ya dhati kwangu nia yake ni kufaidi kutokana na pesa zangu. Sababu ni kuwa kila anapokuja kwangu akiwa na haja ya pesa nikimpa hutoweka na hurudi tu akitaka zingine. Nipe ushauri.
Kupitia SMS

Bila shaka mwanamke huyo hana mpango wowote wa uhusiano wa kudumu kati yenu iwapo hivyo ndivyo anavyofanya. Naona umefunguka na ningekuwa wewe ningejiondoa mara moja katika uhusiano huo.

Penzi letu ni la simu pekee
Shangazi natumai wewe ni mzima. Kuna mwanaume ambaye tulijuana tu kupitia kwa simu na tukapendana. Tumepanga kukutana na nina wasiwasi kwani sijui anakaa vipi, huenda nikapata kwamba maumbile yake si ya mwanaume ninayemtaka. Naomba ushauri wako.
Kupitia SMS

Sielewi ulimpenda namna gani mwanaume huyo kama hujamuona umekuwa uskisikia sauti yake tu kwa simu. Kupendana kunatokana na watu kuonana na kuzungumza ana kwa ana. Ni vyema kuwa mmepanga kukutana. Baada ya hapo utajua iwapo anakufaa. Usiwe na hofu kwani ukigundua siye unayemtaka una haki ya kumwambia ukweli huo.

 

Hataki kuniona na mwingine ingawa tuliachana
Hujambo shangazi? Nilikuwa nimeolewa lakini tukaachana. Sasa kila mwanaume huyo anaponiona na mwanaume mwingine hutishia kunipiga. Nifanye nini na simtaki tena?
Kupitia SMS

Hiyo ina maana kuwa mwanaume huyo anakutishia maisha. Kama mliachana na humtaki, hawezi kukuzuia kuendelea na maisha yako. Unafaa kumchukulia hatua ya kisheria kwa kupiga ripoti kwa polisi kwamba anakutishia maisha.

 

Nimependana na mjomba wangu
Hujambo shangazi. Mimi nimependana na mjomba wangu lakini wazazi wamepinga vikali uhusiano wetu. Ninampenda kwa moyo wangu wote na sidhani ninaweza kumuacha. Nishauri.
Kupitia SMS

Mapenzi yenu hayo ni haramu na hatari. Huwezi kamwe kuwa na uhusiano na mjomba wako kwani huyo ni sawa na baba yako. Ni lazima utii agizo la wazazi wako kwa kuvunja uhusiano huo mara moja la sivyo utajiletea laana maishani.

 

Ataka burudani tu!
Hujambo shangazi. Nimekuwa na uhusiano na mwanamume fulani kwa miezi kadhaa sasa. Nilidhani ananipenda lakini nimegundua nia yake ni kunitumia tu. Sababu ni kuwa hunitafuta tu anapohitaji asali. Ninapokuwa na shida simuoni. Nishauri.
Kupitia SMS

Hayo kamwe si mapenzi ya dhati na ni vyema umegundua mapema nia ya mwanamume huyo. Itabidi uchunguze moyo wako na kuamua kuhusu iwapo utaendelea na uhusiano huo ama utajiondoa.

You can share this post!

TAHARIRI: Serikali kupungukiwa na hela ni hatari kuu

Jombi mlevi pabaya kutukana wakweze

adminleo