Shangazi Akujibu

Nimejipata na wanaume wawili, na tayari nina mimba. Nifanyeje?

October 22nd, 2024 Kusoma ni dakika: 1

Mpenzi wangu nilipomwambia nina mimba yake aliniacha. Nimepata mwingine lakini sijamwambia hali yangu. Sasa mwenye mimba amerudi. Nichague nani kati yao?

Nitakushauri umrudie mpenzi wako aliyekupa mimba kwa sababu unamfahamu vyema kuliko huyu mwingine. Hatua yake ya kurudi ni ishara kwamba anakupenda. Kuna hatari ya huyu mwingine kukuacha akijua una mimba ya mtu mwingine.

Kuna goigoi haachi kunitumia SMS za mapenzi

Kuna mwanamume anayenitaka lakini simtaki. Sijui alivyopata namba yangu ya simu na amekuwa akinikera kwa jumbe za kimapenzi. Nifanyeje?

Itabidi umtafute mwanamume huyo umwambie wazi kuwa humpendi na kumtaka akome kukufuata. Unaweza pia kubadilisha namba yako ya simu ili kuepuka jumbe zake.

Ninampenda lakini hizi simu zanitia wasiwasi

Nina mpenzi na ninampenda kwa dhati. Kwa miaka miwili ambayo tumekuwa pamoja huwa anapigiwa simu na wanawake wengi ambao anasema ni marafiki. Nina wasiwasi.

Ni jambo la kawaida kwa mtu kuwa na marafiki, wanaume kwa wanawake. Kama hujawahi kumfumania na mmoja wao ama kusikia wakizungumzia mambo ya mapenzi, huenda ni marafiki tu. Ondoa wasiwasi.

Mpenzi wangu aliniacha akarudia Ex, inaniuma!

Nilikuwa na mpenzi lakini akaniacha akarudiana na mpenzi wake wa zamani. Bado nampenda na sijui nitafanya nini ili nimpate tena. Nipe ushauri.

Hujaelezea ni kitu gani kilichomfanya akuache na kurudiana na mpenzi wake wa awali. Kama ulimkosea na unahisi mnaweza kuzungumza akusamehe, mtafute muongee uone kama atakubali mrudiane.