SHERIA: Njia mbali mbali za kuzuia ndoa za kulazimishwa ambazo ni haramu kisheria
Ndoa za kulazimishwa bado ni changamoto kubwa nchini Kenya, hasa kwa wanawake na watoto katika baadhi ya jamii.Ndoa za kulazimishwa
Huu ni ukiukaji wa wazi wa haki za binadamu unaowanyima waathiriwa haki ya kufanya maamuzi huru kuhusu maisha yao, elimu na mustakabali wao.
Licha ya kuwepo kwa sheria kali, vitendo hivi vinaendelea kushuhudiwa katika maeneo mbalimbali ya nchi, vikichochewa na umaskini, mila potofu na ukosefu wa elimu.
Kisheria, ndoa za kulazimishwa ni haramu nchini Kenya. Katiba ya Kenya ya mwaka 2010 na Sheria ya Ndoa ya 2014 zinakataza waziwazi ndoa yoyote inayofungwa bila hiari kamili ya wahusika.
Takwimu za Utafiti wa Afya ya Uzazi na Idadi ya Watu (KDHS) zinaonyesha kuwa zaidi ya asilimia 30 ya wasichana huolewa kabla ya kufikisha umri wa miaka 18, huku baadhi yao wakilazimishwa.
Mfumo wa sheria wa Kenya unatoa njia kadhaa za kuzuia ndoa za kulazimishwa.
Miongoni mwao ni kupata agizo la mahakama kuzuia ndoa hiyo kufanyika, kuwasilisha kesi ya kuitangaza ndoa kuwa batili, pamoja na kuripoti tukio hilo kwa polisi ili hatua za jinai zichukuliwe dhidi ya wahusika. Hatua hizi ni muhimu, hasa pale ndoa inapopangwa kwa siri au kwa haraka.
Mbali na msaada wa kisheria, waathiriwa wanahimizwa kutafuta msaada kutoka kwa mashirika mbalimbali ya serikali na yasiyo ya kiserikali.
Mashirika haya hutoa huduma za ushauri nasaha, msaada wa kisheria, pamoja na hifadhi salama kwa waathiriwa wanaohepa mazingira hatari.
Wizara ya Jinsia, Tume ya Kitaifa ya Haki za Binadamu, vitengo vya ulinzi wa watoto vya polisi na mashirika ya kijamii vina nafasi muhimu katika mapambano haya.
Wataalamu wanaeleza kuwa makundi yaliyo hatarini zaidi ni wasichana na wanawake vijana, hasa kutoka familia maskini au maeneo yenye viwango vya chini vya elimu.
Dalili za onyo ni pamoja na posa za mapema, shinikizo la kihisia, vitisho au kutengwa na marafiki na familia. Kuzitambua dalili hizi mapema kunaweza kusaidia kuzuia madhara makubwa.
Adhabu kwa wanaohusika katika ndoa za kulazimishwa ni kali. Sheria inaruhusu kifungo cha hadi miaka mitano jela au kutozwa faini, ama vyote viwili.
Zaidi ya hayo, waathiriwa hupata madhara ya kihisia na kisaikolojia, huku ndoa hizi zikihusishwa pia na unyanyasaji wa nyumbani na ukatili wa kijinsia.