• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 5:50 AM
VYAMA VYA KISWAHILI: Chama cha Kiswahili katika Shule ya Upili ya St Charles Lwanga, Kitui

VYAMA VYA KISWAHILI: Chama cha Kiswahili katika Shule ya Upili ya St Charles Lwanga, Kitui

Na CHRIS ADUNGO

CHINI ya ulezi wa Mwalimu John Muli, Chama cha Kiswahili katika Shule ya Upili ya St Charles Lwanga Kitui (CHAKILWAKI) kiliasisiwa kwa nia ya kuangazia stadi nne kuu za Kusikiliza, Kuzungumza, Kusoma na Kuandika kwa kina.

Madhumuni mengine yaliyochochea kuasisiwa kwa CHAKILWAKI ni haja kubwa ya kukwamua Shule ya Upili ya St Charles Lwanga kutokana na msururu wa matokeo mabaya katika somo la Kiswahili, kubadilisha mtazamo hasi wa wanafunzi kuhusu Kiswahili, kukuza talanta za wanafunzi katika kazi za kubuni, kuzidisha maarifa ya utafiti katika Kiswahili na kushirikiana na vyama vingine ili kuboresha na kuimarisha matokeo ya KCSE Kiswahili.

Chama kina mikakati ya kushiriki makongamano mbalimbali ya Kiswahili kwa maazimio ya kuwakutanisha wanafunzi na waalimu maarufu wa Kiswahili, wanahabari na waandishi mashuhuri ambao kwa wengi ni vielelezo.

Baadhi ya wanafunzi waligundua kwamba wana udhaifu wa kujieleza kwa ufasaha kimazungumzo kwa kutumia lugha sanifu ya Kiswahili.

Mbali na hayo, chama hiki vilevile kinawapa wanafunzi fursa ya kuendesha midahalo wazi ili kuangazia masuala mbalimbali yanayofungamana na maendeleo ya jamii kwa jumla pamoja na changamoto zinazowakabili wanafunzi masomoni.

Warsha za aina hii huandaliwa ndani na nje ya shule huku uzingativu zaidi ukielekezwa katika kujadili masuala kama vile haki za watoto, matatizo yanayowakumba vijana, uongozi katika jamii na nafasi ya vijana katika kuendeleza taifa na utamaduni wa Kiswahili.

CHAKILWAKI kinanuia kuhakikisha kwamba wanafunzi wanaweza kuzungumza lugha sanifu ya Kiswahili bila ya kuathiriwa na tafsiri za moja kwa moja katika mengi ya maneno. Wanachama wanafanya juhudi za kutumia misamiati mwafaka ya Kiswahili katika kuelezea dhana zenye utata miongoni mwa watumiaji wa lugha hiyo. Uzungumzaji na Usikilizaji ni stadi ambazo wanafunzi hawa huzihitaji sana ili kuendesha mijadala yenye mantiki.

Chama hundaa vikao mara kwa mara kwa lengo la kutoa jukwaa bora kwa wanafunzi kuhamasishana, kukumbushana mambo ambayo yalifundishwa darasani na kuzamia kwa kina baadhi ya mada ambazo zinawatatiza madarasani, hasa katika somo la Kiswahili.

Aidha, wanachama huazimia haja ya kudhihirisha upekee wa vipaji vyao katika kutunga na kughani mashairi, kutegua vitendawili na hata kutamba hadithi.

Vinara wa CHAKILWAKI wana mipango ya kuhakikisha kuwa wanapata uanachama wa kila mwanafunzi shuleni hasa ikizingatiwa kwamba Kiswahili ni somo la lazima na la kutahiniwa katika kiwango cha KCSE.

Kupitia CHAKILWAKI, wanafunzi wa Shule ya Upili ya St Charles Lwanga kwa sasa wananuia kuanza kushiriki kwa wingi katika Shindano la Uandishi wa Insha linaloendeshwa na gazeti la Taifa Leo kila mwezi kuanzia Februari hadi Novemba.

You can share this post!

MAPITIO YA TUNGO: Vipawa Vya Hasina; Masimulizi...

KAULI YA MATUNDURA: Tathmini ya ufaafu wa istilahi...

adminleo