Wakulima wa Shimba Hills wakabiliana na uvamizi wa Wanyamapori
MIAKA 12 iliyopita, Mwalimu Francis Mutunga alistaafu akiwa na matumaini ya maisha ya utulivu shambani mwake katika mtaa wa Kipambani Shimba Hills, Kaunti ya Kwale.
Kwa kutumia pesa za pensheni, alianzisha mradi aliouona kama mpango wa dhahabu wa uzeeni kilimo cha nazi.
Mwalimu huyo wa zamani mwenye umri wa miaka 50, alipanda miche 400 ya nazi aina ya kisasa kwenye kipande chake cha ardhi kilichoko pembezoni mwa Hifadhi ya Kitaifa ya Shimba Hills, akiwa na imani kuwa baada ya miaka mitatu, angevuna kwa jasho lake.Lakini ndoto hiyo sasa imeporomoka kwa sababu ya uvamizi wa tembo.
“Kwa sasa nimebakisha miti 10 tu ya nazi. Tembo walingoja hadi miti ilipokomaa, wakaja usiku mmoja na kuharibu yote,” akasema Bw Mutunga huku akisimama kwenye mabaki ya mashamba yake yaliyoharibiwa.
Yeye ni mmoja wa wakulima wengi katika eneobunge la Matuga wanaosema kuwa wanyamapori wanaotoroka kutoka hifadhi ya Shimba Hills wanawaharibia mazao yao.
Baadhi ya malalamishi yao ni kuvamiwa na tembo ambao hukanyaga mimea na kung’oa miti; nyani huvamia mabanda ya kuku na kuharibu maghala ya chakula; chatu huingia manyumbani na kuwala mbwa na mbuzi; nyoka huleta tishio kwa maisha ya binadamu na mifugo.
Mita chache kutoka shamba la Bw Mutunga ni makazi ya Bw Jonathan Nzombo, ambaye naye amebakisha miti miwili pekee ya minazi.
“Sisi hatulimi tena. Ni kana kwamba sasa tunawafuga wanyama pori.Inaonekana kama KWS wameamua kuwalisha wanyama wao kwa mashamba yetu. Hakuna juhudi za kuwazuia,” akasema kwa uchungu.
Manung’uniko ya Bw Nzombo yanawakilisha kilio cha jamii nzima ya wakulima wanaoishi karibu na hifadhi hiyo.
Wanatupia lawama Shirika la Huduma kwa Wanyamapori (KWS) wakidai kuwa licha ya hasara kubwa wanazopata kila mwaka, shirika hilo halijafanya lolote kuwasaidia au kuwafidia.
“Wanatuambia tuzoee kuishi na wanyama pori. Lakini hiyo ni kejeli. Sisi ndio tunapoteza kila kitu. Tutaendeleaje kuishi?” anauliza Bw Mutunga.
Hifadhi ya Taifa ya Shimba Hills ni makazi ya wanyama wa aina mbalimbali kama vile pundamilia, tembo, nyani, nyoka na hata chui.
Ingawa ni hazina ya utalii na urithi wa asili, jamii inayozunguka hifadhi hiyo inasema inaumia kwa gharama ya kuhifadhi mazingira.
“Chatu walikula mbwa wangu. Kuku wangu walichukuliwa na nyani. Kuna tembo mmoja anayejua hata njia ya kuhepa uzio wa umeme.Nimepoteza mbuzi watatu kwa nyoka wa sumu, lakini sijawahi kufidiwa hata mara moja,” anasimulia Bw Nzombo.
Wakulima wanasema mara nyingi uzio wa umeme huzimwa bila taarifa, na wanyama hupenya kwa urahisi. Mitaro iliyochimbwa haitoshi kuwazuia, huku tembo wakionekana kuelewa mianya ya kupita.
“Tembo huingia usiku wa manane au alfajiri sana. Ni kama wanajua sehemu ya uzio iliyo dhaifu,” anasema Bw Mutunga.
Alieleza kuwa waliingia shambani mwake wakati nazi zilikuwa zimeanza kutoa maua. Baada ya miaka ya kutunza miti hiyo.
“Niliamini hatimaye naona mwanga. Halafu yote ikaharibika ghafla.”
Wakazi wanasema wameachwa na serikali, mashirika ya uhifadhi na mfumo mzima unaoonekana kuwathamini wanyama zaidi ya binadamu.
“Tunaambiwa tusiguse wanyama, tusijitetee. Lakini tukiripoti hasara au tukio, hakuna anayesaidia. Hatujawahi kulipwa fidia yoyote,” alisema Bw Nzombo.
Bw Mutunga anakumbuka safari za mara kwa mara hadi ofisi za KWS kutafuta fidia.
“Tangu nilipowasilisha dai langu la kwanza miaka minane iliyopita, bado nasubiri majibu.”
Wanakijiji wanasema hawajawahi kufaidika kwa lolote kutokana na kuishi karibu na hifadhi hiyo. Tofauti na maeneo mengine ambako jamii hunufaika na mapato ya uhifadhi kwa barabara, maji, shule au ufadhili wa masomo, wao hawajapata chochote.
“Tunasikia maeneo mengine wanapata barabara, maji, na hata basari kutoka kwa mapato ya hifadhi. Hapa kwetu hakuna lolote. Paa za shule zinavuja, hatuna hospitali, na mradi wa maji haujawahi kukamilika. Hifadhi hii inatusaidiaje?” akauliza Nzombo.
Wakulima wengine wanasema njia ya pekee ya kujilinda dhidi ya wanyama ni kukata miti.
“Wanatushutumu kwa kukata miti, lakini mimi ninalazimika kufyeka ili nyani na nyoka wasijifiche. Nikiacha msitu ukue, ninaleta majanga zaidi,” akasema Bw Mutunga.
Wakazi pia wanasema wamechoshwa na ahadi zisizotekelezwa kila mara.