Wanavyoingiza mamilioni ya pesa kwa kubinafsisha asali kulingana na mahitaji ya soko
MWAKA 2021, Anthony Mwangi alimtembelea mshirika wake wa sasa wa kibiashara, Henry Guchu, na mkebe wa asali uliokuwa mezani ulichochea wazo la uwekezaji ambalo leo hii wanajivunia.
Wawili hawa ni wanafamilia, na Mwangi alikuwa amemtembelea shemeji yake huyo ambaye ni wakili.
“Nilipofika ofisini kwa Guchu, kulikuwa na mkebe wenye asali mezani — aliniambia nilichotazama ni dhahabu,” Mwangi anakumbuka ziara hiyo.
Mazungumzo kati yao yalipelekea kuzaliwa kwa kampuni ya Kijani Honey inayojihusisha na ukusanyaji wa asali kutoka kwa wafugaji, kuichakata na kuiongeza thamani.
Guchu anasema changamoto kubwa katika sekta hii ni kupata asali iliyoafikia ubora kwa sababu ya uchakachuaji, pamoja na upungufu wa uzalishaji kukidhi mahitaji.
Kuanzia uuzaji wa tani 30 ndani ya mwaka mmoja na nusu wakati wa janga la Covid-19, mwaka wa 2020, sasa wanauza wastani wa tani 10 kila mwezi.
Walianza kwa kufanya utafiti katika maeneo mbalimbali ya nchi kama vile Ukambani, Baringo na West Pokot ili kuelewa kwa kina mtandao wa uzalishaji asali.
“Tuligundua kuwa mbali na changamoto ya ubora, pia, hatuna kiwango cha kutosha kusambaza nchi nzima,” Mwangi anasema. Kwenye safari zao walihakikisha wanabeba kifaa cha kupima ubora wa asali kinachojulikana kama refractometer.

Mwangi, kwenye mahojiano na Akilimali Dijitali alidokeza kwamba walikumbana na malalamiko mengi kuhusu asali iliyochakachuliwa – yaani kuharibiwa ubora.
“Mafunzo muhimu zaidi tuliyapata Tabora, Tanzania, ambako ufugaji nyuki umebobea,” anasema mfanyibiashara huyu.
Walianza biashara ya asali kwa tani 30 kutoka Tanzania, zilizogharimu karibu Sh14 milioni, fedha walizochangisha kutoka akiba zao binafsi.
Hata hivyo, walikumbana na changamoto za ushuru, kodi na taratibu ndefu na ghali za mpakani, huku asali waliyonunua ikichukua zaidi ya mwaka kuuzwa.
Leo hii, wakiwa na kituo cha kupokea asali na kusambaza sokoni Jamhuri Grounds, Nairobi, wamewekeza katika teknolojia ya kisasa kupima na kuchakata.
Asali hupimwa, kupashwa joto zaidi ya nyuzijoto 50°C, kuongezwa thamani na kupakiwa.
Mwangi ameelewa asali kiasi cha kujua ile bora. “Asali bora huwa na unyevuunyevu wa asilimia 17 hadi 20 na kiwango cha sukari zaidi ya 80° Brix,” anaelezea.
Brix kwenye asali hutumika kupima asilimia ya vitu vyote vinavyoyeyuka, hasa sukari, ambavyo kwa kawaida huwa kati ya nyuzi 70° hadi 88° Brix. Thamani ya juu ya Brix huashiria kiwango cha chini cha unyevuunyevu, huku asali bora kwa kawaida ikiwa kati ya 80–85° Brix.

Kuhusu suala la asali kuchakachuliwa, “Mwangi anaonya, kuchanganya asali ni hatua ya kwanza kuharibu ubora wake.”
Kijani Honey hupata asali kutoka maeneo ya Kitui, Kajiado, West Pokot, Uganda, Tanzania na DRC.
Mwangi anasema wamezamia mbinu za kutofautisha ladha na ubora kulingana na eneo, huku Ukambani akiisifia kwa kuwa na asali safi na ya Uganda ikiwa imesheheni virutubisho.
Biashara hiyo pia hubinafsisha (customize) asali kulingana na oda za wateja, na kuichakata kwa kutumia viungo kama tangawizi, mdalasini na limau.
Hali kadhalika, kwa kutumia nta (bee wax) huunda bidhaa zingine kama mishumaa, shampoo na lip balm.
Kijani Honey ikiandikisha kukua, kwa sasa inapokea asali kutoka kwa wafugaji nyuki zaidi ya 100. Licha ya changamoto za mtaji na uaminifu wa wateja, wameweza kupanua biashara yao.
“Siri yetu ni kuhakikisha upatikanaji wa asali mwaka mzima na kufanya utafiti wa mara kwa mara,” Mwangi anasema. Aidha, anasisitiza kuwa mafanikio yao yametokana na ushirikiano, uvumilivu na kuelewa mahitaji ya soko linalobadilika kila wakati.