Makala

Wito Rais Ruto alinde haki ya raia kwa mujibu wa sheria

Na RICHARD MUNGUTI June 21st, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MASHIRIKA ya kutetea haki za binadamu sasa yanatoa wito kwa Rais William Ruto kulinda haki ya raia kwa mujibu wa sheria.

Mashirika haya, Chama cha Wanasheria Nchini (LSK) pamoja na wanaharakati yameisuta serikali na kuishtaki kwa kukandamiza haki za wanananchi.

Kesi dhidi ya serikali ya Rais Ruto zilinongeshwa na kukamatwa na kuuawa kwa vijana wa Gen Z walioshiriki katika maandamano ya kupinga Sheria ya Fedha 2024/2025.

Vijana wa Gen Z waliingia bungeni katika harakati za kuharamishwa kwa Sheria hiyo.

Kufuatia uvamizi wao Rais Ruto alikataa kuitia sahihi na kutimua baadhi ya mawaziri akasalia Waziri mwenye mamlaka makuu Musalia Mudavadi.

Miongoni mwa waandamanaji zaidi ya 30 waliouawa ni pamoja na Rex Masai.

Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma aliamuru uchunguzi kubaini kilichosababisha kifo cha Rex Masai ufanywe.

Hakimu mwandamizi mahakama ya Milimani Geoffrey Onsarigo anaongoza zoezi hilo.

Uchunguzi unaendelea

Kesi nyingine zilishtakiwa na LSK, Kituo cha Sheria, Haki Afrika na Charles Njue kuhoji uhalali wa serikali kukandamiza haki za wananchi na kuuawa kwa wapinzani wa serikali.

Mbali na kuuawa kwa wanaharakati pia utekwaji nyara kwa baadhi ya wapinzani wa utawala wa Rais Ruto umekita mizizi nchini.

Mashirika haya yaliiomba mahakama kuu iamuru waliotekwa nyara wafikishwe kortini na kushtakiwa kwa makosa yaliyofanya ndipo watekwe nyara.

Pia mashirika haya yanasukuma serikali iwalipe fidia waliotekwa nyara na waliojeruhiwa na maafisa wa polisi katika harakati za kuzima maandamano.

Akikataa kuvurumisha kesi hizi za ukandamizaji wa haki za binadamu ICC Jaji Lawrence Mugambi alisema mahakama za nchi hii ziko na asasi nyingine ziko na uwezo na tajriba ya kuamua kesi hizi za ukiukaji wa haki za binadamu.

 “Nchi hii haijalemaa kiasi kwamba asasi zake haziwezi kuamua kesi za ukiukaji wa haki za binadamu ikiwa ni pamoja na utekajiu nyara wananchi na vikosi vya usalama na pia mauaji ya wananchi wakiwa mikononi mwa dola za usalama,”Jaji Mugambi alisema.

Wakili mwenye tajriba ya huu na mkongwe katika masuala ya sheria

Dkt John John Khaminwa anaomba  korti iamuru polisi waliohusika na utekaji nyara na mauaji ya wakenya wasio na hatia wachukuliwe hatua kali za sheria

Mahakama pia inaombwa na walalamishi iamuru serikali itoe majina na idadi ya watu waliotoweka na waliokufa wakiwa wamezuiliwa na polisi.

“Nchi hii iko na asasi za kushughulikia visa vya utekaji nyara na mauaji ya wananchi wakiwa mikononi mwa maafisa wa usalama. Kesi hizi zitaamuliwa humu nchini. Ombi hili halina mashiko kisheria,” Jaji Mugambi alisema.

Na wakati huo huo Jaji Mugambi aliagiza kwamba visa vyote vya wananchi kutekwa nyara , mauaji ya waliotekwa nyara na wale waliopata majeraha wakiwa mikononi mwa polisi vichunguzwe na mamlaka huru ya kusimamia polisi (IPOA).

Jaji huyo alisema maafisa wa polisi hawawezi kujichunguza wenyewe.

Kufuatia uamuzi huo, sasa maafisa wa polisi na maafisa kutoka kitengo cha uchuguzi wa jinai (DCI) hawatakuwa wanachunguza visa vya utekaji nyara.

“Haki haitapatikana iwapo makachero, polisi ama maafisa wa DCI watajichunguza wenyewe,” Jaji Mugambi alisema.

Jaji huyo aliamuru kesi tatu zilizowasilishwa na LSK, Kituo cha Sheria na Charles zikidai kwamba mahakama na asasi za usalama za humu nchini hazitatenda haki kwa wahasiriwa wa utekwaji nyara na mauaji ya wananchi na dola za kiusalama ziamuliwe humu nchini.

Kituo cha Sheria kinalalamika maafisa wa DCI na wale wa kitengo cha masuala ya ndani wizara ya usalama wa kitaifa (IAU) zimeshindwa kudhibiti uhalifu kutekelezwa na maafisa wa kikosi cha polisi.

Jaji huyo ameagiza asasi za humu nchini zilizobuniwa kwa mujibu wa Katibu ya 2010 zitekeleze majukumu yao pasipo ubaguzi wowote.