Wito serikali iwaokoe Wakenya waliokwama katika mataifa ya Mashariki ya Kati mapigano yakichacha
VUGUVUGU la kutetea Haki za Binadamu Mtetezi limekosoa vikali serikali kwa kushindwa kuchukua hatua madhubuti kulinda maelfu ya Wakenya wanaofanya kazi katika mataifa ya Mashariki ya Kati huku mzozo ukiendelea katika eneo hilo.
Akizungumza na Taifa Dijitali, Mkurugenzi wa vuguvugu hilo, Francis Awino alisema kuwa zaidi ya Wakenya 500,000 wanaofanya kazi katika eneo hilo wako hatarini huku familia zao nchini zikiishi kwa hofu kutokana na ukosefu wa taarifa rasmi kuhusu usalama wao.
“Serikali chini ya Rais William Ruto iliwapeleka vijana wengi kutafuta ajira nje ya nchi kupitia mpango wa Kazi Majuu, uliotangazwa kama suluhisho la ukosefu wa ajira nchini. Waziri wa Leba Alfred Mutua aliendesha kampeni za uajiri na ushirikiano na waajiri kutoka Ghuba, akiwahakikishia Wakenya kuwa ajira hizo zilikuwa salama na zimeidhinishwa na serikali,” akasema Bw Awino.
Hata hivyo, anadai kuwa serikali imewatelekeza Wakenya hao.

“Wananchi walihimizwa kwenda kufanya kazi nje ya nchi kwa ahadi kuwa serikali ingewalinda. Leo hii wako katika eneo la vita bila mpango wowote wa kuwaokoa,” aliongeza Bw Awino.
Shirika hilo pia lilimkosoa Mkuu na Waziri Musalia Mudavadi kwa kauli kwamba Wakenya walioko Mashariki ya Kati warejee nyumbani kwa gharama zao wenyewe, likisema hatua hiyo ni ya “kutojali na kukiuka wajibu wa serikali kwa raia wake.”
Kwa mujibu wa Bw Awino, familia nyingi nchini zinategemea mitandao ya kijamii na taarifa zisizothibitishwa kujua hali ya wapendwa wao, hali inayoongeza wasiwasi na mateso ya kisaikolojia.
“Tunampa serikali makataa ya siku tatu kuchukua hatua madhubuti. Iwapo haitafanya hivyo, tutapanga maandamano makubwa kudai uwajibikaji,” alisema Bw Awino.