MAONI: Uhasama wa Oburu na Orengo hautafaidi wakazi wa Nyanza
UHASAMA kati ya Kiongozi wa ODM Dkt Oburu Oginga na Gavana wa Siaya James Orengo hautasaidia kwa vyovyote iwapo eneo la Luo Nyanza halitapata miradi ya maendeleo.
Kwa muda sasa wanasiasa hawa wawili wamekuwa wakivutana na kujibizana vikali kiasi kwamba wafuasi wao wanakabiliana kwenye hafla mbalimbali Nyanza.
Wikendi Gavana Orengo alifurushwa kwenye mazishi eneobunge la Seme na watu ambao hawachangamkii msimamo wake wa kuegemea mrengo wa Linda Mwananchi.
Bw Orengo amekuwa na uhasama na Dkt Oginga tangu mauti ya marehemu Raila Odinga viongozi hao wawili wakizozonia chama cha ODM.
Dkt Oginga aliteuliwa na kuidhinishwa na wajumbe kwenye Kongamano Spesheli la ODM lililoandaliwa mnamo Februari.
Kwa upande mwingine, Bw Orengo amejitangaza kiongozi mpya wa ODM akisema kwamba Dkt Oginga hatoshi mboga.
Mwanzo, Kenya ni taifa la kidemokrasia na vijana kutumika kuzua ghasia ni jambo ambalo halifai hata kidogo.
Kwa hivyo, viongozi wa Linda Ground na wale wa Linda Mwananchi wanastahili kukomesha tabia hii.
Wikendi familia ya Mbunge wa Seme James Nyikal haikuomboleza baba yao kwa staha kutokana na fujo na uhuni ambao uliandamana na cheche kali za kisiasa.
Dkt Oburu na Bw Orengo wanapolumbana, swali ni wananchi wananufaika vipi? Ukweli ni kwamba raia ndio wataamua nani ni kiongozi wao kupitia miradi ya maendeleo.
Linda Ground anayoiongoza Dkt Oburu inastahili kutumia uhusiano wake na serikali kuhakikisha kuwa miradi iliyoanzishwa Luo Nyanza inakamilishwa kwa wakati.
Baadhi ya miradi ilizinduliwa ndio lakini inaenda kwa mwendo wa kasi na kusababisha raia wazue maswali kuhusu utendakazi wa serikali.
Changamoto ambazo wakazi wa eneo hili wanapitia, ndizo pia zinakabili maeneo mengine.
Hata hivyo, viongozi wa Linda Ground Nyanza wanasawiri eneo hilo kama mbingu na isiyokuwa na changamoto zozote.
Dkt Oginga na viongozi wenzake wafahamu kuwa siasa za Serikali Jumuishi na ‘Tutam’ zitanoga tu iwapo wananchi watahisi kuna maendeleo.
Bw Orengo naye anastahili kukoma kusumbua na siasa zake za ubabe kwa sababu hata akiwa mbabe wa siasa za Nyanza na raia wawe na njaa, hatakuwa amesuluhisha chochote.
Tangu miaka ya 80 na 90, Bw Orengo, 75 amekuwa akijisawiri kama mwanaharakati na mwanamageuzi.
Hata hivyo, hafai kujisawiri kama anayepinga maendeleo ambayo yanaletwa Nyanza kwa sababu tu ya kutaka udhibiti wa chama cha ODM.
Hata Bw Orengo akiishia kuwa kiongozi wa ODM, itakuwa vigumu kwake kutamba kwenye siasa za kitaifa kwa sababu hana umaarufu kama Raila Odinga.
Kile ambacho gavana huyu anafanya ni kama alivyotenda baada ya mauti ya Jaramogi Oginga Odinga mnamo 1994.
Baada ya kifo hicho, Bw Orengo aliungana na marehemu Kijana Wamalwa kupinga azma ya Raila ya kutwaa uongozi wa Ford Kenya.
Mwishowe Raila aligura na kuunda NDP kisha kutwaa udhibiti wa siasa za Luo Nyanza. Kwa hivyo, Bw Orengo kupinga familia ya Bw Odinga haijaanza leo.
Licha ya siasa hizi kali, mirengo ya Dkt Oburu na Bw Orengo inastahili kujiepusha na siasa kali ambazo hazimfaidi mwananchi.