MAONI: Usidai maendeleo iwapo utakula hela za wanasiasa
HAKUNA haja ya raia kulalamika kwamba hawapati maendeleo au ahadi zilizotolewa wakati wa kampeni hazitimizwi iwapo watabobea katika kuchukua hela kutoka kwa viongozi wa kisiasa.
Kampeni za uchaguzi wa 2027 zinapoendelea kupamba moto katika maeneo mbalimbali nchini, wawaniaji wamekuwa wakiandaa mikutano ambapo raia huwasikiliza wakinadi sera.
Mara nyingi wakati ambapo viongozi hufika katika mkutano wa kisiasa na kuna mkusanyiko wa umma, wengi wa raia wanapiga tu makofi wala hawamakinikii kile kinachosemwa.
Baada ya mkutano kukamilika, utawapata raia wakiwa wamepanga foleni wakisubiri kupewa Sh200, Sh300 au hata Sh500 kisha wanajiendea zao.
Mwanzo, hii ni tabia ambayo sasa ni kama ya lazima, ni kama kuwahonga wapigakura wamchague kiongozi fulani kwa sababu ya mfuko wake mzito.
Tabia hii sasa imekita mizizi katika maeneo mbalimbali nchini ambapo viongozi sasa wanashindana kutoa pesa huku wananchi wenyewe wakizitia mfukoni na kutabasamu.
Katika Kaunti ya Kisumu, kwa mfano, kumekuwa na ushindani mkali kwa wanaosaka kiti cha ugavana ambapo viongozi sita waliochaguliwa wanamezea mate kiti hicho.
Viongozi hao wamekuwa wakizunguka kaunti hiyo kila wakati wakiwarai raia wawachague mnamo 2027.
Kinaya ni kuwa baadhi husema hadharani kuwa wamekuja na pesa chekwachekwa wala hadhira yao haifai kuingiwa na wasiwasi kwa kuwa watarejea nyumbani wakiwa njaa.
Kinachoshangaza zaidi ni kuwa baadhi ya raia sasa wameanza kuingiwa na kiburi wakisema kuwa hawataki Sh200 tena eti kwa sababu kiongozi fulani huwapa Sh500 au Sh1,000.
Iwapo hali itaendelea hivi basi Wakenya hawafai kuwalaumu viongozi wanaoingia madarakani kwa kutowapa miradi ya maendeleo.
Hii ni kwa sababu, iwapo kila mmoja atahudhuria mkutano wa kisiasa kisha apewe Sh1000 na wanaofika mkutanoni ni zaidi ya 5000 basi hizo ni Sh5 milioni ambazo zimetumika.
Kama mwanasiasa anatumia Sh5 milioni kwenye kampeni kwa siku au hata siku mbili kabla ya kujumuisha gharama nyingine, basi hapo lazima kama mpigakura ujiulize swali. Je pesa hizi amezitoa wapi?
Iwapo pesa hizo zimetoka mfukoni mwake basi bila shaka atazirejesha akiwahi kiti kama ugavana ambapo anasimamia matumizi ya mabilioni ya fedha.
Ukweli ni kwamba baada ya mwanasiasa kutumia hela nyingi wakati wa kampeni, akiingia tu atatumia kila njia ikiwemo kusajili kampuni kupitia marafiki kunufaikia hela za kaunti.
Je, uwajibikaji utatokea wapi iwapo hali itakuwa hivi? Atatekeleza kivipi miradi ya maendeleo iwapo umakinifu wake ni kurejesha hela ambazo alizitumia kuwahonga wapigakura?
Msimu huu wa kampeni, ni vyema wananchi waongozwe na hekima hata wanapokula pesa za wanasiasa. Baadhi ya viongozi wamekuwa madarakani miaka nenda miaka rudi na rekodi yao ya maendeleo ni duni.
Hawa ndio utawapata sasa wanasaka ugavana na kutumia kitita kikubwa kuwahonga wapigakura na haitashangaza wakirejeshwa madarakani.
Hii kauli kwamba mwanasiasa akija na pesa ule kisha uamue kwa hekima debeni haina hekima ndani yake.
Iwapo kiongozi amekuwa madarakani na utendakazi wake umekuwa duni, raia waonyeshe ukakamavu na wamkatae pamoja na pesa zake.
Kama wapigakura watakula hela za wanasiasa wote bila kujali basi uchaguzi ukiisha wasiwe wepesi wa kuitisha mradi usiotekelezwa.