Habari Mseto

Masaibu ya wanafunzi wa chekechea wanaofaa kutunzwa kama mayai

January 26th, 2024 2 min read

NA WANDERI KAMAU

SERIKALI ya Kaunti ya Nyandarua mnamo Alhamisi iliwatuma mafundi kukarabati shule ya chekechea ya Shakora, iliyoko eneo la Ngorika, baada ya wakazi kulalamikia hali yake mbaya.

Vyombo vya habari pia viliangazia hali mbaya ya shule hiyo, hali iliyowalazimu wazazi kutoka eneo hilo kuwahamisha wana wao na kuwapeleka katika shule nyingine.

Ni wanafunzi watatu tu waliokuwa wameachwa kwenye jengo hilo, lililoonekana kuwa mahame.

Kabla ya mafundi hao kufika, wanafunzi walikuwa wakilazimika kuvumilia baridi kali, kwani milango, madirisha na hata sakafu hazikuwa zimekamilika kujengwa.

“Nililazimika kumwondoa mtoto wangu kwa kuhofia hali yake ya afya. Hili ni eneo lenye baridi. Hali ya darasa hilo inahatarisha afya yao zaidi, kwani wanafunzi wengi hutoka nyumbani mapema,” akasema Bi Gloria Gathungu, ambaye ni mkazi wa eneo hilo.

Wazazi wengine waliwalaumu maafisa waliokuwa wakisimamia ujenzi huo kwa “kufanya kazi ovyo”.

“Maafisa hao walifaa kufahamu kuwa shule hii ni muhimu kwa eneo hili, kwani hakuna nyingine iliyo karibu. Pili, hili ni eneo la baridi, kwani liko karibu na Milima ya Aberdares,” akasema mzazi mwingine, aliyetambulika kama Wangui.

Hata hivyo, wazazi hao walionekana kuridhishwa na hatua ya kaunti kuwatuma mafundi kukamilisha ujenzi huo, wakisema hilo litawapunguzia pakubwa mzigo wa kuwapeleka wana wao katika chechechea zilizo mbali sana.

“Hatimaye tumepata afueni, japo hilo linafaa kuwa changamoto kwa serikali ya kaunti kuhakikisha kuwa shule zote za chekechea ziko katika hali nzuri, kwani ni jukumu lake kusimamia elimu ya msingi,” akaeleza mzazi mwingine.

Kwenye taarifa, kitengo cha mawasiliano katika kaunti hiyo kilisema mafundi wa serikali hiyo wataanza kuzuru kila wadi kuhakikisha kuwa shule zote za chekechea ziko katika hali nzuri.

 

Mwonekano wa Shule ya Shakora kutoka nje. PICHA | WANDERI KAMAU

Tukio la shule hiyo linaibua kumbukumbu za masaibu tele wanayopitia wanafunzi wa shule za chekechea.

Mwanzo ni wadogo kiumri na hivyo, huhitaji kutunzwa kama mayai.

Lakini miundomsingu mibovu na isiyo ya kutosha katika shule nyingi nchini hufanya baadhi ya wanafunzi wa chekechea kusomea chini ya miti kwenye kijibaridi kikali.

Watoto wengine hukaa chini sakafuni ama kwa simiti au sakafu iliyotengenezwa kwa kuboma kutumia samadi. Hao hulazimika kuvumilia vumbi.

Wataalamu wa elimu wanasema mazingira mazuri huamsha ari ya mwanafunzi kusoma.