Mashairi

Chungwa ni la nani?

February 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 6

Kuna swali nauliza, naomba lenu jawabu,
Moyo limenilemaza, mwenzenu nina kurubu,
Angani ninaangaza, kitwani nina sulubu,
Hilo chungwa ni la nani, mbona mwaling’ang’ania ?

Lienda zake Odinga, tukabaki njia panda,
Kisha Oburu Oginga, kalidaka hilo tunda,
Naye mwanawe Odinga, mchungwa akaupanda,
Hilo chungwa ni la nani, mbona mwaling’ang’ania?

Leo walipigania, eti kila mtu lake,
Oburu ajivutia, asema chungwa ni lake,
Na Winni hajatulia, eti mali ya babake,
Hilo chungwa ni la nani, mbona mwaling’ang’ania?

Mahasidi mesogea, karibu na chungwa hilo,
Mate wanalimezea, wasema liwe liwalo,
Mtini wanaukwea, kulichuma chungwa hilo,
Hilo chungwa ni la nani, mbona mwaling’ang’ania?

Kama ni lake Winiye, mbona msimkabidhi,
Mbona nanyi mliliye , mwenyewe linamuudhi
Kisha nanyi hatimaye, kajuweni yenu hadhi,
Hilo chungwa ni la nani, mbona mwaling’ang’ania?

Mpeni basi Oburu, kama la kwake hakika,
Mzee ahisi huru, aache kusononeka,
Cha nduye ni uhuru, yeye anapokiteka,
Hilo chungwa ni la nani, mbona mwaling’ang’ania?

DOMIANO ADIBA ONYANGO.
MALENGA ADIBA JINA KUBWA
BUDALANGI, BUSIA

Na bado

Mwilio kama wasema, un’fifia sauti,
Kero la utu uzima, ukishafika wakati,
Ngoja na mwili kupuma, nyonga na hata magoti,
Huna ghera huna mati.

Tumbolo litaroroma, ingawa halisokoti,
Lifuriane ja ngoma, huwezi hata kuketi,
Kiambiwa kusimama, utaanza ati ati,
Huna ghera huna mati.

Mato huwezi kusoma, mato hayaoni khati,
Yana ukungu daima, waona kana mangati,
Utabaki na lawama, na msaada hupati,
Huna ghera huna mati.

Kikwita mwana halima, ukamlishe visheti,
Akuhisi mume mwema, mwenye nguvuze na dhati,
Baba washikwa na homa, wakucha kupiga goti,
Huna ghera huna mati.

Yankwisha machachanjama, wala huna mikakati,
Si wawali si wasima, riyahi hazikuwati,
Mbwakuonewa huruma, ukisubiri mauti,
Huna ghera huna mati.

Twaambiwa sikilema, uzee na wenye n’ti,
Mimi hilo kilipima, naona kuna ghalati,
Wala pia siuzima, zikishaanza laiti,
Huna ghera huna mati.

Hapa basi n’takoma, yatosha yano katiti,
Uzee una zahama, na usingizi hupati,

Hata na huko kusema, utawekewa shuruti,
Huna ghera huna mati.

MUHAMMAD OMAR CHETEZO
MALINDI

Mama utapona

Jinsi unavyosonona, moyoni ukiumia,
N’namuomba Rabbana, maumivu yatasia,
Usikerwe kama jana, kitandani ukilia,
Tulia mama tulia, usilie utapona.

Mwili unavyokuchana, na miguu kuumia,
Mwanao uwezo sina, ila mungu namwachia,
Akuponye uwe tena, mzima wa kuridhia,
Tulia mama tulia, usilie utapona.

N’najua raha huna, mawazo yakuzidia,
Kila unapojiona, wazoroteka afia,
Ila mama tulizana, tumuachie jalia,
Tulia mama tulia, usilie utapona.

Mwili mzima hauna, salama ukatulia,
Hata na macho kuona, nuru yako yafifia,
Viungo vyote vyaguna, havitaki kutulia,
Tulia mama tulia, usilie utapona.

N’najua wangu nina, hulali ukatulia,
Kila dakika waguna, huwezi ukasinzia,
Hata mamangu waona, inakutesa dunia,
Tulia mama tulia, usilie utapona.

Hata kule kutafuna, chakula unaumia,
Na maono pia huna, zimekutoka hisia,
Nalijua hilo sana, sio nakunyamazia,
Tulia mama tulia, usilie utapona.

Jinsi unakunjamana, mamangu n’nakwambia,
Mjuzi ni maulana, mengi utayapitia,

Ya kupwaya na kubana, ya dhamira na ya nia,
Tulia mama tulia, usilie utapona.

Mimi nakupenda sana, n’nakuomba sikia,
Huku kufa na kupona, ni agizo la jalia,
Lakini waja hatuna, uwezo wa kuzuia,
Tulia mama tulia, usilie utapona.

Uzee umekubana, mengi unayapitia,
Ndivyo hivyo Albina, hujafa hujatulia,
Unasinywa unanuna, na maradhi yakwingia,
Tulia mama tulia, usilie utapona.

Amina Rabbi Amina, Rabbi Amina Jalia,
N’namuomba Rabbana, ikurudie afia,
Ukae ucheke tena, usiwe wachiachia,
Tulia mama tulia, usilie utapona.

LUDOVICK MBOGHOLI
AL – USTADH – LUQMAN
NGARIBA MLUMBI (006)

Amka mama

Imetosha sasa Congo, usingizi ulolala,
Amuka acha maringo, utupe hata chakula,
Rauka na zako bongo, tetee lako kabila,
Umelala sana mama, amka ututetee.

Chudere wako Lumumba, alitahidi kwamusha,
Akanguruma ja simba, hajetu kukujulisha,
Ukaona ni kasumba, asehitaji mkesha,
Umelala sana mama, amka ututetee.

Ni wapambe wako mama, mbaroni walitutia,
Wakaja kwako kusema, eti wametukomboa,
Ndo usije kulalama, wanako tukijutia,
Umelala sana mama, amka ututetee.

Amuka utakumbuka, nasaha ulotupea,
Tujafa tujaumbika, ya nini kujichukia,
Wa kwetu wakianguka, mbona tunasherekea,
Umelala sana mama, amka ututetee.

Vipi mama usihisi, harubu na tabu zetu,
Mbona huna wasiwasi, likatwapo tumbo letu,
Lini tawa na kisasi, na wavunjao galetu,
Umelala sana mama, amka ututetee.

Sitokatia hukumu, amesema baba Mungu,
Ila mwana chakaramu, natoa moyoni mwangu,
Utakwenda jehanamu, ukizidi mama yangu,
Umelala sana mama, amka ututetee.

ALLAN CHENGE
SHULE YA UPILI YA KACHIENG’
KABKARA, BUNGOMA

Bungoma hoyee!

Jukwaani naingia, habari njema naleta,
Bungoma tumeamua, viongozi kuwaleta,
Afisini wametua ,nani huyo anateta?,
Walimu kiboko chao, wenye wivu wajinyonge!

Luketelo kiongozi, walimu wameamua,
Tena ni mchapa kazi, na sasa wamechagua,
Sera zake ziko wazi, kazi atatufanyia,
Luketelo ndiye Simba, tayari ananguruma!

Hongera bwana Walela, kuwakilisha junia,
Sasa hakuna kulala, walimu twajivunia,
Kahutini tuko jela, walimu tunaumia,
Walela atatulea,tayari ameonesha!

Asante kaka Busolo, ni naibu mwenyekiti,
Ufahamu Jambo hilo ,tunakupenda lusweti,
Tongareni tuna kilo, tumekupa nacho cheti,
Busolo ni baba lao ,walimu tumekubali!

Simba jike la Bungoma ni chaguo la walimu,
Fei wafula ni noma, Sisi sote twafahamu,
Hela zetu ni salama , Fei tunakuheshimu,
Wafula chaguo bora ,hela zetu atachunga!

Kunaye Linda Wekesa, huyu binti ni shupavu,
Tulimpiga na msasa, maono yake mabivu,
Tunatabasamu sasa, ongoza kwa utulivu,
Linda wekesa hongera, timiza maono yako!

Bingwa Anodi Nyongesa, wala sijakusahau,
Debeni uliwatesa, tambulika kwa wadau,

Zidisha bidii sasa, utayala malimau,
Anodi mchapa kazi,walimu wajivunia!

Ni tamati nimefika, nimesema ya muhimu,
Nenda zangu pumzika,imeisha yangu zamu,
Nawaombea baraka, nyote nyie wakarimu,
Viongozi tumepata, Bungoma twajivunia!

KAKA KULE,
AUGUSTINE KULECHO,
LUKHUNA-TONGAREN

Hakitoshi

Nusu mfuto sipishi, kichachu hakiwi tamu,
Chakula hakishibishi, kipimo kisipo timu,
Nateseka ningaishi, maisha yangu magumu,
N’patacho hakitoshi!

N’nenalo siubishi, moyo umengia hamu,
N’tendapo sinyooshi, n’kapumua ghulamu,
Dau langu halivushi, matundu kila sehemu,
N’patacho hakitoshi!

Shida huja kama moshi, kunipaliza mwalimu,
Hapa pataka uashi, wana wataka ilimu,
Ningajipinda hayeshi, hazitoshi darahimu,
N’patacho hakitoshi!

Jamani hili sighushi, ndugu zangu mahashumu,
Msinione mzushi, bure mkanituhumu,
Faradhi pia sifishi, mahitaji hayatimu,
N’patacho hakitoshi!

Mwaka hwisha sizalishi, hata ubae wa ndimu,
N’patacho hakifishi, kuondoa majukumu,
Lawama nazo hazishi, meondoka hitiramu,
N’patacho hakitoshi!

Nafusi yanishawishi, “tenda japo ni haramu”
Kukamilisha utashi, nile nyali kwa “lahamu”
N’siteseke bilashi, n’kashindwa kujikimu,
N’patacho hakitoshi!

Sizimi wala siwashi, najihisi madhulumu,
Haramu sihalalishi, sisawa kwa isilamu,

N’tendeni wafatishi, mlo jaliwa fahamu?
N’patacho hakitoshi!

USTADH MUHAMMAD ABDALLAH (CHETEZO)
“MKINAMLUNDE”
MWANATI WA AFRIKA MASHARIKI
MALINDI

Siutangui udhu

Nilikosa pale mwanzo, nikachezea najisi,
Kumbe kile ndicho chanzo, cha mimi kuwa muasi,
Nimeshalipata funzo, vivi nimesema basi,
Nimeshatawadha tena, sasa sitangui udhu.

Nilihisi ni mchezo, wa kuupoteza muda,
Kumbe navunja vigezo, kujitia kwenye shida,
Ela sasa ni mtuzo, kutulia kuwe ada,
Nimeshatawadha tena, sasa sitangui udhu.

Wallahi najiapiza, udhu sitangui tena,
Huno naubembeleza, mashuzi nitayabana,
Sitaki kuupoteza, nitamakinika sana,
Nimeshatawadha tena, sasa sitangui udhu.

Kuutanguwa sitaki, hunu hunu wanifaa,
Vizuri kuumiliki, najivika ushujaa,
Ni nao haunitoki, kutangua nakataa,
Nimeshatawadha tena, sasa sitangui udhu.

Ilikuwa si rahisi, kutawadha na baridi,
Kwa wingi wa wasi wasi, kutetema kukazidi,
Hivi narudia basi, sitangui wa Hamadi,
Nimeshatawadha tena, sasa sitangui udhu.

Kaditama udhu wangu, n’na nao umakini,
Hadi ile siku yangu, kugeuzwa kitandani,
Namaliza neno langu, aniongoze Manani,
Nimeshatawadha tena, sasa sitangui udhu.

HAMZA AR-RIYAM
(MJUKUU WA RIYAMY- MWANA WA MJANE)
SAYARI YA BUSARA
MOMBASA

Hiyo mimba si yangu!

Nimezipata habari, zimenitia uchungu,
Wala sikuwa na ari, ya kutunga ndugu zangu,
Na vyenye ulibashiri, eti una mimba yangu,
Hiyo mimba sio yangu, itafutie mwenyewe!

Tulifanya siku moja ,kile kimoja cha chali,
Iweje unanitaja, ilo siwezi kubali,
Kama umekosa hoja, sitaki unikejeli,
Iyo mimba sio yangu, itafutie mwenyewe!

Nilizipata fununu, ulitembea na Joni,
Wambie watu wa kwenu, wanitoe midomoni,
Nikishakata rununu, usipige abadani,
Iyo mimba sio yangu, itafutie mwenyewe!

Kitu cha kukitabiri, hakinao uhakika,
Kwa hiyo yako sitori ,ninaipinga haraka,
Na tuachane kwa kheri, sizitaki patashika,
Iyo mimba sio yangu, itafutie mwenyewe!

Sana likupeleleza, si leo tangu mwanzoni,
Tamaa uliijaza, wapenda hadi vipeni,
Ndo mimba wakakujaza, kwangu waileteani,
Iyo mimba sio yangu, itafutie mwenyewe!

Naweka msisitizo, na tena unisikie,
Hayo yako maelezo, kwangu usiniletee,
Usitokee mzozo, maovu nijiwazie,
Iyo mimba sio yangu, itafutie mwenyewe!

ONESMUS KATANA
MALENGA MSIKIVU
KILIFI

Bustani ya mahusiano

Moyo kama bustani, ondoa yote magugu,
Kusiwe za nuksani, maradhi yaliyosugu,
Ama watu kufitini, hadaifu kama pwagu,
Uwe hadithi ya mema, timazi uelekevu,

Kiunga unapolima, upandacho ni hiari,
Mbuyu mti tuhuma, vyungani hamna kheri,
Mwaridi mkono fuma, sura kufwata ghururi,
Uwe hadithi ya mema, timazi uelekevu,

Mema unapowazia, kama miche ilochanga,
Dhamiri safi kazia, ifwate ni yako tanga,
Kama meli baharia, ni dira inavyozinga,
Uwe hadithi ya mema, timazi uelekevu,

Wapi pate rutubisho, mahusiano nawiri,
Ndugu awe hakikisho, mikataba ukafiri,
Hiana sasa utisho, machukizo kusawiri,
Uwe hadithi ya mema, timazi uelekevu,

Kaditama wa tamati, hoja sijamalizia,
Usiku wa katikati, ni chini yende pazia,
Kosa sasa silifuti, kazi kwenu kubakia,
Uwe hadithi ya mema, timazi uelekevu,

JUMA OKAL,
MALENGA USTADH,
MIGORI

Hujafeli mtihani

Mwanangu nisikilize, baba yako nakurai,
Bora katu sijibeze, na kujiona hufai,
Hata hasi usiwaze, wewe ni bingwa jidai,
Kuifeli mitihani, si kufeli maishani.

Alama hizo ni zako, zipokee ufurahi,
Sijipunguze ni mwiko, nafsio istahi,
Na kuko huko uliko, weye bora na sahihi,
Kuifeli mitihani, si kufeli maishani.

Ujipe moyo mwanangu, sio mwisho wa maisha,
Usijitiye machungu, kona dunia kaisha,
Elimu si kifo tangu, walofeli wanabisha,
Kuifeli mitihani, si kufeli maishani.

Usijinyime sururi, ambaa wano ghururi,
Na wenye alama nzuri, nyote mengi yasubiri,
Penda wenye ushauri, wenye wema sio siri,
Kuifeli mitihani, si kufeli maishani.

Na maisha ni karata, udhaniye ndiye siye,
Katu usije kusita, juhudi ukumbatiye,
Na bahati ukipata, Jalali umsifiye,
Kuifeli mitihani, si kufeli maishani.

Tafuta chako kipawa, na kwacho ukajituma,
Kikuze utajaliwa, maisha ukasimama,
Ukimbiaji ni sawa, ama pia ukulima,
Kuifeli mitihani, si kufeli maishani.

Wengi wetu wasanii, twachora pia twaimba,
Wengine vinyago nui, uchongaji wametamba,

Sisahau wangu bui, kwa ufundi hapa simba,
Kuifeli mitihani, si kufeli maishani.

Kaditama sikiliza, kipaji chako tambua,
Nami nitajikaza, matilaba kupatia,
Maishani takutuza, omba Jalali jalia,
Kuifeli mitihani, si kufeli maishani.

CHRISTOPHER MUSA KALUNDA
MALENGA MWEPESI
AIC VISA OSHWAL-KABARNET