Wahenga hawaamini
Kumbe pia mashujaa, hupoteza ujasiri,
Wakabaki kuzubaa, inapozidi hatari,
Mili yao hulemaa, huwaishia kiburi,
Kumbe pwagu duniani, nae upata pwaguzi.
Wanajeshi hukomaa, kwa mazoezi makali,
Ujuzi wakachukua, wakapewa na vibali,
Nao hufika hatua, wakashindwa kuhimili,
Wakapata majangili, vishinde na makatili.
Wavumilivu wa hali, tulowajuwa kitambo,
Wenye vifua vya ghali, kutusitiria mambo,
Nao hufika mahali,wakawa na masimango,
Kweli umdhaniae, sie katu maishani.
Bwana mpanda membari, na kuhusia umati,
Gwiji na tena hodari, mashallahu kwa sauti,
Siri tena sio siri, amefumaniwa gesti,
Ulimwengu wa uzinzi, peupe twahazirika.
Oneni hino stori, ya kaka mvaa suti ,
Kwakufeki utajiri, na magari tofauti,
Ni mtu wa diridiri, kumbe analiwa buti,
Leo siri imevuja, ni mtu wa sim tuu.S
RISALATY SWALEH MWALOMBA
Kuolewa
Mutafutao waume, ili kupata sitara,
Kupangarara kukome, zituwe zenu fikira,
Msishakizwe na tume, mkazowa matambara,
Kuolewa si ajira.
Hamumu huja kwa shime, ikaathiri busara,
Hukusomba usipime, panajisi na twahara,
Majuto yaje kinyume, yakikupata madhara,
Kuolewa si ajira.
Jitulize kwenye ngome, usiwe wakuzurura,
Kwa babaako na mame, walokuzaa kwa ghera,
Acha sifazo zivume, siitafute izara,
Kuolewa si ajira.
Aliye m’mwanamume, dini, tabia na sera,
Kwenu aje angurume, alete posa jahara,
Wazazio wamsome, yumume ama taira?
Kuolewa si ajira.
Kwenye mahaba sizame, huba kukuteka nyara,
Ujitafutie mume, kwa kuvutiwa na sura,
Wengine m’paka shume, wako na simba marara,
Kuolewa si ajira.
Akonyezae mnyime, mwanamwali mbwa kujera,
Sikubali msukume, linda wako ubikira,
Joto la uwi lizime, tuwa ungoje kudura,
Kuolewa si ajira.
Bahari chafu si zame, utangaziwe ujura,
Mji binti ukuseme, uambiwe umkora,
Utamani upahame, uishipo kupagura,
Kuolewa si ajira.
Iwa mwekevu mwatime, tulia acha papara,
Sipapie uangame, kila mtu mekudara,
Kisha uje ulalame, kila mtu kumzira,
Kuolewa si ajira.
USTADH MUHAMMAD ABDALLAH (CHETEZO)
“MKINAMLUNDE”
MWANATI WA AFRIKA MASHARIKI
MALINDI
Makiwa Sandichi
Kwa uwezo wa Rabuka, Mola wetu wa mbinguni,
Shairi naliandika, japo ninao huzuni,
Matozi yananishuka, ndia mbili mashavuni,
Makiwa ndugu Sandichi, kwa kumpoteza mama.
Ujumbe ulipofika, ulotuma kikashani,
Kusema wahuzunika, umekuvama huzuni,
Mtima uliatuka, nikashindwa kuamini,
Makiwa ndugu Sandichi, kwa kumpoteza mama.
Najua wasononeka, kukosa raha moyoni,
Mama anapotoweka, si jambo jepesi sini,
Punguza kufadhaika, angali nawe Manani,
Makiwa ndugu Sandichi, kwa kumpoteza mama.
Kiwango ulichofika, alijituma yakini,
Jukumu akajitwika, ukafuzu masomoni,
Na sasa waheshimika, upitapo mitaani,
Makiwa ndugu Sandichi, kwa kumpoteza mama.
Muhali kusahulika, amekuata mwandani,
Utaishi kukumbuka, wema wake maishani,
Na muda utapofika, yazoeleke moyoni,
Makiwa ndugu Sandichi, kwa kumpoteza mama.
Dunia ina mashaka, tena mingi mitihani,
Aliyapanga Rabuka, apime yatu imani,
Kwa hivyo inapozuka, usikate tumaini,
Makiwa ndugu Sandichi, kwa kumpoteza mama.
Wino umeshakauka, hautoki kalamuni,
Mwenzio ninang’atuka, nimefika kikomoni,
Magoti nitatundika, akurehemu Manani,
Makiwa ndugu Sandichi, kwa kumpoteza mama.
FRANK ORINA,
JOMVU MADAFUNI MOMBASA
Heko Steve Kisukwa
Naanza yangu bahati, vina vilandane vyote,
Nilitunge kwa wakati, liwe tamumu popote,
Lake mwana harakati, mwingine asimpite,
Heko Steve Kisukwa, mhasibu wetu bora.
Umeiva hisabati, kuongeza na kugawa,
Nambari hazikukuti, uje kurudia sawa,
Pamwe na alfabeti, nazo mezihesabiwa,
Heko Steve Kisukwa, mhasibu wetu mwema.
Unapendeza jamani, kimavazi kielimu,
Wapenda hurujuani, rangi tamu tena tamu,
Iliyokolea mwambani, waja hilo wafahamu,
Heko Steve Kisukwa, mhasibu wetu bingwa.
Asiyekujua nani, jinsi una moyo safi,
Mzuri nambari wani, huna kinyongo hafifi,
Nakupenda jamanini, ninasema kierufi,
Heko Steve Kisukwa, mhasibu namba moja.
Nakukabidhi kwa Mungu, Muumba mwenye dunia,
Akuondolee mizungu, upate kufurahia,
Ukaishi ulimwengu, miaka tisini mia,
Heko Steve Kisukwa, mhasibu mwenye tiba.
Kisukwe wangu rafiki, Moindi nimeridhia,
Leo sifa kazilaki, kisha ukashangilia,
Pole yake mwenye chuki, moyoni ataumia,
Heko Steve Kisukwa, mhasibu aso doa.
Saba natia mhuri, limetosha langu tungo,
Zuri hili tena zuri, lapendeza kama fungo,
Lisome usisubiri, mudawe bora kiungo,
Heko Steve Kisukwa, mhasibu heko tena.
HENRY MOINDI MONG’ARE
MGANGA WA MISTARI
CHUO CHA MATIBABU-BOMET
Mama sikate tamaa
Kwenye huu ulimwengu, viumbe hutaataa,
Kwa maumivu machungu, wakawa wagaagaa,
Yamekufika mamangu, lakini nasema laa,
Usiikate tamaa, utapona mama yangu.
Kuumwa kuna uchungu, tena uchungu hasaa,
Wakupalia majungu, popote unapokaa,
Wahisi kizunguzungu, na moyo ndani wapaa,
Usiikate tamaa, utapona mama yangu.
Kuishi kuna mizungu, usiikate tamaa,
Maana kazi ya mungu, huwa ameiandaa,
Kwa yeyote mlimwengu, apate kizaazaa,
Usiikate tamaa, utapona mama yangu.
Maradhi ni kama rungu, yaki kwangukia pwaa,
Si maini si mawengu, na viungo hulemaa,
Ukawa kama chachangu, ukikaa huna raa,
Usiikate tamaa, utapona mama yangu.
Unavyoumwa mamangu, n’nakubali hasaa,
Ni kazi ya bwana mungu, ingawa twaona baa,
Na mimi kivyanguvyangu, waniisha ushujaa,
Usiikate tamaa, utapona mama yangu.
Hakuna mvunja chungu, maradhi yakakujaa,
Ila ni kazi ya mungu, kwake yenye manufaa,
Usikufuru mamangu, ni amri ya Allaha,
Usiikate tamaa, utapona mama yangu.
LUDOVICK MBOGHOLI
AL – USTADH – LUQMAN
NGARIBA MLUMBI (006)