• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 8:55 PM
Hatimaye Nzoia yaonja ushindi KPL

Hatimaye Nzoia yaonja ushindi KPL

Na GEOFFREY ANENE

NZOIA Sugar FC hatimaye imepata ushindi wake wa kwanza kwenye Ligi Kuu ya Kenya tangu Novemba mwaka 2017 baada ya kuzima Kakamega Homeboyz 3-1 uwanjani Sudi, Bungoma, Jumamosi.

Wanasukari hawa, ambao ushindi wao wa mwisho ulikuwa 2-0 dhidi ya AFC Leopards mnamo Novemba 1, 2017, hawakuwa wameonja ushindi katika mechi nane mfululizo.

Msimu huu wa mwaka 2018 pekee, Nzoia ilikuwa imepoteza dhidi ya Kariobangi Sharks 1-0 (Februari 3), Mathare United 2-1 (Februari 11), Nakumatt 1-0 (Februari 17) na Tusker 2-1 (Februari 24) kabla ya kulemea Homeboyz.

Nzoia iliingia mchuano wa Jumamosi na rekodi nzuri dhidi ya Homeboyz ya ushindi mmoja na sare moja iliyopata iliporejea kwenye Ligi Kuu mwaka 2017 baada ya kuwa nje miaka 10.

Haikusikitisha mashabiki wake ilipojikakamua na kulinda mabao matatu iliyopata kutoka kwa Elvis Rupia hadi kipenga cha mwisho. Kikoyo Hassan alifungia Homeboyz bao la kufuta machozi.

You can share this post!

Gor, Nzoia, Chemelil na Sofapaka zawika KPL

Kenya yaona vimulimuli tenisi ya Afrika Mashariki

adminleo