Dimba

‘Juogi’ yakosa kusaidia Gor Debi ya Mashemeji ikitoka sare Homa Bay

Na GEORGE ODIWUOR, CECIL ODONGO June 2nd, 2025 Kusoma ni dakika: 2

KAIMU Kocha wa Gor Mahia Zedekiah ‘Zico’ Otieno Jumatatu  aliwakashifu wachezaji wake kwa kuonyesha mchezo mbovu kipindi cha pili, hali iliyosababisha wapata sare ya 1-1 dhidi ya AFC Leopards kwenye Debi ya Mashemeji Kaunti ya Homa Bay.

Debi hiyo ya 97 ilichezwa kwenye uga wa Raila Odinga na kuhudhuriwa na Kinara wa Upinzani Raila Odinga, Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga, Naibu Mkuu wa Wafanyakazi katika afisi ya Rais, Eliud Owalo na wageni wengine wa heshima.

Gor ilichukua uongozi dakika ya 31 pale Austin Odhiambo alipokea mpira kutoka pembeni mwa kijisanduku kisha akaachilia fataki ya kichinichini ambayo ilimlemea Levis Opiyo kunyaka. Hilo lilikuwa bao la 10 kwa Austin msimu huu, akiwa mabao saba nyuma ya mfungaji bora hadi sasa Moses Shumah wa Kakamega Homeboyz.

Opiyo amekuwa akikashifiwa kutokana na masihara ambayo amekuwa akifanya kwenye debi ya Mashemeji mara kwa mara. Leopards ilisawazisha kupitia bao la dakika ya 49 kipindi cha pili lililonyamazisha mashabiki wengi wa Gor waliokuwa wamefurika uwanjani humo.

Fowadi Brian Wanyama alifunga bao baada ya mpira aliouachilia kumpita kipa wa Gor Gad Mathews. Otieno akihojiwa baada ya mechi alisema kuwa kucheza kizembe na kufungwa bao rahisi kipindi cha pili kiliwaponza ilhali walihitaji kupata ushindi.

“Tulicheza vizuri kipindi cha kwanza na hata kupata uongozi lakini kipindi cha pili tuliporomoka na kufungwa bao rahisi. Kwa kifupi hatukucheza vizuri sana katika mtanange huo hasa kipindi cha pili,” akasema Otieno.

“Leopards walitulemea kupitia mbinu zao na wakapunguza kasi ya mchezo ili kutuhangaisha. Ilikuwa mechi ngumu lakini napongeza Ingwe kwa kucheza vizuri kipindi cha pili,” akaongeza.

Mwenzake wa AFC Leopards Fred Ambani alifurahia kudumisha rekodi yake ya kutoshindwa na Gor kama mchezaji na pia kama kocha.

Gor sasa ipo katika nafasi ya pili kwa alama 55 alama sita nyuma ya viongozi Kenya Police zikiwa zimesalia mechi mbili msimu huu utamatike.

K’Ogalo itacheza dhidi ya Ulinzi Stars na Kenya Police mechi ya mwisho huku maafande hao wakivaa na Shabana kabla ya kuhitimisha msimu Juni 15 dhidi ya K’Ogalo.