Mercy Oketch raha tele Kip Keino Classic, Omanyala alimwa tena
MERCY Oketch amesisimua mashabiki ugani Ulinzi Sports Complex mjini Nairobi baada ya kutwaa umalkia wa mbio za mita 400 kwa rekodi mpya ya kitaifa mnamo Jumamosi, Mei 31, 2025 akifuzu kushiriki Riadha za Dunia baadaye mwaka huu.
Oketch aliyeimarisha muda wake bora 51.64 akitwaa taji kwa 50.14, alifuatwa kwa karibu na Mganda Leni Shida (50.93), Mercy Chebet (51.52) na raia wa Norway, Astri Ertzgaard (52.39) na Josefine Eriksen (52.40), mtawalia.
Mbali na kuvunja rekodi ya Mary Moraa ya 50.38 iliyowekwa Julai 2023, Oketch pia alifuta rekodi ya Kip Keino Classic ya 50.99 iliyomilikiwa na Beatrice Masilingi kutoka Namibia ugani Nyayo mwaka 2020.
“Nafurahia sana muda nimepata. Nimeweka rekodi mpya ya kitaifa kwa kuinyakua kutoka kwa shujaa wangu Mary Moraa na kufuzu kushiriki Riadha za Dunia. Mashabiki walinipa msukumo kabisa,” akaeleza Oketch aliyeshiriki Riadha za Dunia za Kupokezana Vijiti zaidi wa majuma mawili yaliyopita nchini China ambako pia alijikatia tiketi katika 4x400m (mseto).
Lilian Odira (800m) na Edmund Serem (3,000m kuruka viunzi na maji) pia walitawala vitengo hivyo vyao kwenye makala hayo ya sita yaliyovutia washiriki kutoka Canada, Afrika Kusini, Amerika, Norway, Ethiopia, Uhispania, Poland, Croatia, Hungary, Uganda, Japan, Ugiriki, Ukraine, Djibouti, Morocco, Ufaransa, Ujerumani, Denmark, Ureno, Ubelgiji, Liberia, Botswana, Finland, Cameroon, Czech, Uswisi, Misri, Romania, Slovakia na Kenya. Mshikilizi wa rekodi ya Afrika ya 100m, Ferdinand Omanyala, ambaye alikamata nafasi ya tano, aliridhika na nafasi ya tatu katika umbali huo kwa sekunde 10.07 baada ya kumaliza nyuma ya Lachlan Kennedy kutoka Australia (9.98) na Bayanda Walaza kutoka Afrika Kusini (10.03).
Odira alikamilisha mizunguko yake miwili katika nafasi ya kwanza kwa dakika 1:58.31 kutoka 1:58.53 aliokuwa nao. Alifuatwa na Oratile Nowe kutoka Botswana (1:58.47), bingwa wa Afrika Sarah Moraa (1:58.96) na Shafiqua Maloney kutoka Saint Vincent & Grenadines (1:59.13).
Mganda Sarah Chelangat alinyakua taji la 5,000m kwa dakika 15:03.33, huku Maurine Chebor (15:14.57) na Muethiopia Gemene Mamite (15:21.25) wakifunga tatu-bora.
Wawakilishi wa Kenya katika urushaji mkuki, Julius Yego na Alex Kiprotich, walikamata nafasi ya tano na tisa, mtawalia. Bingwa wa zamani wa dunia Yego aliandikisha mtupo wake bora wa mita 78.74 baada ya kutokana na majaribio manne. Kiprotich alipata alama zake (74.17) kutokana na mtupo wake wa kwanza. Mbrazil Luiz Mauricio da Silva aliibuka mshindi wa mita 86.34 akifuatiwa na Mjerumani Thomas Rohler (80.79) na Mreno Leandro Ramos (80.68). Bingwa mtetezi Anderson Peters alikamata nafasi ya saba (77.49) kutoka orodha ya washiriki 11.
Katika 10,000m, Silas Senchura alitwaa ubingwa baada ya kukamilisha mizunguko hiyo 25 kwa dakika 28 na sekunde 18.46 akifuatiwa na Titus Kiprotich (28:21.79) na Joseph Kimutai (28:23.83).
George Malala, ambaye alikamata nafasi ya tano mwaka jana, alitawala kurusha tufe kwa mita 16.66, mita moja mbele ya Benson Maina (15.56) naye Leonard Bett akafunga tatu-bora (15.27).
Dominic Abunda alimaliza mkiani kwa mita 61.50 katika Hammer Throw ambapo bingwa wa 2024 Ethan Katzberg kutoka Canada, Matija Greguric wa Croatia na Daniel Raba kutoka Hungary walifuatana katika nafasi tatu za kwanza kwa 82.73, 76.68 na 75.93, mtawalia.
Wiseman Were alishinda 400m kuruka viunzi kitaifa baada ya kuandikisha muda wake bora wa sekunde 48.34. Kemorena Tisang kutoka Botswana (48.59) na Kipkorir Rotich (49.17) walimaliza nambari mbili na tatu, mtawalia.
Zablon Ekwam aliridhika na nafasi ya tatu katika 400m wanaume kwa sekunde 45.01, nyuma ya mshindi Zakithi Nene kutoka Afrika Kusini (43.76) na nambari mbili Chidi Okezie wa Nigeria (44.98).
Stanley Waithaka aliridhika na nafasi ya tatu katika 5,000m kwa 13:38.17, nyuma ya Waethiopia Hailemariyam Amare (13:34.02) na Ayele Tadesse (13:34.86).
Edmund Serem alitimiza ahadi kuwa ataponyoka na taji la 3,000m kuruka viunzi na maji kwa kuzikamilisha kwa 8:27.68 akifuatwa na Waethiopia Dinka Fikadu (8:27.97) na Gemechu Godana (8:31.82). Cornelius Kiplagat, Wilberforce Kones na Amos Kimeli walisalimu amri mapema.
Amalie Luel kutoka Norway alimarisha rekodi yake ya Kip Keino Classic kutoka sekunde 54.89 hadi 54.80 akishinda 400m kuruka viunzi.
Joseph Fahnbulleh kutoka Liberia aliibuka mfalme wa 200 kwa 20.40, mbele ya Shaun Maswanganyi wa Afrika Kusini (20.47) na Mswisi William Reais (20.72).
Abel Kipsang (3:35.09), Mathew Kipsang (3:35.87) na Vincent Keter (3:37.59) walifagia nafasi tatu za kwanza katika 1,500m. Diana Chepkemoi akawa Mkenya wa kwanza katika kitengo cha kinadada cha 3,000m kuruka viunzi na maji ambacho Ethiopia ilizoa nafasi tatu za kwanza.
Maia McCoy na Destiny Smith-Barnett kutoka Liberia walikamata nafasi mbili za kwanza za 100m kwa 11.21 na 11.29, mtawalia. Bassant Hemida kutoka Misri alifunga tatu-bora (11.49). Jonah Koech kutoka Amerika, Nicholas Kebenei na Alex Ngeno walifuatana katika nafasi tatu za kwanza katika 800m kwa dakika 1:43.32, 1:43.75 na 1:45.17, mtawalia.
Purity Chepkurui naye alimaliza katikati ya Waethiopia Hawi Abera na Ksanet Alem katika 1,500m.