• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 10:50 AM
Muethiopia Lemlem aonyesha kinadada Wakenya kivumbi mbio za mita 1,500

Muethiopia Lemlem aonyesha kinadada Wakenya kivumbi mbio za mita 1,500

Na GEOFFREY ANENE

Lemlem Hailu amezidia maarifa wenyeji Kenya katika mbio za mita 1,500 za wanawake kwenye makala ya kwanza ya Kip Keino Classis uwanjani Nyayo jijini Nairobi, Jumamosi.

Katika duru hii ya mwisho ya Riadha za Dunia za Continental Tour, Muethiopia huyo alilazimika kukamilisha mizunguko hiyo mitatu kwa kuongeza kasi ikisalia mita 200 hivi baada ya Mkenya Winny Chebet kutisha kuvuruga mpango wake alipompita, japo kwa hatua chache tu.

Mshindi huyo wa nishani ya shaba kwenye Michezo ya Afrika mjini Rabat nchini Morocco mwaka 2019 alikuwa ameonyesha ana nguvu kwa kukimbia kama kwamba alikuwa akifanya mazoezi akifuata Silvia Chesebe kwa karibu katika mizunguko ya kwanza miwili. Chesebe alijiondoa kabla ya kufika mwisho, huku Hailu akisalia mbele.

Hata hivyo, Chebet,29, ambaye alishinda medali ya dhahabu katika Riadha za Bara Afrika mjini Asaba nchini Nigeria mwaka 2019 alimpita Hailu wakikaribia kona ya mwisho na kulazimu Muethiopia huyo kuongeza kasi na kutwaa taji kwa dakika 4:06.43.

Chebet alikamilisha kwa dakika 4:06.78 akifuatiwa na bingwa wa mbio za mita 5,000 wa michezo ya Jumuiya ya Madola 2014 Mercy Cherono, ambaye alikuwa akirejea ulingoni baada ya kuwa nje na jeraha kwa miaka miwili, aliyetumia dakika 4:0679.

Bingwa wa Olimpiki za Makinda 2018 Edinah Jebitok aliridhika katika nafasi ya nne (4:0724) katika kitengo hicho kilichovutia wakimbiaji 10.

You can share this post!

WASONGA: Matiang’i na Kibicho watoe majibu kuhusu Huduma...

Kiprotich aapa kumaliza utawala wa Julius Yego