Nairobi United yalenga fainali ya Mozzart Bet ikivaana na Mara Sugar leo
Nairobi United itakuwa ikilenga kuandikisha historia kufika fainali ya Kombe la Mozzart Bet itakapovaana na Mara Sugar kwenye mechi ya nusu fainali itakayogaragazwa Jumapili uga wa Dandora, Nairobi.
Timu hiyo ndiyo pekee isiyokuwa ya Ligi Kuu (KPL) ambayo imebakia kwenye kipute hicho ambacho mshindi hufuzu Kombe la Mashirikisho Afrika (Caf) na pia kushinda Sh2 milioni.
Mshindi wa mechi hiyo ya nusu fainali atachuana na Gor Mahia kwenye mchuano wa fainali katika tarehe ambayo itatangazwa baadaye mwezi huu.
Gor ilitinga fainali wikendi iliyopita kwa kuichapa Murang’a Seal 5-4 kupitia mikwaju ya penalti baada ya timu zote mbili kutoka sare tasa muda wa kawaida.
Mara Sugar nayo iliwaondoa mabingwa watetezi Kenya Police pia 5-4 kupitia mikwaju ya penalti, timu hizo zikiagana sare ya 1-1 katika muda wa kawaida kwenye mechi ya robo fainali.
Mechi hiyo ya robo fainali ilichezwa kwa kuchelewa ikilinganishwa na nyingine kutokana na kesi ambayo ilikuwa imewasilishwa na AFC Leopards.
Ingwe ilikuwa inapinga Mara Sugar kupewa ushindi kufuatia ghasia zilizogubika mechi yao ya raundi ya 32 mnamo Machi 8.
Nairobi United ambayo inanolewa na Kocha Nicholas Muyoti imekuwa mwiba kwa timu za KPL na haitashangaza iwapo watapiga Mara Sugar.
Kwenye robo fainali walipiga Kakamega Homeboyz 2-0. Walipiga KCB 6-5 kupitia penalti baada ya sare tasa kwenye muda wa kawaida katika raundi ya 16.
Pia walibandua Tusker 5-4 kupitia mikwaju ya penalti baada ya timu hizo zote kutoka 1-1 muda wa kawaida kwenye raundi ya 32.
“Tumeonyesha kuwa tunaweza kupiga timu za KPL na tutajituma kuhakikisha kwamba tunatinga fainali kwa sababu lengo letu ni kushinda taji hili,” akasema Muyoti.
Nairobi United pia tayari imefuzu kushiriki KPL msimu ujao kwa kuwa inaongoza msimamo wa jedwali la Supa Ligi (NSL) kwa alama 65 zikiwa zimesalia mechi tatu msimu utamatike.