Michezo

Nairobi United yatwaa ubingwa wa Mozzart Bet na kufuzu Caf

Na CECIL ODONGO June 29th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

Nairobi United Jumapili iliendelea kuangusha mibabe ikitwaa ubingwa wa Kombe la Mozzart Bet baada ya kuipiga Gor Mahia 2-1 kwenye mechi fainali.

Fainali hiyo iligaragazwa katika uga wa Ulinzi Sports Complex, Langáta Nairobi.

Kwenye mechi ya tatu ambayo ilisakatwa uwanja huo kuanzia saa sita mchana, Murangá Seal iliipiga Mara Sugar 1-0 na kumaliza nambari tatu.

Nairobi United ilichukua uongozi mapema kipindi cha kwanza kupitia Frank Ouya ambaye alifunga bao kiufundi, mpira ukimlemea kipa Kevin Omondi kuunyaka.

Gor ilirejea mchezoni dakika ya 36, Ben Stanley Omondi akimaliza vizuri mpira mrefu ulionzishwa na kipa na kuangukia Austin Odhiambo baada ya shambulizi la Nairobi United.

Kwenye kipindi cha pili, aliyekuwa mwanasoka wa Bandari Enock Machaka dakika ya 73 aliachilia fataki kali ambayo ilimlemea Omondi.

Gor ilikuwa na nafasi ya kusawazisha dakika ya 86 baada ya Austin Odhiambo kuangushwa ndani ya kijasanduku. Hata hivyo, Alpha Onyango alipoteza penalti na Naiboys’ ikawahi kombe hilo.

Kutokana na ushindi huo, Nairobi United imeandikisha historia kuwa timu ya kwanza isiyokuwa ya Ligi Kuu (KPL) kushinda Kombe la Mozzart Bet.

Sasa watawakilisha taifa kwenye Kombe la Mashirikisho Afrika (CAF) msimu ujao pamoja na kutia kibindoni Sh2 milioni kutoka kwa wadhamini Mozzart Bet.  Aidha umekuwa msimu mzuri wa Naiboys’ kwa kuwa walipandishwa kushiriki KPL baada ya kutwaa ubingwa wa NSL

“Tumefunga mabao mawili ya kipekee na niliwaambia vijana wangu hatuna chochote cha kupoteza kwa hivyo wapambane kufunga mabao. Gor ni timu kubwa, ilibidi tujizatiti na tukawaweza, nimefurahi sana jinsi tulivyocheza na kupata ushindi,” akasema Kocha wa Nairobi United Nicholas Muyoti.

KCB, Kakamega Homeboyz, Tusker na Mara Sugar ni kati ya timu ambazo Nairobi United ilibandua kwenye hatua za awali na sasa wengi wanasubiri iwapo watatambisha nchi kwenye Caf.

Kocha wa Gor Mahia Zedekiah ‘Zico’ Otieno alilazimika kutoroka mbio kuokoa maisha yake baada ya mashabiki kumwaandama mara tu kipenga cha mwisho kilichopulizwa.

Gor Mahia wamekuwa na msimu mgumu baada ya kushindwa kutetea taji la KPL na tena kupoteza hili la Mozzart Bet. Hii ni mara ya kwanza wanakosa ligi na kombe la Mozzart Bet (Kombe la FKF) tangu 2011.

Kwa kumaliza nambari mbili, walifaulu kutia kibindoni Sh1 milioni huku Murangá Seal na Mara Sugar zikienda nyumbani na Sh750,000 na Sh500,000 mtawalia.