Okutoyi atinga nusu-fainali ya mashindano ya tenisi ya malipo
Nyota Angella Okutoyi ametinga nusu-fainali ya mashindano ya tenisi ya malipo ya wanawake ya W15 Bolszewo baada ya kuzidia maarifa Emilija Tverijonaite kutoka Lithuania kwa seti mbili bila jibu katika robo-fainali ya mchezaji mmoja kila upande nchini Poland mnamo Ijumaa, Juni 20, 2025.
Okutoyi, ambaye alipepeta Barbora Michalkova (Czech) 6-2, 6-2 katika raundi ya 32-bora na Inka Wawrzkiewicz (Poland) 6-3, 6-3 katika hatua ya 16-bora, aliongoza 3-0 seti ya kwanza kabla ya kujinasua kutoka 3-3 baada ya Tverijonaite kusawazisha. Alipata alama nyingi kwa kupokea vyema na pia kupiga mipira moto katika seti hiyo.
Alianza seti ya pili vizuri na hata kufungua mwanya wa 4-1, lakini Tverijonaite akapigana vilivyo na kutoka nyuma kumpita Okutoyi 5-4. Hata hivyo, Okutoyi alijikakamua na kuhakikisha mchuano hauingii seti ya tatu, akisawazisha 5-5 na 6-6 kabla ya kushinda seti ya pili 7-6.
Katika kitengo cha wachezaji wawili kila upande, Okutoyi anashirikiana na Salma Drugdova kutoka Serbia wako katika fainali.
Okutoyi/Drugdova wamekung’uta Zuzana Kudlackova/Magdalena Smekalova kutoka Jamhuri ya Czech 6-0, 6-1 katika nusu-fainali iliyodumu dakika 49, Ijumaa.
Walipepeta Nadia Affelt na Inka Wawrzkiewicz kutoka Poland 6-4, 6-3 katika raundi ya kwanza na kunyamazisha Venla Ahti (Finland)/Helena Buchwald (Ujerumani) 7-5, 6-4 katika robo-fainali.
Okutoyi atakuwa akifukuzia taji la tatu mfululizo mwaka huu la wachezaji wawili kila upande baada ya kutawala W35 Nairobi akishirikiana na Sada Nahimana kutoka Burundi mwezi Januari, na kushinda W50 Troisdorf nchini Ujerumani akishirkiana na Mwamerika Rasheeda McAdoo na W15 Madrid nchini Uhispania akishirikiana na Mwitaliano Sofia Rocchetti mapema mwezi huu wa Juni.