• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 10:48 AM
Rangers yalenga nafasi ya 3 ikimenyana na SoNy Sugar

Rangers yalenga nafasi ya 3 ikimenyana na SoNy Sugar

Na CECIL ODONGO

KOCHA wa Klabu ya Posta Rangers Sammy ‘Pamzo’ Omollo amesema kwamba anatarajia upinzani mkali kutoka kwa Klabu ya SoNy Sugar katika pambano kali ya ligi siku ya Jumapili Uwanjani Awendo Green Stadium.

Omollo ambaye alishinda ubingwa wa ligi mwaka wa 2012.akinoa wanamvinyo Tusker, amewataka vijana wake kutowadharau wanaSoNy ambao msimu huu wanaonekana kusuasua ligini.

Wakiwa na motisha ya hali ya juu baada ya kuwashinda viongozi wa ligi Mathare United, Klabu ya Posta Rangers itaazimia kuishinda mechi hiyo ili kupaa hadi nafasi ya tatu ligini.

“SoNy Sugar imekuwa timu imara ligini na unapofikiri wako katika hali ngumu hapo ndipo watakapokubana na kukufunga haswa wakiwa nyumbani,” akasema Kocha Omollo.

Aliongeza kwamba wachezaji wa klabu hiyo ya Awendo watakuwa katika hali nzuri lengo lao likiwa kujitahidi kuridhisha kocha wao mpya.

Kwa upande wao SoNy wataweka mzaha kando katika jitihada zao za kujinasua kutoka eneo hatari la kuteremshwa ngazi kwenye msimamo wa jedwali la ligi.

Wakiwa na mkufunzi mpya Patrick Odhiambo aliyetoka Klabu ya Chemelil kuchukua mahala pa kocha wao wa zamani Salim Babu, wanasukari hao watakuwa na ari ya kuboresha matokeo yao ya wiki jana walipolazimisha sare ya 1-1 dhidi ya Sofapaka FC.

Katika msimamo wa jedwali SoNy wako katika nafasi hatari ya 16 huku Posta Rangers wanaohesabiwa kama wagombezi halisi wa taji la KPL wakijikita katika nafasi ya nne nyuma viongozi Mathare United, GorMahia na AFC Leopards.

“Tumejitayarisha na nina imani kwamba tutashinda na kupata alama zote tatu,” akasema Kocha Omollo.

Mechi hiyo itaanza saa tisa kamili siku ya Jumapili.

You can share this post!

Kocha wa Chemelil awataka vijana wake kufuata maagizo

Sh48 milioni zatengwa kuwalipia karo wanafunzi 15,000 Nakuru

adminleo