• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 7:55 PM
Uhuru azindua ujenzi wa uwanja mpya na wa kisasa mjini Kisumu

Uhuru azindua ujenzi wa uwanja mpya na wa kisasa mjini Kisumu

Na CHRIS ADUNGO

RAIS Uhuru Kenyatta amehakikishia vijana kwamba Serikali yake imejitolea kujenga viwanja vipya, kukarabati vile vilivyopo na kuimarisha miundo-msingi iliyopo ili kufanikisha ndoto zao katika fani mbalimbali za michezo.

Uhuru alisisitiza hayo mnamo Oktoba 22, 2020, katika mji wa Kisumu alikozindua mpango wa kujengwa kwa uwanja mpya wa kisasa na kuamuru ukarabati wa uga wa Moi mjini Kisumu kukamilishwa chini ya kipindi cha miezi sita ijayo.

Ujenzi na ukarabati huo umekadiriwa kugharimu Sh350 milioni.

Rais aliyewahutubia Wakenya katika uwanja wa Maonyesho ya Kilimo mjini Kisumu, alikuwa ameandamana na Kinara wa Chama cha ODM Raila Odinga, Waziri wa Michezo Amina Mohamed na Spika wa Seneti, Ken Lusaka.

“Niko hapa na ndugu yangu Raila (Odinga) kuweka msingi wa ujenzi wa uwanja mpya. Mkandarasi ametuhakikishia kwamba uga huu utakuwa tayari kufikia Aprili 2021. Kwa hivyo, tutarejea hapa kuufungua uwanja huo kwa mechi itakayowakutanisha Gor Mahia na AFC Leopards. Naomba Lusaka aanze mipango ya kuandaa kikosi chake (Leopards) kwa minajili ya gozi hilo,” akasema Uhuru huku akishangiliwa na wakazi wa jiji la Kisumu.

Uhuru alimtaka pia Waziri wa Usalama, Fred Matiang’i kuhakikisha kwamba barabara zote kuelekea katika uwanja huo zinakarabatiwa, kuwekwa lami na taa.

“Ni matarajio yetu makubwa kuona vijana wetu wakichezea vikosi vya haiba kubwa barani Ulaya kama vile Liverpool na Manchester. Tumepania kujenga viwanja hivi kwa ajili yenu. Ni wajibu wenu sasa kuazamia haja ya kutambua vipaji vyenu na kuvitumikisha ipasavyo,” akasema Uhuru.

“Tulikuwa na mpango wa kujenga uwanja mpya kwenye sehemu iliyoko uga wa Jomo Kenyatta kwa sasa. Lakini tulielezwa kwamba nafasi hiyo ni ndogo ndipo tukahamishia mradi huu hapa katika sehemu hii ya Mamboleo ambayo imekuwa ikitumiwa kwa maonyesho ya kilimo,” akaongeza kwa kusisitiza kwamba idhini hiyo ilitolewa na Gavana wa Kisumu Prof Anyang Nyong’o ambaye amejitolea mwenyewe kusimamia ujenzi huo uliozinduliwa na Rais.

Mbali na kutumiwa kwa maonyesho ya kilimo, uga wa Mamboleo umekuwa mwenyeji wa mechi mbalimbali za kikosi cha raga cha Kisumu RFC na mapambano ya kila mwaka ya Onge Ringo kwa wanaraga sita kila upande.

Kukamilika kwa uwanja huo mpya kutaufanya kuwa na uwezo wa kubeba zaidi ya mashabiki 30,000 walioketi kwa minajili ya mashindano mbalimbali ya Ligi Kuu ya Soka na michezo ya kila sampuli katika viwango vya kitaifa, kimaeneo na kimataifa.

Ua utakaozingira uwanja huo ambao utakuwa pia na uwezo wa kuandaa michezo ya hoki, voliboli, riadha, uogeleaji, mpira wa vikapu na netiboli; utakuwa wa kuta za saruji.

Utakuwa pia na mahali pa mashabiki, wachezaji wa akiba na maafisa wa benchi za kiufundi kukalia pamoja na vyumba vya wachezaji kubadilishia sare.

Vyumba vya mazoezi ya viungo, kumbi za burudani, sehemu za watoto kuchezea, vyoo vipya na maegesho ni kati ya maeneo yatakayokuwa na sura mpya katika uga huo utakaowekewa zulia jipya la kisasa.

You can share this post!

Nimechangia kuporomoka kwa taaluma ya Oezil – Arteta

BBI: Rai ya wabunge dhidi ya upotoshaji