ODM ilivyomeza chambo cha Ruto
KUFIKIA Juni mwaka jana, kila mara chama cha ODM au kiongozi wake Raila Odinga alipozungumzia masuala muhimu ya kitaifa, alitoa matamshi makali dhidi ya maafisa wa serikali ya Ruto.
Raila alikuwa akikosoa vikali serikali na mara nyingi alishutumiwa kwa kuhujumu serikali na hata kutuhumiwa kwa kushirikiana na mataifa ya kigeni kuchochea vurugu.
Kila ODM ilipoitisha maandamano jijini Nairobi au miji mikubwa, shughuli za biashara zilikwama. Wakati mmoja, Wizara ya Fedha ilikadiria nchi ilipata hasara ya Sh2 bilioni kila siku maandamano yalipofanyika.
Lakini kupitia weledi wake wa kisiasa, Rais William Ruto alisuka mkakati wa kumuingiza boksi ambao wadadisi wanasema umefaulu.Raila alikuwa mwiba kwa Rais William Ruto.
Wasaidizi wa rais wanakiri kuwa kama Raila angejiunga na maandamano ya Gen Z mnamo Juni 2023, huenda serikali ya Kenya Kwanza ingezama.
Kwa hivyo, mkakati ulisukwa ili kumdhibiti kwa njia yoyote.
Mkakati huo uliwezesha kumvuta Raila na chama chake upande wa serikali na uliiva alipotangaza kuwania wadhifa wa bara hata kabla ya maandamano ya Gen Z.
Rais Ruto pia alianza kupenyeza maendeleo katika ngome ya Raila ya Nyanza ili kuyeyusha mioyo ya wafuasi wa waziri mkuu huyo wa zamani.
Leo hii, ODM inaonekana kama kiungo cha serikali, licha ya viongozi wake kukanusha wamo ndani.
Wanapokea lawama sawa na Kenya Kwanza kwa matatizo kama ongezeko la gharama ya maisha na changamoto za utekelezaji wa mradi wa SHA.
Wakosoaji hawachelei kuwaambia wafuasi wa ODM kuwa, aliyekuwa mwenyekiti wao, John Mbadi, sasa anasimamia Hazina ya Taifa.
Raila mwenyewe wakati mwingine hutambua hatari ya kuhusishwa na serikali zilizo madarakani, hali aliyopitia awali.
Wasaidizi wake wanasema ndio maana yeye husema, “hatuko serikalini, tumechangia tu wataalamu.”
Kauli hiyo humpa nafasi ya kujitenga na serikali inapobidi.
Kwa kiwango fulani, Rais Ruto ameweza kuanzisha migawanyiko ndani ya ODM.
Chama hicho sasa kinakumbwa na migawanyiko na mivurutano, kinyume na kilivyokuwa awali kabla ya serikali Jumuishi.
Mbali na Mbadi, walioteuliwa serikalini ni pamoja na Wycliffe Oparanya (Vyama vya Ushirika na Biashara Ndogo), Hassan Joho (Madini na Uchumi wa Bahari) na Opiyo Wandayi (Nishati).
Aidha, wanachama wa ODM wanaongoza kamati muhimu bungeni kama Afya (James Nyikal – Seme) na Bajeti (Samuel Atandi – Alego Usonga).
Wadadisi wanasema washirika wa Raila serikalini walichaguliwa kuwakilisha ngome zake za Nyanza, Magharibi na Pwani katika mkakakti mpana wa kumtoa katika upinzani.
Katibu Mkuu wa ODM, Edwin Sifuna, alisisitiza kuwa uteuzi wa viongozi wa ODM serikalini haumaanishi kuwa chama kiko serikalini.
“Baba aliniambia hata baada ya kutoa wataalamu, ODM haiko serikalini,” alisema.
Wakati wa kutia saini mkataba wa ushirikiano (MoU), Rais Ruto alimpongeza Raila kwa mchango wake kwa taifa.
“Kila mara taifa linapokutana na changamoto, Baba huchukua hatua za kishujaa kwa manufaa ya taifa,” alisema Ruto.
Dalili za awali za nia ya Rais Ruto kudhibiti ODM zilionekana mapema, alipowavutia wabunge waasi wa ODM kabla ya MoU.
Wanasiasa kama Gideon Ochanda (Bondo), Elisha Odhiambo (Gem), Mark Nyamita (Uriri), Caroli Omondi (Suba South), Shakeel Shabbir (Kisumu East), Felix Odiwuor Jalang’o (Lang’ata), Paul Abuor (Rongo), John Owino (Awendo) na Seneta Tom Ojienda walikuwa tayari wanashirikiana na Ruto kufikia Februari 2023.
Kwa kumkaribisha Raila, Rais Ruto pia alishawishi wabunge wa ODM, ambao sasa wanatetea serikali kama kwamba ni yao.
Gavana wa Siaya James Orengo, ambaye awali alikuwa mkosoaji mkubwa wa serikali Jumuishi, juzi alitembelea Ikulu akiongoza ujumbe kutoka kaunti yake.
Orengo hapo awali aliwahi kusema kuwa maendeleo hayawezi kuwa kigezo cha kupigia magoti kwa serikali.
Viongozi wengine wakuu wa ODM kama Prof Anyang’ Nyong’o (Gavana wa Kisumu) pia wamebadilisha msimamo.
Mnamo Jumatano, Prof Nyong’o alitoa taarifa akisifu serikali kwa miradi inayoendelea Kisumu.
“Tunaunga mkono uamuzi wa Rais Ruto na Raila Odinga kushirikiana kwa umoja na maendeleo ya taifa.”
Baada ya ziara ya viongozi wa Siaya Ikulu, Rais Ruto alitangaza miradi mikubwa ya mabilioni katika uchumi wa baharini (bandari ya Usenge – Sh600 milioni, soko la samaki – Sh400 milioni).
Ruto ametembelea Nyanza mara kadhaa tangu atofautiane na aliyekuwa naibu wake Rigathi Gachagua na ameahidi kuwa ataanzisha na kukamilisha miradi ya maendeleo katika kaunti nne za Kisumu, Migori, Homa Bay na Siaya.