Gen Z ndio kusema 2027, ripoti yaonya
RIPOTI mpya ya kimataifa inaonya kuwa kuna nguvu mpya ya kisiasa ambayo haijawahi kushuhudiwa itakayobadilisha haraka mustakabali wa nchi.
Ripoti hiyo inasema Gen Z, kizazi kilichozaliwa katika enzi ya kidijitali, kinachokabiliwa na changamoto za kiuchumi na kisiasa, kinajitokeza kama kundi lenye ushawishi mkubwa linaloweza kuchochea maandamano ya umma, kuathiri matokeo ya uchaguzi na kushinikiza mageuzi makubwa.
Ripoti ya muungano wa kimataifa wa mashirika ya kiraia, Civicus, iliyotolewa Ijumaa, Machi 13, 2026, inaeleza kuwa Gen Z ni nguvu kuu ya mabadiliko ya kisiasa duniani, kuanzia Ulaya Mashariki hadi Asia Kusini.
Ripoti hiyo pia inasema mienendo kama hiyo inaonekana barani Afrika, hasa Afrika Mashariki ambako idadi kubwa ya raia ni vijana.
Afrika ndiyo bara lenye watu wachanga zaidi duniani, ikiwa na wastani wa umri wa chini ya miaka 20, ilhali nchi nyingi zinaongozwa na viongozi walio na umri mkubwa kwa miongo kadhaa.
Tofauti hii ya vizazi, ripoti hiyo inaonya, inazua pengo kubwa ambalo linaweza kuyumbisha mifumo ya kisiasa iwapo matakwa ya vijana hayatashughulikiwa.
Nchini Kenya, ambapo zaidi ya robo tatu ya wananchi wako chini ya miaka 35, vijana wanakabiliwa na ukosefu mkubwa wa ajira, gharama ya maisha inayoongezeka na hawana uwakilishi wa kutosha kisiasa. Kwa wengi wao, siasa za jadi za vyama hazionekani kutoa matumaini makubwa.
“Vijana wanazidi kuwa mstari wa mbele katika maandamano duniani,” ripoti ya Civicus inaeleza, ikiongeza kuwa washiriki wengi hawakuwa na historia ya uanaharakati kabla ya kusukumwa kuchukua hatua kutokana na ugumu wa maisha au kile wanachohisi ni dhuluma.
Maandamano ya hivi majuzi nchini Kenya kuhusu ushuru, bei ya mafuta na ufisadi yalionyesha jinsi hasira inayochochewa mitandaoni inaweza kuhamia haraka barabarani.
Mitandao ya kijamii kama TikTok, X na Instagram imekuwa vituo vya kupanga maandamano, na kuruhusu harakati zisizo na viongozi rasmi ambazo ni vigumu kwa mamlaka kudhibiti.
Tofauti na vizazi vilivyotangulia, wanaharakati wa Gen Z mara nyingi hufanya kazi nje ya mashirika rasmi.
Viongozi wa wanafunzi, wajasiriamali vijana na wabunifu wa maudhui ya kidijitali wanaunda mijadala ya umma kupitia video zinazosambaa kwa kasi, matangazo ya moja kwa moja mtandaoni na michango ya fedha inayopatikana kupitia umma.
Ripoti hiyo inasema muundo huu usio na kitovu maalumu cha uongozi hufanya harakati za vijana kuwa imara, kwani hawana kiongozi mmoja anayeweza kamatwa, kununuliwa kisiasa au kudhalilishwa ili kuzivunja.
Kulingana na Civicus, vijana wanatumia teknolojia pia kufuatilia mienendo ya polisi, kurekodi ukiukaji wa haki na kuratibu msaada wa kibinadamu kwa waandamanaji.
Katika nchi jirani, hali kama hiyo inaibuka. Maandamano yanayoongozwa na vijana yameyumbisha serikali kutokana na madai ya uwazi wa uchaguzi, kashfa za ufisadi na usimamizi mbovu wa uchumi, hali inayodokeza kuwa ni mwenendo wa kikanda badala ya matukio ya pekee.
Wachanganuzi wa siasa na utawala wanakubaliana na ripoti hii kwamba kiini cha ongezeko hili la ushiriki wa vijana ni mgogoro wa kiuchumi.
“Mamilioni ya vijana wa Kiafrika walioelimika wanaingia katika soko la ajira ambalo haliwathamini, huku mfumuko wa bei ukipunguza uwezo wa kununua hata kwa wale walioajiriwa,” asema David Wahito, mtaalamu wa utawala.
Kwa wapiga kura wa mara ya kwanza, masuala haya ni ya kibinafsi sana: ajira, gharama ya elimu, makazi na uwezo wa kuanzisha familia.
“Malalamiko ya kiuchumi ni kichocheo kikuu cha uhamasishaji,” ripoti hiyo inaonya, ikieleza kuwa ugumu wa maisha ukiendelea kwa muda mrefu, unaweza kubadilisha hasira kuwa hatua za kisiasa za kudumu.
Hali hii ni muhimu hasa kuelekea uchaguzi wa 2027, wakati vyama vya kisiasa tayari vinaanza kurekebisha ujumbe wao ili kuwavutia wapiga kura vijana, huku makundi ya kijamii yakianzisha kampeni za elimu ya uraia zinazolenga majukwaa ya kidijitali.
Ripoti inasema kwamba ushawishi wa Gen Z hauishii kwenye maandamano pekee. “Kampeni za mtandaoni zinaweza kuunda simulizi za kisiasa, kufichua kashfa na kulazimisha taasisi kujibu kwa haraka. Maudhui yanayosambaa kwa kasi yanaweza kuwafikia mamilioni ya watu ndani ya saa chache, na kuwafanya viongozi kuchukua hatua au kuhatarisha sifa zao,” inaeleza,
Vita dhidi ya ufisadi vimefaidika sana na uchunguzi huu wa kidijitali. Wanaharakati vijana mtandaoni wanazidi kufichua kashfa, uandishi wa habari wa wananchi na uchunguzi unaotegemea taarifa za wazi.
Ripoti inasema mamlaka katika eneo hili pia zinaanza kupanua sheria za makosa ya mtandao, uwezo wa ufuatiliaji na udhibiti wa maudhui mtandaoni—hatua ambazo wakosoaji wanasema zinaweza kukandamiza upinzani.
Kenya inapoelekea uchaguzi wa 2027, swali kuu si kama vijana watashiriki, bali ni jinsi watakavyoshiriki,” asema mchanganuzi wa siasa Dkt Isaac Gichuki.
CIVICUS inaonya kuwa kupuuza malalamiko ya vijana kunaweza kuongeza mvutano. Kinyume chake, mageuzi yenye maana yanaweza kutumia nguvu ya kundi hili kubwa la watu kama nguzo ya utulivu.
Kwa mamilioni ya vijana wa Kenya, uchaguzi ujao ni zaidi ya mabadiliko ya kawaida ya uongozi; ni kura ya maoni kuhusu mustakabali wao.