Siasa

Kujipanga: Ruto aongezea Mudavadi, Kindiki, Murkomen mamlaka kimyakimya

Na JUSTUS OCHIENG June 15th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

MPANGILIO mpya wa serikali uliotangazwa katika Agizo la Rais Nambari moja la mwaka 2025, umebadilisha kimya kimya mwelekeo wa madaraka, ukiongeza ushawishi katika ofisi mpya huku ukipunguza nguvu za zingine.

Msingi wa muundo huu mpya ni ugawaji wa kimkakati wa majukumu na rasilmali ambao unaongeza hadhi za idara muhimu.

Uchanganuzi wa karibu wa agizo hilo unaonyesha kuibuka kwa vituo vipya vya madaraka, hasa katika ofisi za Mkuu wa Mawaziri, Naibu Rais, na baadhi ya wizara za kimkakati.

Majukumu yaliyobadilishwa na kuongezwa yanaonyesha si tu mabadiliko ya siasa za ndani bali pia yanaonyesha azma ya Rais kuweka kumbukumbu yake na kudhibiti serikali kwa umakini.

Rais Ruto anasema mpangilio huu ni muafaka kwa kuwa “Serikali Jumuishi inatekeleza Mpango wa Nne wa Kati wa Muda Mrefu (MTP IV) wa ruwaza ya kiuchumi ya Kenya, Vision 2023, kama sehemu ya Ajenda ya Mabadiliko ya Kiuchumi Kuanzia Mashinani (BETA).”

“Imekuwa muhimu kurekebisha Agizo la Rais la Utendaji kuboresha utendaji na mabadiliko ya majukumu katika serikali,” alisema Rais Ruto.

Mabadiliko hayo, alisema, yanakusudia kuimarisha ushirikiano wa serikali katika kuendeleza utawala wa kikatiba na kulinda haki za binadamu kwa kuanzisha Idara ya Serikali ya Haki, Haki za Binadamu na Masuala ya Katiba. Idara hii itakuwa katika ofisi ya Mwanasheria Mkuu, Dorcas Oduor.

Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi, mmoja wa washindi wakubwa katika mabadiliko haya, amepewa majukumu zaidi ya kuratibu, akisimamia masuala ya kigeni na uwekezaji na kumfanya balozi mkuu wa Kenya na uchumi wa nchi.

Ofisi yake sasa ni kitovu cha ushirikiano wa kimataifa na kukuza uwekezaji, ikionyesha nia ya kumuwezesha kuwa na umaarufu na ushawishi katika ulingo wa kimataifa. Hali hii inaimarisha hadhi ya kisiasa ya Bw Mudavadi.

Mkuu wa Mawaziri hivi karibuni alitoa onyo kwa viongozi wa Mlima Kenya kwamba kumtema Dkt.Ruto kunaweza kufanya eneo hilo kupoteza wadhifa wa Naibu Rais.

“Hii haikuwa tishio wala utabiri wa kitu chochote kinachokuja. Ilikuwa ni kukumbusha eneo hilo kuthamini na kulinda nafasi yake ya sasa katika uongozi wa taifa,” Bw Mudavadi aliambia Taifa Leo.

Ujumbe huu uliokuwa wa wazi ulionekana kuimarisha nafasi ya Naibu Rais Profesa Kithure Kindiki kama daraja la jamii kuelekea urais.

Lakini pia unaonyesha udhaifu wa wadhifa wake kwamba kubaki katika siasa kunategemea kuchaguliwa tena kwa Rais Ruto na Mlima Kenya kuunga Kenya Kwanza. Katika agizo la rais , Prof Kindiki anabaki na majukumu muhimu katika uratibu wa serikali za kaunti na marekebisho ya sekta ya kahawa, ishara Ruto anamtumia kulenga Mlima Kenya.

Naibu Rais ameongeza juhudi za kuimarisha mipango ya uwezeshaji wa kiuchumi kote nchini, hasa katika eneo lake la Mlima Kenya hatua inayochukuliwa kama mbinu ya kujiimarisha kisiasa ili kuendelea kushikilia wadhifa wake katika uchaguzi wa 2027.

Wizara ya Fedha, inayoongozwa na Waziri John Mbadi, ambayo ni kitovu cha kudhibiti rasilmali na ufadhili wa maendeleo, bado ni kitovu muhimu cha madaraka.

Nguvu yake katika kutayarisha bajeti, ufadhili wa miradi, na sera za kifedha inafanya wizara hii kuwa kivutio kikuu kwa wale wanaotaka ushawishi. Vilevile, Wizara ya Masuala ya Ndani, chini ya Kipchumba Murkomen, ina mamlaka makubwa kuhusu usalama wa ndani na utawala wa mikoa na hivyo kuwa muhimu katika mkakati wa serikali wa kusimamia siasa.

Wizara iliyoundwa upya ya Uwekezaji, Biashara na Viwanda, chini ya Lee Kinyanjui, pia inajitokeza kuwa muhimu, ikiwa na jukumu la kuendesha mabadiliko ya kiuchumi chini ya Dkt Ruto.

“Kuinua Idara ya Uwekezaji wa Umma kuwa Idara Kamili ya Serikali ya Uwekezaji wa Umma na Usimamizi wa Mali kunalenga kuongeza matumizi bora ya pesa za umma na kuboresha utendaji wa kifedha wa Mashirika ya Serikali, kulingana na ahadi ya Kenya Kwanza kufanya mageuzi na kuimarisha sekta ya umma.”

Inatarajiwa kusimamia miradi mikubwa ya ushirikiano wa umma-na sekta ya kibinafsi na viwanda vya kibiashara, ambavyo ni muhimu katika siasa za 2027. Mpangilio huu una athari kubwa.

Kwa kugawa upya majukumu, kuhamisha bajeti mikononi mwa watu wa kutegemea, Rais Ruto amebadilisha mkondo wa madaraka ndani ya utawala wake.

Wachambuzi wanasema agizo hilo ni chombo cha utawala na mkakati wa kisiasa kwa lengo la kurekebisha ushawishi, kusawazisha uaminifu, na kuandaa viongozi muhimu kwa majukumu yajayo.