Mbadi sasa ‘avaa kiatu cha Raila’ akionekana kutoa maagizo ODM
WAZIRI wa Fedha, John Mbadi anaonekana kujivika kiti cha mfalme katika chama cha ODM akitoa onyo kali kwa wanachama waasi na kuhakikisha anayosema yanatimia.
Ifahamike kuwa Bw Mbadi kwa sasa hana wadhifa wowote katika chama hicho na akiwa waziri hafai kujihusisha na siasa za vyama. Hata hivyo, amekuwa akitoa matamshi yanayoonekana kama maagizo kwa viongozi wa ODM kinachoongozwa na Oburu Oginga.
Siku moja kabla ya Baraza Kuu la Kitaifa la chama kumuondoa Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna kama Katibu Mkuu, Bw Mbadi alisema ni lazima avuliwe wadhifa huo. Na baada ya kuondolewa kwa Sifuna alionya wanachama wengine waasi kuwa chuma chao kiko motoni.
Akizungumza Jumatano, Februari 11, 2026, katika mahojiano na kituo kimoja cha televisheni cha humu nchini, Mbadi alisisitiza kuwa maafisa wakuu wa chama hawawezi kupinga maamuzi ya chama na wakose kuchukuliwa hatua.
Alieleza wazi kuwa kuondolewa kwa Sifuna kunapaswa kuwa funzo kwa wanachama wengine wanaoonekana kwenda kinyume na msimamo wa chama, akiwemo Gavana wa Siaya James Orengo na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, ambao wamekuwa wakishirikiana na Bw Sifuna kupinga maamuzi ya chama hasa ushirikiano wake na chama tawala cha United Democratic Alliance (UDA).
“Kuna watu ambao hawashikilii nyadhifa za msingi ndani ya chama. Lakini kama wanashikilia nyadhifa hizo na kauli au matamshi yao yanasababisha mgawanyiko ndani ya chama, basi ni lazima wachukuliwe hatua,” alisema Mbadi.
“Lakini kumbukeni, Sifuna hakuwa mwanachama wa kawaida; alikuwa Katibu Mkuu wa chama. Mwelekeo aliochukua—kiongozi yeyote mkuu wa chama katika nchi hii anayechukua mwelekeo kama huo hajawahi kubaki katika chama hicho. Ilikuwa ni kupoteza muda kutarajia muujiza kwamba Sifuna angebaki ODM; hilo halingewezekana,” aliongeza.
Mbadi pia alipuuza hofu kuhusu ushawishi unaoendelea wa Bw Orengo, akisema siasa zake za “kuvuruga” si jambo geni kwake, lakini hatashangaa iwapo gavana huyo atarejea katika mkondo rasmi wa chama.
“Siasa za kuvuruga za Orengo nimezoea, lakini sitashangaa akirejea katika mkondo mkuu wa ODM,” alisema Mbadi.
Kamati Kuu ya Kitaifa ya ODM (NEC) ilipendekeza kuondolewa kwa Sifuna kama Katibu Mkuu na kumteua Naibu Katibu Mkuu Catherine Omanyo kushikilia wadhifa huo kwa muda.