Siasa

Mkakati wa Ruto ‘kuteka’ ngome ya Matiang’i

Na NDUBI MOTURI Na RUTH MBULA February 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 3

RAIS William Ruto anaendelea kupanga upya siasa za Gusii kwa kasi kubwa huku akilenga kuwavuta wanasiasa ‘wanaoasi’ vyama vyao.
Wachambuzi wanasema ni mkakati wa makusudi wa kumtenga kisiasa aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani, Dkt Fred Matiang’i, katika ngome yake kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Mkakati huo unahusisha kuwazawadi wanaohamia upande wake, na kutumia mizizi ya kisiasa katika kaunti za Kisii na Nyamira ambako Dkt Matiang’i ni maarufu miongoni mwa wakazi.
Kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa, Rais Ruto amekuwa akijipenyeza kimyakimya lakini kwa uthabiti katika siasa za Gusii, akifanya kazi kwa karibu na Gavana wa Kisii Simba Arati wa ODM, huku wakati huohuo akiimarisha mizizi ya Chama cha United Democratic Alliance (UDA) kupitia wabunge wanaohudumu, walioasi vyama vingine na mabroka wa kisiasa wa eneo hilo.
Vigogo wa UDA katika eneo hilo sasa wanajumuisha Mbunge wa South Mugirango Silvanus Osoro, Mbunge wa Kitutu Chache North Japheth Nyakundi ambaye pia ni mweka hazina wa kitaifa wa chama na Mbunge wa Nyaribari Chache Zaheer Jhanda.
Waziri wa Elimu, Julius Ogamba na Katibu wa Utangazaji na Mawasiliano, Stephen Isaboke, pia ni sehemu ya kikosi cha Ruto kisiasa mashinani.
Ufanisi wao wa wazi ni Mbunge wa Kike wa Kisii, Donya Toto, aliyehama chama cha Wiper baada ya kushinda kiti chake kwa kura zaidi ya 190,000 mwaka 2022.
 Hivi majuzi, chama tawala kilipata ushindi mwingine wa kiishara baada ya Jonah Onkendi, mshirika wa zamani wa Matiang’i katika chama cha Jubilee na aliyeibuka wa pili katika uchaguzi kiti cha ubunge cha Bonchari kuhamia UDA.
Kuondoka kwake kumeangazia hali ya kukata tamaa inayoongezeka miongoni mwa baadhi ya wanasiasa wa eneo hilo wanaohisi kutengwa ndani ya kampeni za kitaifa za Dkt Matiang’i—udhaifu ambao washirika wa Rais Ruto wamekuwa wepesi kuutumia.
Wanasiasa kadhaa wa zamani wa ODM na Jubilee waliokuwa karibu na Matiang’i pia wamehama.
Mbunge wa Kitutu Masaba Daniel Manduku, aliyekuwa akionekana kama mfuasi wake mkubwa, alijiunga na kambi ya Ruto mapema mwaka huu.
Vivyo hivyo Mbunge wa West Mugirango Stephen Mogaka na Irene Mayaka wa ODM.
Seneta mteule wa UDA, Esther Okenyuri, pia amekuwa mstari wa mbele katika juhudi za kisiasa katika eneo la Kisii.
“Nimefanya kazi na Rais Ruto tangu alipokuwa Naibu Rais,” alisema Bi Okenyuri. “Kupitia kampeni tulizofanya pamoja, nilipata nafasi yangu ya sasa na naamini kuna mengi zaidi tunaweza kufanikisha tukifanya kazi na serikali hii.”
Nyuma ya pazia, UDA pia inawavuta watu wenye ushawishi wasiokuwa na nyadhifa za kuchaguliwa, akiwemo aliyekuwa karani wa Kaunti ya Kisii, Alfred Ong’era, ambaye mitandao yake katika Kitutu Chache North bado ina nguvu kubwa kisiasa. Mwingine anayelengwa ni mgombea wa ubunge wa Bobasi Wilkins Nyangweso ambaye bado hajajiunga na upande wowote.
“Ni mapema sana kutangaza chama,” alisema. “Kwa sasa, nimejikita katika kampeni za kuwa Mbunge wa Bobasi. Wakati ukifika, nitaweka msimamo wangu wazi.”
Hata hivyo, licha ya uhamaji huo wa wanasiasa maarufu, uhalisia wa uchaguzi katika Kisii bado unalemea UDA.
Mnamo Novemba 2025, chama tawala kilipata pigo kubwa katika chaguzi ndogo tatu zilizofanyika Kisii na Nyamira licha ya kutumia pesa nyingi katika kampeni zilizoongozwa na viongozi wa kitaifa.
Viti vyote vitatu vilinyakuliwa na chama cha United Progressive Alliance (UPA), chama cha kikanda kinachosimamiwa na Gavana wa Nyamira Amos Nyaribo na kinachoegemea waziwazi upande wa Matiang’i.
Katika Wadi ya Nyamaiya, Christopher Moturi Osiemo alishinda baada ya kifo cha kaka yake, MCA Elijah Osiemo. Katika Wadi ya Ekerenyo, Jeremiah Ongaro alishinda baada ya MCA wa awali kujiuzulu ili kuwa Spika wa Bunge la Kaunti.
Nayo Wadi ya Nyansiongo ilimchagua mgombea wa UPA baada ya mahakama kufuta matokeo ya 2022 kwa dosari za kujumlisha kura.
Ni katika muktadha huu ambapo Naibu Kiongozi wa Chama cha Jubilee ameanza mashambulizi makali, akilaumu serikali ya Ruto kwa kupanga kampeni ya kumzima kisiasa katika ngome yake.
“Wanatumia vitisho na shinikizo kuwafanya wafuasi wangu waniache,” alisema Dkt Matiang’i katika hotuba ya hivi majuzi.
Alidai kuwa viongozi wakuu wa eneo hilo wamekuwa wakiraiwa kwa ahadi za ajira katika mashirika ya umma, fedha taslimu kujitenga naye.