Raila akejeli ‘Wantam’ ya Gachagua
KIONGOZI wa ODM, Raila Odinga amemkashifu aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, akimtaja kama kiongozi asiyeweza kupatia nchi mwelekeo ufaao.
Bw Odinga alipuuzilia mbali kauli ya “Wantam” inayopigiwa debe na Bw Gachagua, akisema kuwa yeye (Raila) anaelewa vizuri anakoelekea kisiasa.
Aidha, alisisitiza kwamba hawezi kushirikiana na Bw Gachagua, akimkosoa kwa kumtaka ateme Rais Ruto na kushirikiana naye.
Waziri Mkuu huyo wa zamani alikuwa akizungumza katika Shule ya Upili ya Makasembo, eneobunge la Rarieda, alipokuwa akiongoza harambee, saa chache baada ya Bw Gachagua kuwataka Wakenya kutomchagua Rais William Ruto tena mwaka 2027 ili awe rais wa muhula mmoja tu.
“Hauwezi kutuelekeza kuhusu njia ya kisiasa ya kufuata. Unaendelea kutuambia kuhusu ‘Wantam’ kana kwamba hatuelewi siasa zetu. Tunajua tunakoelekea na hatuhitaji mwelekeo kutoka kwa Naibu Rais wa zamani,” alisema Bw Odinga.
Alimtaja Bw Gachagua kama kiongozi anayepalilia ukabila hasi na ambaye hawezi kuongoza Kenya kwa njia inayofaa.
“Nitashirikianaje na mtu anayelinganisha serikali na kampuni ambapo watu wanamiliki hisa – wengine nyingi, wengine chache na wengine hawana kitu kabisa?” alihoji Bw Odinga.
Aliendelea kusema: “Aliwahi kusema kuwa akiwakuta watu foleni ya Ikulu, angewafukuza wale wasiopenda serikali na kuwaacha waliompigia kura pekee.”
Wakati huohuo, wafuasi wa Bw Odinga walizungumza nyakati tofauti walisema hawatashiriki maandamano ya kitaifa, wakisema tayari wamefanyia taifa ya kutosha.
Waziri wa Kawi na Petroli Bw Opiyo Wandayi aliwasifu wakazi wa Kisumu kwa kutojiunga na maandamano ya hivi majuzi.
“Mlifanya vyema Jumatano, Juni 25, kwa kukataa kushiriki maandamano. Ilikuwa wazi kuwa ghasia zilitarajiwa Kisumu. Vijana wetu wameandamana kwa miaka mingi—wengine wamekufa; wengine wamejeruhiwa. Sasa wamechoka,” alisema.
Alisisitiza kuwa serikali kwa sasa inalenga maendeleo na si siasa.
“Tumshukuru Raila Odinga kwa uamuzi wake wa kushirikiana na Rais. Mkataba wao wa maelewano umeleta amani na utulivu,” alisema.
Mbunge wa Alego Usonga Bw Samuel Atandi alisisitiza msimamo wa kiongozi wa ODM huku akikosoa maandamano yaliyosababisha uharibifu wa mali na majeraha.
“Sisi kutoka Luo Nyanza tumekuwa tukijulikana kwa maandamano, lakini hatujawahi kuchoma kituo cha polisi au kuharibu mali kwa kiwango hicho,” alisema Bw Atandi.
Aliongeza kuwa maandamano hayo yalikuwa na nia ya kupindua serikali ya Rais Ruto.
“Kuna watu ambao hawafurahii kuwa watu kutoka eneo la ziwa wamehusishwa katika maamuzi ya taifa. Ndio maana wanajaribu kila njia kuitikisa serikali ya Rais kupitia nguvu,” alidai.
Aliwashauri viongozi aliowatuhumu kufadhili maandamano hayo kusubiri uchaguzi mkuu na kupiga kura kama katiba inavyoelekeza.
“Rais Ruto alichaguliwa kidemokrasia. Huwezi kumng’oa madarakani kwa nguvu; alitangazwa na IEBC, na hata baada ya baadhi ya watu kwenda kortini, ushindi wake ulithibitishwa,” aliongeza Mwenyekiti huyo wa Kamati ya Bajeti.
“Rais Ruto alichaguliwa, na kama ataondoka, basi iwe kwa kura, si kwa kutumia nguvu kama baadhi ya viongozi wanavyotaka kwa kutumia vijana wetu,” alisema mbunge huyo.
Wafanyabiashara wa Kisumu pia waliwasifu vijana wa kaunti hiyo kwa kudumisha amani na kuepuka maandamano siku hiyo.