Uhuru na Gachagua sasa kuwania Mlima
RAIS mstaafu Uhuru Kenyatta ameibuka mshindi katika mvutano wa muda mrefu kuhusu uongozi wa Chama cha Jubilee, baada ya Mahakama Kuu ya Milimani kuthibitisha uhalali wa maamuzi yaliyopitishwa katika Mkutano Mkuu wa Kitaifa wa Wajumbe (NDC) uliofanyika Mei 2023.
Wadadisi sasa wanasema ushindi huo unampa nguvu ya kuimarisha chama kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027 huku kikikabiliana na wimbi la kile cha aliyekuwa naibu rais Rigathi Gachagua cha Democratic Citizens Party (DCP).
Ushindi wake katika vita vya uongozi wa Jubilee ni pigo kwa washirika wake wa zamani aliyekuwa mbunge wa Kieni, Bw Kanini Kega na Mwakilishi wa Wanawake wa Kaunti ya Murang’a Sabina Chege ambaye pia ni mbunge wa kuteuliwa wa chama hicho.
Wawili hao waliongoza mrengo uliokuwa umempokonya Uhuru uongozi wa chama hicho wakidai akiwa rais mstaafu hafai kujijhusisha na siasa za vyama.
“Kikao cha Kamati Kuu ya Kitaifa (NEC) kilichofanyika Aprili 28, pamoja na Mkutano Mkuu wa Kitaifa wa Wajumbe (NDC) wa Mei 22, 2023, vinatambuliwa kama halali, na hivyo maamuzi yote yaliyotokana na mikutano hiyo yanathibitishwa,” mahakama ilisema.
Hii inamaanisha kuwa Uhuru Kenyatta sasa anarudi rasmi kama kiongozi wa chama hicho, huku Saitoti Torome akithibitishwa kuwa Mwenyekiti wa Kitaifa na Jeremiah Kioni kama Katibu Mkuu wa Jubilee.
Viongozi hao wawili waliteuliwa na kuidhinishwa katika mkutano wa NDC wa 2023.
Mahakama pia iliagiza kuwa maamuzi hayo yawasilishwe kwa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa (ORPP) kwa hatua za mwisho za kutambuliwa rasmi.
Uamuzi huu umetafsiriwa kama pigo kubwa kwa mrengo ulioongozwa na Kega na Bi Chege, ambao waliwasilisha kesi katika ya Mahakama ya Mizozo ya Vyama vya Kisiasa (PPDT) kupinga uhalali wa mkutano huo wa Mei 2023. Katika hatua ya kisiasa ya kushangaza mwezi Machi 2025, aliyekuwa mwenyekiti wa chama hicho Nelson Dzuya, ambaye awali alikuwa upande wa Kega, alibadilisha msimamo wake na kuwasilisha makubaliano ya kuunga mkono matokeo ya NDC.
Kupitia wakili wake Jackson Awele, Dzuya alithibitisha kuwa mzozo kati yake na upande wa Uhuru ulikuwa umeisha, na hivyo IDRC haikuwa na mamlaka ya kuendelea kushughulikia suala hilo.
Uamuzi huu pia umewavutia wadau mbalimbali wa kisiasa akiwemo Moses Kuria, mshirika wa zamani wa Uhuru na mshauri mkuu wa Rais William Ruto katika Baraza la Ushauri wa Kiuchumi.
Bw Kuria alimpongeza Bw Kenyatta kwa kuthibitishwa kuwa kiongozi wa Jubilee.
“Hongera kaka yangu mkubwa, Rais Uhuru Kenyatta, kwa kurejeshewa uongozi wa Jubilee. Katika kipindi ambapo taifa linaelekea kugawanyika, chama hiki chini ya uongozi wako kina nafasi muhimu katika kuleta mshikamano wa kitaifa,” alisema.
Kwa mujibu wa wadadisi wa siasa, kauli ya Kuria inaashiria kuwa Kenya Kwanza inafahamu au inahofia mchango wa Bw Kenyatta katika uchaguzi mkuu ujao na inamchukulia kama anayeweza kupunguza kasi ya Gachagua anayeendelea kujiimarisha katika siasa za Mlima Kenya.
“Hatua hii inamweka Uhuru katika nafasi nzuri ya kuchangia na kushawishi siasa za kitaifa hususan wakati huu ambapo vyama vya upinzani vinaungana kuelekea uchaguzi wa 2027 japo huenda hatafanya hivyo moja kwa moja,” asema mchanganuzi wa siasa Gabriel Kibe.
Anasema kuimarika kwa Jubilee chini ya Kenyatta kutachangia ushindani katika eneo la Mlima Kenya hasa baada ya Bw Gachagua kuzindua chama chake cha DCP.
Kuna dalili kwamba Jubilee inaelekea kuungana na vyama vingine vya upinzani ikiwemo DCP ya Bw Gachagua na Peoples Liberation Party (PLP) ya aliyekuwa waziri Martha Karua.
Bw Torome amekuwa akiungana na viongozi wengine wa upinzani wanaosuka muungano wa kushindana na Kenya Kwanza katika uchaguzi mkuu ujao.Bw Kioni ametangaza kuwa Jubilee inamuunga mkono aliyekuwa waziri wa usalama wa ndani Fred Matiang’i ambaye pia amekuwa akihudhuria vikao vya viongozi wa upinzani na anachukuliwa kuwa mradi wa Bw Kenyatta.
“Kilicho wazi ni kuwa mchango wa Bw Kenyatta katika uchaguzi mkuu ujao hauwezi kupuuzwa hasa baada ya kuthibitishwa kuwa kiongozi wa chama cha Jubilee,” asema Bw Kibe.