• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 10:55 AM
CHOCHEO: Akikuacha kwenye dhiki utamsamehe ukiomoka?

CHOCHEO: Akikuacha kwenye dhiki utamsamehe ukiomoka?

NA BENSON MATHEKA

Miaka minne iliyopita, Rosa* alimuacha mumewe kwa sababu hakuwa na uwezo wa kukimu mahitaji ya familia. Mumewe Alex* hakuwa na kazi na maisha yalipokuwa magumu baada ya kuugua, Rosa aliondoka na watoto wao watatu. Hata hivyo, haikuchukua muda, Alex alipona na akatia bidii hadi akajaliwa kupata mali.

“Baada ya kusikia niliomoka, Rosa amerudi kwangu na kuniomba msamaha. Anataka arudi tujenge ndoa ambayo alibomoa nilipokuwa nikimhitaji zaidi wakati wa ugonjwa. Sidhani ninaweza kumsamehe,” asema Alex.

Kinachomuuma mwanamume huyu ni kwamba Rosa hakurudi kwa wazazi wake alipomuacha akiteseka.

“Japo nilikuwa sijiwezi, nilifuatilia na nikaibaini kwamba hakuenda kwa wazazi wake alipoondoka kwangu akidhani nitakufa kwa sababu ya shida na ugonjwa. Sijui alikokuwa na sitaki anieleze,” asema Alex.

Visa vya wachumba kutema wenzao shida zikiongezeka ni vingi mno hasa wakati huu wa janga la corona.

“Sio kwamba ni jambo geni lakini kipindi hiki cha corona, visa vya waume na wanawake, kuwapiga teke wachumba wao vimeongezeka. Ni mtindo unaoshuhudiwa kote ulimwenguni,” asema Talia Simiyu mshauri wa wanandoa wa kituo cha Big Hearts jijini Nairobi.

Anasema watu wanaowaacha wapenzi wao wakilemewa na shida na kuwarudia wakifanikiwa huwa hawana mapenzi ya dhati.

“Wakati wa harusi hasa za Kikristo, wanandoa huwa wanaapa kuishi pamoja wakati wa faraja na wakati wa dhiki. Kwa hivyo ukimuacha mchumba wako kwa sababu ya kufilisika au kuwa mgonjwa unaenda kinyume na viapo vya ndoa,” asema.

Hata hivyo anasema kuna watu wanaowasamehe waenzao waliowaacha wakiwa na shida na kurejea wakipata pesa.

“Wapo wanaoamua kuwasamehe hasa ikiwa walikuwa wamezaa watoto. Hata hivyo, ni vigumu mtu kusahau kitendo kama hicho na lazima uhusiano wao uwe na misukosuko,” aeleza Talia,Dorcas Kibaya, mwanadada mwenye umri wa miaka 32 anasema kwamba hawezi kumsamehe mumewe aliyeamuacha akiwa mgonjwa mahtuti.

“Mtu ambaye aliniacha nikiwa mgonjwa mahtuti na kuenda kuishi na mwanamke mwingine nimsamehe mimi? Wallahi siwezi!” asema kwa machungu. Mwanadada huyu anasimulia kwamba kama haingekuwa majirani waliomsaidia mumewe alipotoroka, yeye na watoto wake wawili hawangekuwa hai.

“Alijitokeza baada ya miaka sita aliposikia sikufariki, akapata watoto wakiendelea vyema na kudai ni wake. Nilimwambia sikatai watoto ni wake wa kuzaa lakini nikamkumbusha aliwatelekeza nikiwa hoi kwa ugonjwa. Nilimwambia apotelee mbali,” aeleza Kibaya.

Kulingana na Talia, watu wanaweza kuwasamehe wachumba wao wanaowatema wakati wa shida hasa ikiwa walikuwa na watoto lakini wakose kuishi pamoja.

“Msamaha ni muhimu kwa mwanadamu kupata uponyaji wa moyo lakini kwa sababu ya yaliyotokea, napendekeza watu wasipapie kuishi pamoja ikiwezekana,” aeleza.

Peter Kamau alizingatia ushauri huu mkewe aliyemuacha akiwa chumba cha wagonjwa mahtuti aliporejea baada ya kupona na kurudia shughuli zake za kawaida.

“Nilikuwa na uchungu mwingi moyoni lakini nikaumeza kwa sababu niliwapenda watoto wangu. Hata hivyo sikukubali kuishi nyumba moja na mtu aliyeniacha nikiwa ICU na kusomba mali na pesa ambazo ningetumia kulipa bili ya hospitali,” aeleza Kamau.

Kamau ambaye ni mfanyabiashara jijini Nairobi huwa anatenga muda wa kuwa na watoto wake ambao anakidhi mahitaji yao kikamilifu.

“Kutokana na yaliyonipata, nimeamua kwamba hakuna mapenzi ya dhati ulimwenguni. Kuna kinachomfanya mtu kumpenda mwingine na kikikosekana huwa hauna thamani kwake,” aeleza Kamau.

Kulingana na Pasta Isaac Okoth wa kanisa la Reoboth Revival, mtaani Kayole Nairobi, moja ya nguzo kuu za ndoa ni msamaha.“Msamaha ndio nguzo ya ndoa japo ni uchungu kuachwa na mtu wakati unamhitaji zaidi hasa aliyeapa kuishi nawe hadi kifo kiwatenganishe,” asema.

You can share this post!

FUNGUKA: Utamu wa ubuyu ni ladha tofauti

Mbunge akamatwa kuhusu mapigano Kapedo