NA CECIL ODONGO
ULAJI wa chumvi nyingi umekuwa ukihusishwa na maradhi tele kama vile shinikizo la damu, magonjwa ya moyo, kiharusi kati ya mengineyo.
Shirika la Afya Duniani (WHO) linapendekeza kuwa mtu anafaa kula chini ya gramu tano za chumvi kwa siku.
Kwa mujibu wa WHO, idadi kubwa ya watu, wakiwemo Wakenya, hula gramu 10 au zaidi ya kijiko kimoja cha chumvi kwa siku hivyo kuhatarisha afya zao.
Wataalamu wanasema kuwa chumvi nyingi hufanya maji kuingia kwenye mishipa ya damu hivyo kumfanya mtu kuandamwa na shinikizo la damu.
Lakini sasa utafiti mpya umebaini kuwa chumvi nyingi mwilini pia husababisha msongo wa mawazo (stress).
Utafiti uliofanywa na Chuo Kikuu cha Edinburgh nchini Uingereza, umebaini kuwa chumvi nyingi hufanya mwili kutoa kiasi kikubwa cha homoni ambazo husababisha ubongo kuandamwa na msongo wa mawazo.
Japo jinsia zote hukumbwa na msongo wa mawazo, wanaume ndio huathirika zaidi. Takwimu zaonyesha kuwa idadi kubwa ya wanaume hukimbilia kujitoa uhai wanapokumbwa na msongo wa mawazo ikilinganishwa na wanawake.
Nchini Kenya, idadi ya wanaume wanaojitoa uhai ni mara tatu ya wanawake.
Watalaamu wanasema kuwa tofauti na wanawake ambao huzungumza na wenzao kuhusu masaibu wanayowakumba, wanaume husalia kimya.
Wanaongeza kuwa malezi yanachangia pakubwa hali hiyo kwani wanaume wamefunzwa tangu utotoni kuwa ‘mwanamume hafai kulia hata akiumia’.