• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 5:22 PM
DOMO: Aisee ukiwa mzembe, nyeti ndio zitaumia!

DOMO: Aisee ukiwa mzembe, nyeti ndio zitaumia!

NA MWANAMIPASHO

NDUGU zanguni leo nilikuwa niendelee na tulikoachia wiki iliyopita, ila bwana kuna haya mapya.

Hivi mnazo hizo habari za huyo soshiolaiti anayekwenda kutesekea nyuma ya nondo akila maharage kwa miaka sijui mingapi vile? Namzungumzia soshiolaiti Sheila Wairimu aliyekutwa hatiani ya kumwibia tajiri mmoja gari la kifahari aina ya Toyota V8.

Dada yenu bwana tetesi zinadai kwamba alikuwa akimpa jamaa mautamu na mahusiano yao yalikuwa chini ya maji.

Wairimu au ukipenda Shay Diva alikuwa akiishi maisha ya ki-diva sana. Maisha ya kutamanisha kweli kweli.

Sasa mzee baba alipotangulia mbele za haki, Diva akaamua haachwi mikono mitupu.

Mrembo akaamua kujihamishia umiliki wa mchuma huo wa V8 kutoka kwa tajiri hadi kwenye jina lake.

Diva alighushi stakabadhi na kubadilisha mambo kiulaini. Sasa Hakimu Mkuu wa mahakama ya Kitale juzi kamkuta na hatia ya wizi wa gari hilo.

Ndio ujue Diva alijua sasa maisha yake yanakwenda kuwa magumu kidogo baada ya kuondokewa na muhimili, alifanya mchakato huo wa kujibadilishia umiliki wa gari siku moja tu baada ya kifo cha tajiri huyo.Haiwezekani kuwa, wawili hao hawakuwa na mahusiano. Ndio afikie log book na kufanya ukarabati wake, lazima Diva alikuwa anajua vya ndani vya mwenda zake.

Diva mwenye umri wa miaka 30, alikuwa akimpa utamu tajiri huyo aliyefariki akiwa na umri wa miaka 61.

Familia ya tajiri ilikuwa inajua sema mzee akiwa hai, walishindwa kumfanyia njama Diva. Sasa dada yenu anasubiri hukumu yake Jumatatu ijayo. Amekuwa akihangaika kupinga kesi hiyo lakini sasa mambo hayamwendei poa.

Kisanga hiki kimenikumbusha kitu. Kuna mawaidha ya mamangu huwa hachoki kuwaambia dada zangu kwamba, ‘mwanamke mzembe kinachoumia zaidi ni sehemu zake za siri.’

Sasa mzee baba alifaidi mautamu, na kwa muda waliokuwa pamoja alimkabidhi sista gari atese nalo mjini bila ya kumkabidhi stakabadhi za umiliki.

Baada ya kifo, dada kwa uzembe wake akawa amejiaminisha kuwa gari ni lake na akaamua kuhamisha umiliki akitumaini atafanikiwa. Sasa mwoneni dada yenu.

Anakwenda kula maharage makavu gerezani. Natamani kumhurumia ila nashindwa sababu huyu ni bonzo. Kinachomkuta ni malipo sahihi.

Lakini hata kubwa ni kwamba hili liwe funzo kwa hawa mademu wanaotuuzia maisha feki mitandaoni. Wanaweza kukufanya ukashindwa kupumua kwa kuishi maisha ambayo ndio sisi kwenye umri huu tunahangaika kuyafikia.

You can share this post!

TAHARIRI: Muda mfupi wa kulipa Hustler Fund hakika haufai

Cherera: Raila tayari kwa mapambano

T L