• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 3:03 PM
FATAKI: Ajabu jamii kutilia shaka werevu wa binti kwa kuangalia maumbile

FATAKI: Ajabu jamii kutilia shaka werevu wa binti kwa kuangalia maumbile

Na PAULINE ONGAJI

MAJUMA kadhaa yaliyopita kulikuwa na binti fulani aliyetuzwa tuzo ya uanahabari wa sayansi ambapo hadithi yake iliangaziwa na kuchapishwa kwenye jukwaa la mtandao wa gazeti analofanyia kazi.

Makala hayo yaliandamana na picha moja mufti ya binti huyo ambapo ilionyesha uzuri wake sio tu kisura, bali kimaumbo.

Picha hiyo ilionyesha sehemu yote ya mwili wake kutoka utosini hadi miguuni, ikimulika umbo lake la chupa.

Lakini cha kushangaza ni kwamba pindi makala hayo yalipochapishwa, badala ya watu kumpongeza kwa kuafikia hayo, cheche za matusi ndizo zilizotawala kwenye sehemu ya maoni, chini ya chapisho hilo.

Kulingana na asilimia kubwa ya waliotoa maoni hayo, maafikio ya binti huyo hayakutokana na bidii yake, ila yalichochewa na mwonekano wake.

Aidha, kauli ya wengi ilikuwa kwamba hakuna jinsi binti mrembo anavyoweza kupokea tuzo za haiba ya juu hivyo, ila tu kwa kuteremshia mtu au watu fulani bendera.

Ni sawa na makala ya binti fulani wa chuo kikuu kimoja aliyetambuliwa kama mwanafunzi wa kipekee kupata alama za juu zaidi katika taasisi hiyo. Katika habari hizo, picha iliyotumika ilimuonyesha binti huyo akiwa amevalia mavazi ya kupendeza na kujipodoa kweli kweli.

Cha kushangaza ni kwamba maoni ya wengi hapo yalikuwa kuhusu mwonekano wake na wala sio maafikio yake kimasomo.

Ni jambo la kustaajabisha na kuhuzunisha, lakini huo ndio uhalisi wa jamii yetu. Tunaishi katika jamii ambapo uerevu wa mwanamke unapimwa kuambatana na mwonekao wake wa nje, yaani ikiwa una kichwa kizuri juu ya mabega yako basi haupaswi kupendeza, na ikiwa wapendeza, basi sharti kichwa chako kiwe tupu.

Nakumbuka wakati mmoja nikizungumzia kuhusu mjadala wa wanawake wanaojipodoa na wasiotumia vipodozi, ambapo nilisema kwamba hayo ni mpambo ya nje na kamwe hayaathiri kilichoko kichwani mwako. Kujipodoa au kutojipodoa hakubadilishi hali ya ubongo wako.

Cha msingi ni kwamba suala la kuwahukumu hasa mabinti kupitia mavazi au mwonekano wa nje, inathibitisha tabia ya jamii yetu ya kutosoma. Yaani, inadhihirisha uvivu wetu wa kuwa na mazoea ya kuhukumu kitabu kwa jalada lake, badala ya kupitia yaliyomo.

You can share this post!

TAHARIRI: Chanjo inatolewa sasa michezo irudi

Atwoli apewa miaka mingine mitano kutetea wafanyakazi