• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Granton Samboja arudi kwa utangazaji redioni

Granton Samboja arudi kwa utangazaji redioni

NA VALENTINE OBARA

ALIYEKUWA Gavana wa Taita Taveta, Bw Granton Samboja, amerudi kuwa mtangazaji redioni baada ya kimya cha miezi mingi tangu Uchaguzi Mkuu wa 2022 ulipokamilika.

Bw Samboja, ambaye alikuwa gavana kati ya mwaka wa 2017 hadi 2022, amekuwa nahodha wa kipindi cha ibada ambacho hupeperushwa kwa kituo cha redio kilicho kaunti ya Taita Taveta.

Kwa wikendi mbili zilizopita, alipeperusha moja kwa moja kipindi hicho kwenye mitandao ya kijamii.

“Usikate tamaa kwa sababu ya magumu unayopitia katika maisha yako,” alisema, kwenye himizo ambalo yeye hutoa wakati wa kipindi hicho cha kila wikendi.

Bw Samboja alikuwa ameshinda ugavana 2017 kupitia Chama cha Wiper lakini akahamia Chama cha Jubilee mwaka wa 2022.

Kiongozi huyo alikuwa mtangazaji redioni akahusishwa pia na umiliki wa kituo kikubwa cha redio nchini kabla ajitose kwa siasa.

Katika uchaguzi wa mwaka uliopita, aliyekuwa mbunge wa Mwatate, Bw Andrew Mwadime, ndiye aliibuka mshindi kwa kupata kura 49,901 akiwa mgombeaji huru hivyo basi kutwaa ugavana Taita Taveta. Bw Samboja alipata kura 23,703.

Katika matokeo yaliyotolewa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), aliyekuwa gavana wa kwanza kaunti hiyo, Bw John Mruttu (UDA), alipata kura 13,865 akifuatwa na aliyekuwa seneta Dan Mwazo (Wiper) aliyepata kura 11,543.

Kinyang’anyiro hicho kilikuwa kimewavutia wawaniaji 13.

  • Tags

You can share this post!

Seneta Nyutu aitaka Del Monte kukoma kuua vijana...

Alishwa kifungo cha miezi 36 jela kwa kutusi mkewe

T L