• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 6:50 PM
Kanisa alimozikwa Yesu lafungwa

Kanisa alimozikwa Yesu lafungwa

Na AFP

JERUSALEM, ISRAELI

VIONGOZI wa kidini nchini Israeli Jumatatu walifunga kanisa moja la kihistoria, ambako Yesu anaaminika kuzikwa, kulalamikia sheria mpya ya kuyatoza kodi makanisa.

Viongozi hao walisema walichukua hatua hiyo, kama juhudi za kuishinikiza serikali kuitathmini upya sheria hiyo.

Aidha, walisema kuwa kanisa hilo litabaki limefungwa hadi pale watakapotoa tangazo la kufunguliwa kwake tena.

Kanisa hilo huwa muhimu sana, kwani huwa linatumika na waumini wa makanisa ya Orthodox kutoka Ugiriki, Kanisa la Kiarmenia na Wakatoliki kuendeshea ibada zao.

Kanisa hilo linachukuliwa kuwa eneo takatifu zaidi katika dini ya Kikristo, kwani limejengwa katika eneo ambalo Yesu anaaminika kusulubiwa.

Malalamishi makuu ya viongozi ya kidini ni kwamba kodi hiyo ni sawa na kuingilia utakatifu wa makanisa.

Mbali na hayo, wanashikilia kwamba hilo litatoa nafasi kwa ufisadi kuanza katika shughuli za usimamizi wa masuala ya kanisa. “Lazima sheria hiyo itathminiwe upya ili kuhakikisha kuwa utakatifu wa kanisa umedumishwa,” akasema kiongozi mmoja.

Israeli ni baadhi ya nchi ambazo haziingilii masuala ya dini hata kidogo, ila sheria hiyo imezua hisia mbalimbali katika ulimwengu wa kidini.

 

You can share this post!

Nigeria yaanza kusaka wasichana 110 waliotekwa na Boko Haram

TAHARIRI: Haki itendewe wote Turkana

adminleo