• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 7:55 AM
Karakara ni matunda ya thamani na rahisi kuyastawisha

Karakara ni matunda ya thamani na rahisi kuyastawisha

Na SAMMY WAWERU

MATUNDA ya karakara ni kati ya yanayompa mapato ya kuridhisha kijana Robert Kirinyet, ambaye ni mkulima wa mimeamseto Kaunti ya Bomet.

Aliingilia ukuzaji wa matunda hayo mwanzoni mwa 2019, baada ya kushawishiwa na rafiki yake kazini kukumbatia mimea ya thamani.

Akiwa alianza na miche 140 ya mikarakara, kufikia sasa Kirinyet ana jumla ya 600 inayozalisha.

Anasema anaendelea kuandaa robo ekari zaidi ili kuyaongeza, kutokana na mapato ya kuridhisha anayotia kibindoni kupitia karakara.

Kwa sasa anayalima katika kipande cha shamba chenye ukubwa wa robo tatu.

Kinachomvutia zaidi katika ukuzaji wa matunda hayo, ni wepesi wake kuyapanda na kuyatunza.

Mosi, anasema ukishaandaa shamba, chimba mashimo yenye kina cha urefu wa futi moja, kuenda chini.

“Upana, mimi huyapa kipenyo (diameter) cha sentimita 15,” aelezea Kirinyet.

Kulingana na ufafanuzi wake, nafasi kati ya mashimo huipa umbali wa mita moja, na laini za mashimo mita moja na nusu.

Mkulima huyo anasema mikarakara haina ugumu kupanda, akielezea kwamba huchanganya udongo na mbolea ya mifugo; ng’ombe, mbuzi na kuku, ikizingatiwa kuwa pia ni mfugaji.

“Baada ya upanzi, shughuli muhimu ni kuitunza kwa njia ya fatalaiza, mbolea na maji ya kutosha,” anasema.

Wataalamu wa masuala ya kilimo wanasisitiza ufanisi katika kilimo cha matunda hauna siri, ila kuwa na chanzo cha maji ya kutosha.

“Kabla kuingilia kilimo cha matunda, hakikisha una chanzo cha maji ya kutosha. Isitoshe, kumbatia mfumo wa mifereji kunyunyizia mimea na mashamba maji,” anashauri Daniel Mwenda, mtaalamu.

Kulingana na mdau huyo, mataifa kama vile Israili na Misri, yameboresha kilimo cha matunda ilhali ni jangwa kwa sababu ya kukumbatia uvunaji maji.

Kando na matunzo kwa njia ya maji na mbolea, mikarakara inahitaji kusitiriwa kwa fito.

“Katika kilele cha fito, ziunganishe kwa nyaya. Mikarakara hutambaa na maumbile hayo huiwezesha kuzalisha kwa wingi na mazao bora,” asema mkulima Kirinyet.

Robert Kirinyet, mkulima wa matunda aina ya karakara Kaunti ya Bomet. Picha/ Sammy Waweru

Vile vile, ni muhimu kupogoa matawi (pruning), ili kupunguza ushindani wa lishe na kuruhusu miale ya jua kupenyeza.

Kulingana na Kirinyet, ekari moja inahitaji jumla ya fito 1, 400.

Mbali na hayo, muhimu pia ni palizi kuzuia kero ya kwekwe ambayo huchangia maenezi ya magonjwa na wadudu.

“Inapoanza kuchana maua na kutunda, wadudu aina ya vidukari ni waharibifu sana. Wasipodhibitiwa kwa dawa za wadudu, mkulima hatapata mavuno. Hula maua na matunda yanayojitokeza,” anaonya, akihimiza mkulima kuhusisha mtaalamu wa kilimo ili kushauriwa dawa bora na ambazo hazina athari kwa binadamu.

Magonjwa ya matunda pia hushuhudiwa.

Mwaka mmoja baada ya upanzi, mkulima huanza kuvuna matunda ya kwanza.

Kerinyet anaiambia Taifa Leo kwamba kwa sasa anavuna kati ya kilo 50 na 100 kila wiki, katika kipande cha shamba chenye ukubwa wa robo tatu.

“Mavuno huendelea kuongezeka kila juma,” anasema.

Ukiitunza vyema mikarakara utaivuna kati ya miaka mitano hadi minane. Soko la mazao yake ni mithili ya mahamri moto.

  • Tags

You can share this post!

Shujaa, Lionesses kurejea nyumbani leo Jumamosi kutoka raga...

Ombi la mawakili kwa kaimu Jaji Mkuu