• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 5:55 AM
Kinara wa UoN kusomewa hukumu Januari 22 kwa kuidharau mahakama

Kinara wa UoN kusomewa hukumu Januari 22 kwa kuidharau mahakama

Na RICHARD MUNGUTI

NAIBU Chancela wa Chuo Kikuu cha Nairobi Prof Stephen Kiama huenda akasukumwa jela kwa kukaidi agizo la mahakama kuu.

Kufuatia kukaidi kwa agizo la mahakama kuu, Jaji Maureen Onyango, Ijumaa alasiri wiki jana alimwamuru Prof Kiama afike kortini Januari 22, 2022 kuhukumiwa.

Jaji Onyango alimwamuru Prof Kiama afike kortini baada ya kumpata na hatia ya kukaidi agizo la Mahakama la Julai 14, 2021 ambapo alisimamishwa kufanya mabadiliko makuu katika usimamizi wa chuo hicho kikuu zaidi nchini.

Prof Kiama alipatikana na hatia ya kukaidi agizo akome kubadilisha muundo msingi wa usimamizi wa chuo hicho kikuu na kufutilia mbali vitivo kadhaa bila ya kuwashirikisha washika dau.

Agizo la kumzima Prof Kiama kufanya mabadiliko hayo bila kushauriana na wasimamizi wa vitivo mbali mbali, Wizara ya Elimu, Tume ya Elimu katika Vyuo Vikuu Nchini (CUE), mwanasheria mkuu, Waziri wa Elimu Prof George Magoha na katibu mkuu katika wizara ya elimu, lilitolewa mnamo Julai 14, 2021.

Chama cha kutetea wafanyakazi katika vyuo vikuu (Uasu) kupitia kwa wakili Titus Koceyo kilimshtaki Prof Kiama kikisema ameidharau mahakama kwa kutositisha uzinduzi wa usimamizi mpya katika Chuo Kikuu cha Nairobi (UoN).

Bw Koceyo alieleza mahakama Prof Kiama ameendelea kukaidi agizo la korti kwa kuendelea na kufutilia mbali baadhi ya vitivo na kupunguza nyadhifa za wahadhiri.

“Kutokana na kukaidi huku Prof Kiama ameagizwa afike mbele ya hii mahakama kuhukumiwa Januari 22, 2022,” aliamuru Jaji Onyango.

Jaji huyo alisema Uasu kimethibitisha kwamba Prof Kiama amekejeli na kudharau agizo la mahakama.

Jaji huyo alisema Uasu kimemsihi Prof Kiama achukuliwe hatua kali ndipo mahakama iheshimiwe.

“Prof Kiama ameidharau hii mahakama na kile kinachotakiwa ni achukuliwe hatua kali,” alisema Bw Koceyo.

Wakili huyo alisema lazima kinara huyo wa chuo kikuu ajue maagizo ya mahakama sio ubatili mtupu bali yako na nguvu na mamlaka ya kubadilisha hali katika usimamizi wa chuo kikuu.

Uasu kimewashtaki Prof Kiama, tume ya kuajiri watumishi wa umma, mwanasheria mkuu na CUE.

Katika kesi hiyo, Uasu kinaomba mahakama ipige kalamu mageuzi ya usimamizi wa UoN yaliyotangazwa na Prof Kiama na mwenyekiti wa baraza la elimu katika vyuo vikuu Prof Julia Ojiambo.

Uasu kimeomba mahakama itoe maagizo ya kudumu kwamba Prof Kiama akome kuvuruga usimamizi wa UoN.

“Baada ya kusikiliza kesi ya Uasu, hii mahakama imesema madai dhidi ya Prof Kiama yako na mashiko kisheria. Prof Kiama ameagizwa akome kuyafanyia mabadiliko aliyotangaza,” Jaji Onyango aliamuru.

Prof Magoha aliunga mkono kesi hiyo akisema kinara huyu wa UoN hakufanya mashauriano alipoashiria kufanyia marekebisho usimamizi wa UoN.

You can share this post!

Saba wafariki kwenye ajali matatu zilipogongana Kaunti ya...

Walioingiza raia wa Ethiopia watozwa faini ya Sh60 milioni

T L