NA AFP
KIGALI, RWANDA
MSHUKIWA wa ufadhili wa mauaji ya halaiki mnamo 1994 nchini Rwanda, Felicien Kabuga, kesho Alhamisi atafikishwa katika Mahakama ya Kimataifa ya Kushughulikia kesi za Uhalifu jijini The Hague, Uholanzi.
Mshukiwa huyo ameshtakiwa kwa mauaji ya halaiki na kukiuka haki za binadamu kufuatia jukumu lake katika mauaji hayo yaliyotokea miaka 28 iliyopita.
Upande wa mashtaka na ule wa utetezi zinatarajiwa kutoa maelezo yao ya ufunguzi kesho na Ijumaa, na ushahidi katika kesi hiyo kuanza kuwasilishwa Jumatano ijayo.
Waendesha mashtaka wanadai Kabuga alisaidia kuanzisha vyombo vya habari vya kupeperusha habari za chuki, ambapo aliwataka Wahutu kuua ‘mende wa Kitutsi’.
Kabuga alikamatwa nchini Ufaransa mnamo Mei 2020 baada ya kuwakwepa polisi katika nchi kadhaa kwa muda mrefu.Baada ya kukamatwa, alihamishwa hadi mahakama iliyoundwa kukamilisha kazi ya mahakama ya uhalifu Rwanda jijini Arusha, Tanzania ambayo haitumiki kwa sasa.
Kabuga, ambaye inasemekana kuwa na afya dhaifu, alifika mbele ya majaji Agosti akiwa kwenye kiti cha magurudumu na haikujulikana kama atafika mahakamani kesho Alhamisi ama majaji watamruhusu kuhudhuria vikao kupitia mtandao.
Awali Kabuga alipangiwa kufika mahakamani Arusha, lakini majaji waliamua kwamba angesalia katika Mahakama ya Kitaifa hadi itakapoamuliwa vinginevyo.
Mwezi Juni, majaji walipinga maelezo ya upande wa utetezi walipoamua kuwa Kabuga alifaa kujibu mashtaka.Umoja wa Mataifa unasema watu 800,000 waliuawa nchini Rwanda mwaka 1994 katika mashambulio ya siku 100.
Kabuga anadaiwa kusaidia kuunda kundi la wanamgambo wa Kihutu la Interahamwe na Radio-Television Libre des Mille Collines (RTLM), ambayo matangazo yake yaliyochochea watu kuuawa.
Zaidi ya mashahidi 50 wanatarajiwa kutoa ushahidi wao kuhusiana na kesi hiyo.
Waendesha mashtaka walisema Kabuga alidhibiti na kuhimiza matangazo ya RTLM na kukitetea kituo hicho wakati waziri wa habari alipokosoa matangazo hayo.
Kabuga pia anatuhumiwa kwa ‘kusambaza mapanga’ kwa vikundi vya mauaji ya halaiki, na kuwaamuru kuwaua Watutsi.
Kufuatia kukamatwa kwake katika nyumba ndogo karibu na Paris, mawakili wake walidai kuwa Kabuga, ambaye ana umri wa miaka 87, anapaswa kushtakiwa nchini Ufaransa kwa sababu za kiafya.
Hata hivyo, mahakama kuu ya Ufaransa iliamua kwamba anapaswa kuhamishwa chini ya ulinzi wa Umoja wa Mataifa, kulingana na hati ya kukamatwa iliyotolewa mnamo 1997.
Waathiriwa wa mauaji hayo wametoa wito kesi hiyo isikizwe haraka kabla ya Kabuga kufa.
Subscribe our newsletter to stay updated