• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Mchepuko wavuruga harusi siku ya mwisho

Mchepuko wavuruga harusi siku ya mwisho

MASHIRIKA na PETER MBURU

MWANAMKE mmoja Uingereza ameshangaza ulimwengu baada ya kuvuruga harusi kati yake na mumewe dakika za mwisho, alipogundua kuwa mumewe huyo alikuwa akimchepukia.

Shirika moja la habari kutoka UK liliripoti kuwa Casey* na Dan* (majina yasiyo yao) walikuwa wamepanga harusi kwa njia bora kabisa, lakini usiku wa mwisho kabla ya siku ya harusi Casey akabaini kuwa Dan alikuwa na uhusiano mwingine.

Hii ilikuwa baada ya Casey kupokea jumbe kwenye simu yake zikibeba skrinishoti zilizoonyesha namna mumewe Dan alikuwa akizungumza na mpango wake wa kando, na hata picha za selfie ambazo walikuwa wamepiga wakiwa pamoja.

Inadaiwa kuwa mwanamke huyo, ambaye pamoja na mumewe wana watoto wawili, alilia alipokuwa akipitia jumbe hizo, mara moja akibaini kuwa hatimaye mapenzi kati yake na mumewe yalikuwa yameisha.

Baadhi ya jumbe zilisema “Wikendi hii, mimi na wewe. Tutakuwa na mambo moto, leta mchezo wako.”

Mwingine ulisema “Mwili wako ni mzuri sana na natumai unafahamu jinsi ya kuutumia.”

Alitumiwa na nambari asiyoijua, huku ikimwambia “Ingekuwa ni mimi singemuoa. Utamuoa?”

Mwanamke huyo alisema kuwa kilichomshangaza pia ni kuwa jamaa alimwambia mpango wa kando kuwa alikuwa na maumbile kinyume kabisa na ya Casey, akiongeza “Sijawahi kuwa na uhusiano wa aina hii mbeleni.”

Japo marafiki zake walimshauri ampigie Dan na kumwambia kuwa harusi imekatika, Casey aliamua kulipiza kisasi kwa njia ya aina yake.

“Nilipokuwa nikipita kanisani, miguu haikuwa na nguvu na vazi langu la harusi lilipoteza maana na kuwa vazi tu. Alipoona uso wangu, alijua sikuwa mwanamke mwenye furaha haswa siku hiyo lakini hakufahamu kilichomsubiri,” Casey akasema.

Alipofika mbele, umati ulishtuka kumsikia akitangaza kuwa hakuna harusi ingefanyika, akieleza “Inaonekana Dan si mtu niliyemdhani kuwa ndiye.”

Baadaye aliweka maua chini na kutoa simu yake, kisha akaanza kusomea familia na marafiki jumbe alizotumiwa.

Wakati huo huo, jamaa naye alitoka nje ya kanisa mbio mbio, huku akiandamwa na mwanaume aliyekuwa msimamizi wake wa harusi

Mwanamke huyo baada ya kutoboa ukweli huo anadaiwa kwenda kujiburudisha vilivyo, kusherehekea kuwa alipata ukweli mapema.

You can share this post!

Kenya inaongoza Afrika kwa ukarimu – Utafiti

Zoezi la kiusalama lasababishia abiria na wafanyakazi...

adminleo