• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:58 PM
MIMBA ZA MAPEMA: Chifu aliyejitolea kukuza maadili katika jamii

MIMBA ZA MAPEMA: Chifu aliyejitolea kukuza maadili katika jamii

Na RUSHDIE OUDIA

HUKU taifa likiduwazwa na idadi kubwa ya wasichana wa shule za msingi na upili wanaogonga vichwa vya habari kwa kushika mimba za mapema, wakazi wa eneo la Nyawita, Maseno, Kaunti ya Kisumu, wanatamani enzi ambapo walikuwa na chifu mchapa kazi.

Mojawapo ya hatua ambazo zimechukuliwa na serikali kuu kutatua janga hilo la wasichana wadogo kupata uja uzito ni kutoa onyo kwa machifu ambao wamezembea kazini, kwani inaaminika baadhi yao hujihusisha katika maelewano kati ya familia za wasichana wanaonajisiwa ili wahusika wakwepe adhabu za kisheria.

Katika kata ndogo ya Nyawita, Chifu Mstaafu Harrison Okwema, amesalia kuwa maarufu na kipenzi cha wengi kwa misimamo mikali ya kunyorosha maadili katika jamii, aliyokuwa akichukua kabla kustaafu kwake miaka miwili iliyopita.

Bw Okwama, ambaye kwa sasa ana umri wa miaka 64 anasifika sana kwa juhudi zake katika kukabiliana na ukahaba, utengenezaji pombe haramu hasa katika mtaa duni wa Obunga na kuwakabili wahalifu.

Juhudi zake zilirejesha hali ya nidhamu katika mtaa huo duni. Kutokana na kuwa jina lake na sura yake pekee zilitosha kuwatia wasiwasi waliotaka kuthubutu kupotoka kimaadili, alikuwa akiweka picha yake nje ya afisi alimohudumu, hali iliyoonekana kuwatia wasiwasi wahalifu.

Kwa sasa, umaarufu wake unalinganishwa na machifu wa awali kama Chifu Onunga wa Kisumu na Chifu Odera Akang’o, ambao walihudumu miaka mingi iliyopita. Machifu hao waliogopwa sana na wakazi kutokana na ukakamavu mkubwa wa kinidhamu katika utendakazi wao.

Bw Okwama amemwoa Bi Ludia Adoyo, na ni baba wa watoto watatu. Na licha ya ukakamavu wake kazini, mojawapo wa sifa zake kuu ni kuwa mcheshi.

Hata hivyo, hilo halikumfanya kushawishiwa na vitendo vya wahalifu. Alibaki mtetezi mkuu wa serikali ya kitaifa, hali iliyomfanya kujipatia umaarufu mkubwa unaomfuata hata baada ya kustaafu.

Wakati ‘Taifa Leo’ ilipomtembelea katika mtaa wa Migosi, alikuwa akiendelea na shughuli zake za kawaida.

Chifu huyo alizaliwa katika eneo la Kitutu Chache, Kaunti ya Kisii. Alisomea katika Shule ya Msingi ya Ong’icha ambapo baadaye alijiunga na Shule ya Upili ya Agoro Sare katika eneo la Oyugis, Kaunti ya Homa Bay. Alifanya Mtihani wa Baraza la Afrika Mashariki (EAEC) mnamo 1979.

Baadaye, alijunga na Kampuni ya Sukari ya Chemelil kutoka 1981 hadi 1988. Baada ya kuhudumu huko, alifanya kazi katika Wizara ya Kazi za Umma kama fundi wa mitambo kwa miaka sita.

Akiwa humo, serikali ilitangaza kazi katika za utawala wa mkoa, ambapo alituma maombi.

Aliitwa katika mahojiano na kupita. Aliajiriwa kama Naibu Chifu wa Kata Ndogo ya Nyawita alikohudumu hadi kustaafu kwake mnamo 2016. Baadhi ya maovu anayochukia hadi sasa ni ukahaba, wizi wa mabavu na ulevi.

“Nachukia sana pombe haramu, hasa zinazotengenezewa sehemu za Alego na Ugenga. Vile vile, nawachukia sana makahaba ambao huendesha shughuli zao hasa katika mtaa wa Kondele. Hao ndio wanawapotosha vijana wengi na kupoteza mwelekeo katika maisha yao. Hilo ndilo lilinifanya kuendeleza -misako mikali dhidi yao na kuwakamata,” akasema.

Katika kuukabili ukahaba, Bw Okwama alikuwa akiwakamata wasichana wadogo ambao walikuwa wakijihusisha katika vitendo hivyo na kuwapeleka katika vituo vya polisi vya Kondele na Obunga.

Hili lilimfanya kupendwa zaidi na wakazi, kwani suala la ukahaba miongoni mwa watoto limebaki kuwa tatizo sugu miongoni mwao.

Anaeleza kuwa alifanikiwa kupata habari kuhusu visa vilivyokuwa vikiendelea katika maeneo fiche kutokana na ushirikiano mwema na wakazi.

“Walikuwa wakinieleza kuhusu maovu yote yanayoendelea. Hilo liliifanya kuwa rahisi kuwakabili wahalifu wote waliohusika au kushiriki katika vitendo vyovyote vile,” anaeleza.

Kutokana na juhudi zake, baadhi ya mafanikio makuu aliyopata ni kupunguza kiwango cha ulevi katika eneo hilo. “Nilifanikiwa kupunguza ulevi katika kata ya Nyamita kwa zaidi ya asilimia 50,” asema.

Zaidi ya hayo, anajivunia kuwaondoa wahalifu katika kata hiyo, hali iliyowafanya kutorokea maeneo kama Riat na milima ya Nyahera.

“Wakati nilistaafu, nilizungumza na naibu chifu mpya, ambapo nilimwambia kuendeleza kazi yangu kwani ndipo ataweza kupata uungwaji mkono kutoka kwa wakazi,” akasema.

Baadhi ya mambo anayojivunia ni kutokamatwa au kushtakiwa kwa kujihusisha na kitendo chochote cha uhalifu katika muda wote aliohudumu kama naibu chifu.

Kwa sasa, Bw Okwama anajihusisha na kilimo katika kaunti za Kisii na Kisumu.

Na licha ya kustaafu kwake, anaamini kwamba bado ana uwezo wa kuwahudumia wananchi ikiwa anaweza kupewa nafasi ya msimamizi wa wadi ama kijiji chini ya mfumo mpya wa ugatuzi.

Asema kuwa anaweza kutumia mbinu zizo hizo katika utendakazi wake. “Ikiwa ninaweza kupewa jukumu hilo, nitatumia tajriba yangu kubwa kwa manufaa ya wananchi,” aliongeza.

Na kwa kuwa eneo hilo lina uongozi mpya, hakuwa na budi ila kuondoa picha yake iliyokuwepo afisini na kuipeleka nyumbani kwake Kisii.

Wakazi wanamsifia kwa kutekeleza yale yote aliyoyasema au kuahidi. “Ni mtu wa kipekee ambaye tungali tunatamani kuwa naye,” mkazi Collins Omondi, aliambia Taifa Leo.

You can share this post!

Japo Tottenham hawakujisuka upya, wanayo makali ya...

Afrika Kusini yaahidi mabinti wa kikosi cha soka mamilioni...

adminleo