• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Mume, 55, achapa mamaye akitaka kujua babaye

Mume, 55, achapa mamaye akitaka kujua babaye

Na JOSEPH NDUNDA

MWANAMUME mwenye umri wa miaka 55 ameshtakiwa kwa madai ya kumpiga mama yake, 88, akitaka aambiwe baba yake ni nani.

John Kinuthia ameshtakiwa pia kwa uharibifu wa mali alipompiga mama yake, Bi Naomi Kamuyu, nyumbani kwake Riruta, Nairobi mnamo Januari 21.

Alikanusha mashtaka mbele ya Hakimu Mkuu Mwandamizi Derrick Kuto, katika Mahakama ya Kibera, Kaunti ya Nairobi.

Imedaiwa mshukiwa alimpiga mama yake ngumi kwenye mapafu na kumjeruhi kisha akatupa mikongojo yake. Mama yake alipiga kelele na kuokolewa na wananchi.

Katika kosa la kusababisha uharibifu, Bw Kinuthia alisemekana kukata mkoba wa mama yake, uliogharimu Sh200, vipandevipande, na kuharibu simu yake ya mkononi iliyokuwa ndani ya Sh15,000.

Mwanamume huyo aliye kitinda mimba, alishtakiwa pia kwa kuzua rabsha alipotishia kumuua mama yake kwa kisu. Yasemekana alimshambulia mama yake akitaka apewe sehemu ya nyumba za kukodisha ili awe akikusanya kodi, lakini mamaye akakataa.

Mshukiwa amedaiwa kutaka aambiwe babake yuko wapi ili afahamu ukoo anakotoka lakini mamake alimjibu kwamba hajui babake ni nani.

Kupitia kwa wakili wake, aliambia mahakama familia inatatua mzozo huo na kuna uwezekano wataafikiana nje ya mahakama. Aliachiliwa kwa bondi ya Sh100,000 au Sh30,000 pesa taslimu.

  • Tags

You can share this post!

Vijana wakosa nafasi KDF kwa kutumia vyeti feki

Kambi yafungwa ili kudhibiti corona