• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:30 PM
Naivas yawapa wahudumu wa afya wa Thika Level 5 vyakula na sabuni

Naivas yawapa wahudumu wa afya wa Thika Level 5 vyakula na sabuni

Na LAWRENCE ONGARO

WAHUDUMU wa afya katika hospitali ya Thika Level 5 wapatao 100 walipokea vyakula kutoka kwa supamaketi ya Naivas tawi la Thika.

Daktari mkuu katika hospitali hiyo Jesse Ngugi, alithibitisha jambo hilo akisema hiyo ni njia moja ya kuwapa matumaini wahudumu hao kuwa pia wanatambulika “kule nje.”

“Kwa niaba ya hospitali, tunashukuru sana dukakuu la Naivas kwa kuonyesha ukarimu wao wa kuwajali wengine. Wameonyesha ya kwamba kutoa kwa umma ni jambo la kujitolea na ni kutoka moyoni,” alisema Dkt Ngugi.

Alisema wahudumu hao wa afya katika hospitali hiyo wamajitolea mhanga kukabiliana kwa vyovyote kuwahudumia wagonjwa bila kusita.

“Kwa wakati huu tumejiandaa vilivyo ambapo tumetenga wadi maalum ya kuwaweka wagonjwa endapo watapatikana na Covid-19. Wodi hiyo ina vitanda 10,” alisema Dkt Ngugi.

Alisema masharti yaliyowekwa na serikali ya kudumisha usafi na hasa kunawa mikono, yameleta mabadiliko makubwa kwa mwananchi wa kawaida.

“Siku hizi hata homa ya kawaida imepungua pamoja na maradhi ya kuharisha na homa ya matumbo,” alisema Dkt Ngugi.

Kudumisha usafi

Alitoa mwito kwa wananchi popote walipo wazidi kudumisha usafi kwa sababu “tutapunguza magonjwa mengi kwa  asilimia 70 hivi.”

Hafla hiyo iliyofanyika Jumatatu iliwaacha wahudumu hao na mshangao kwani hawakutarajia ukarimu kama huo ungeonekana siku hiyo.

Baadhi ya vyakula walivyopokea ni unga wa ugali, sharubati, sabuni ya kuoga na ya kufua nguo, mchele, na sukari, ambapo kila kifurushi kiligharimu Sh2,000.

Kampuni hiyo ya Naivas, kwa niaba ya wasimamizi wake, iliwapongeza wahudumu hao kwa kazi ngumu wanayofanya ya kutibu wagonjwa bila kusita.

Ilizidi kusema ya kwamba watazidi kushirikiana na hospitali ya Thika Level 5 na kila mara kukiwa na haja watawatembelea tena na mazuri.

You can share this post!

Chama cha maslahi ya wanasoka chataka majadiliano kabla...

Jinsi kikundi kinavyosaidia jamii wakati huu wa janga la...

adminleo