• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 5:54 PM
KURUNZI YA PWANI: Waganga 20 sasa waililia serikali iwatambue

KURUNZI YA PWANI: Waganga 20 sasa waililia serikali iwatambue

Na CHARLES LWANGA

KUNDI la waganga 20 eneo la Magarini, Kaunti ya Kilifi wameitaka serikali itambue kazi yao ya kutibu wagonjwa ili waepuke kushambuliwa na umma kwa madai ya kufanya uchawi.

Kundi hilo linaloongozwa na Bi Dahabu Ngumbao lilisema linataka kutambuliwa na serikali na kupewa leseni itakayowawezesha kuendelea na ‘kazi yao nzuri’ ya kutibu wagonjwa bila haya na uwoga wowote.

“Hii ni kwa sababu kizazi cha sasa ambacho hakitambui mila na utamaduni hutusingizia kuwa tunafanya uchawi, kisha wanauwa wazee hao bila sababu yoyote,” alisema na kuongeza kuwa “jambo hili limeweka maisha yetu hatarini kwani wazee huuliwa kila uchao kwa madai ya uchawi.”

Wakizungumza na wanahabari katika eneo la kimatamaduni huko Gongoni, alisema hakuna haja yoyote ya serikali kupiga vita waganga na akasisitiza kuwa wanatelekeleza kazi yao kulingana na utamaduni.

“Tunatibu watu kutumia tiba za kiasili baada ya kurithi na kusomea tiba za kiasili msituni,” alisema na kuongeza “pia tunatibu mapepo yanayomwingia mtoto mchanga kichwani wakati wa kuzaliwa ambazo humfanya ajae maji kichwa.” Bi Ngumbao ambaye pamoja na wenzake walizungukazunguka nyungu iliyowekwa tiba za kiasili huku wakiimba, alisema amefanya kazi hiyo kwa miaka 55 baada ya kurithi uganga kutoka kwa nyanya zake.

Vilevile, alisema leseni itapatia umma imani kufanya waondolewe lawama itakayopunguza visa vya mauwaji ya wazee kwa madai ya kufanya uchawi.

“Tunataka serikali ituruhusu tubebane na vifaa na tiba zetu hadi hospitali ili tusaidie wauguzi wa kisanyansi na utaalamu wetu wa kitamaduni,” alisema.

Mguzi huyo alisema wanaujuzi wa kutibu baadhi ya magonjwa sugu wanayosumbuwa jamii kwa bei nafuu kama vile Sh1,000 pekee.

Isitoshe, Bi Ngumbao alizidi kusema kuwa wanaotafuta hudumu zao kwa sasa ni wazee ambao ni waaminifu kwa mila na utamaduni ya jamii ya Mijikenda.

Kulingana na idara ya polisi, takriban wazee 400 wasiokuwa na hatia haswa mababu na wajane wameuwawa na umma kwa kipindi cha miaka mitano zilizopita kwa madai ya uchawi katika Kaunti ya Kilifi pekee.

You can share this post!

OBARA: Ujeuri wa MCAs ni tishio kwa ufanisi wa ugatuzi

Wanasoka wa mashinani wapata fursa ya kuchuana na wabunge

adminleo