Safari za ngámbo mwanya mkubwa wa ufujaji kwenye kaunti
KAUNTI hazifai kuitisha fedha zaidi ilhali kiasi cha pesa zinazoelekezwa kwenye miradi ya maendeleo ni finyu huku uongozi, maafisa na madiwani nao wakijivinjari na hela kupitia ufisadi na ziara za ngámbo.
Ripoti ya Mdhibiti wa Bajeti (COB) imefichua kuwa kaunti zilitumia Sh1 bilioni katika ziara za nje, japo matokeo ya ziara hizo hayaonekani kimaendeleo.
Kaunti 30 ziliorodheshwa kati ya zile ambazo maafisa wake na madiwani walienda ziara za nje huku wakitumia mamilioni ndani ya miezi minane pekee.
Jambo la kusikitisha ni kuwa baadhi ya malengo ya ziara hizo hayashangazi tu bali yanachekesha.
Kuna afisa wa Kaunti ya Nakuru ambaye alitumwa kujifunza kuhusu matumizi ya mfumo wa malipo ya IFMIS kule Tanzania. Kwani hayo mafunzo hayangefanyika nchini?
Aidha maafisa wengine sita kutoka Kaunti ya Bungoma nao walihudhuria Kongamano Kuhusu Kuteka na kuyahifadhi maji ya mvua lililofanyika China. Maafisa hawa walitumia Sh3 milioni.
Ni kipya au kikubwa zaidi ambacho maafisa hawa wangejifunza kuhusu kuyahifadhi maji ya mvua?
Si wangeenda hata Bwawa la Kiambere wajifunze kuhusu jinsi maji yanavyohifadhiwa na kilimo cha unyunyuziaji mashamba maji?
Aidha kaunti nyingi ziliorodhesha kuwa magavana na madiwani walikuwa wakienda mafunzo kuhusu hili ama lile, mambo ambayo yanaweza kufanywa hapa nchini na pesa zinazotumika kuelekezwa kwenye miradi ya maendeleo.
Ripoti ya COB inaonyesha wazi kuwa ziara ambazo zimekuwa zikifanyika ngámbo za maafisa wa kaunti, madiwani na hata magavana ni za kujistarehe na kufyonza hela tu.
Kinaya ni kuwa kaunti zimekuwa zikipigania ziongezewe mgao wao katika mwaka huu wa kifedha hadi Sh465 bilioni na kuzua mvutano mkubwa na wabunge.
Hata Sh415 bilioni ambazo sasa watapokea mwaka huu wa kifedha baada ya muafaka kuafikiwa, hazitakuwa na maana iwapo mtindo utakuwa tu huu wa kujivinjari na uporaji
Ni wazi hakuna haja hata kaunti kuitisha hela zaidi ilhali pesa nyingi wanazielekeza katika ulipaji mishahara na kujivinjari kuhusu miradi ya maendeleo.
Magavana wamekuwa wakitaka wapewe pesa na waruhusiwe wasimamie Hazina ya Ustawi wa Maeneobunge Nchini (CDF) na pia Ada ya kukarabati barabara nchini.
Mbona wasiutumie mgao wa sasa kwa hekima kabla ya kuitisha hela zaidi?
Ugatuzi utafaulu tu iwapo hela zitakuwa zikitumiwa vizuri kwenye kaunti na si hii hali ambapo watu wachache ndio hunufaika kupitia wizi