Tahariri

TAHARIRI: Ni aibu kwa polisi kushiriki uhuni ili kufaidi wanasiasa

Na MHARIRI MKUU February 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KATIKA taifa linalojivunia misingi ya demokrasia na utawala wa sheria kama Kenya, ni jambo la kusikitisha na kuaibisha kushuhudia wale waliokabidhiwa jukumu la kulinda Katiba wakigeuka na kuwa wakiukaji wake wakuu.

Idara ya Polisi, ambayo kikatiba inapaswa kuwa huru na isiyopendelea upande wowote wa kisiasa, imejikuta mara kwa mara katika lawama za kushiriki uhuni na hata kushirikiana na wahuni ili kukandamiza upinzani.

Katika siku za hivi majuzi, taifa limeshuhudia visa vya kutisha ambapo polisi wamenaswa na wanahabari wakivamia mikutano halali na hata maeneo matakatifu ya ibada.

Tukio la uvamizi wa Kanisa la ACK Witima katika Kaunti ya Nyeri liliacha wengi vinywa wazi.

Wakati wa ibada iliyohudhuriwa na viongozi wa upinzani wakiongozwa na Rigathi Gachagua, polisi walirusha vitoza machozi ndani ya kanisa.

Kitendo hicho si tu ukiukaji wa haki ya kuabudu, bali ni dharau kwa taasisi za kidini.

Si hilo tu. Jumapili, katika mkutano wa hadhara wa mrengo wa Orange Democratic Movement (ODM) unaoongozwa na Seneta wa Nairobi na Katibu Mkuu wa chama hicho, Edwin Sifuna, polisi walinaswa wakirusha tena vitoza machozi kuwatawanya wafuasi.

Badala ya kulinda haki ya wananchi kukusanyika kwa amani kama inavyolindwa na Katiba, walionekana kutekeleza maagizo ya kisiasa ya kuwanyamazisha wakosoaji wa serikali.

Hali haikuwa tofauti hapo jana katika jiji la Nairobi, eneo la Nyamakima, ambapo mkutano mwingine wa upinzani uliohudhuriwa na Kalonzo Musyoka pamoja na Rigathi Gachagua ulitibuliwa kwa kurushiwa vitoza machozi.

Matukio haya yanajenga taswira kuwa baadhi ya maafisa wa polisi wamegeuka kuwa chombo cha kisiasa badala ya kuwa walinzi wa sheria.

Aibu kubwa zaidi ni pale ambapo polisi wanaonekana kushirikiana na wahuni kuwavurugia wapinzani mikutano.

Badala ya kuwakamata wahuni na kuwafikisha mahakamani, wakati mwingine polisi huonekana wakiwaangalia tu au hata kuwapa ulinzi.

Hii inazua maswali mazito kuhusu uhuru na uwajibikaji wa Idara ya Polisi.

Iwapo taasisi za usalama zitageuzwa kuwa silaha za kisiasa, demokrasia yetu iko hatarini.

Wananchi watapoteza imani kwa vyombo vya dola, na hali hii inaweza kuchochea machafuko na migawanyiko ya kitaifa.

Ni muhimu kwa viongozi wa serikali kuheshimu uhuru wa polisi na kwa maafisa binafsi kukumbuka kiapo chao cha kulinda Katiba bila woga wala upendeleo.

Ni wajibu wa vyombo huru vya uangalizi, asasi za kiraia na wananchi kwa ujumla kudai uwajibikaji.

Polisi wanapaswa kurejea katika mstari wa sheria na maadili, wakikumbuka kwamba mamlaka waliyo nayo ni kwa manufaa ya wote, wala si kwa ajili ya kuwakandamiza wale wenye maoni tofauti.