• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 6:55 AM
HADITHI FUPI: Majibu kwa maswali ya ‘Shibe Inatumaliza’

HADITHI FUPI: Majibu kwa maswali ya ‘Shibe Inatumaliza’

YAFUATAYO ndiyo majibu kwa maswali ya juma lililopita kuhusu hadithi ‘Shibe Inatumaliza’ iliyoandikwa na Salma Omar Hamad.

Rejelea makala ya wiki jana.

(a) Eleza muktadha wa dondoo. (alama 4)

Haya ni maneno yake Mbura akizungumza na Sasa. Wamehudhuria sherehe nyumbani mwake Mzee Mambo. Wanajadiliana namna wamekula awamu tatu na bado watazidi kula.

(b) Tambua mtindo wa lugha unaotawala dondoo hili. (alama 2)

Mbinu ya jazanda imetawala dondoo. ‘Kula’ kunarejelea namna viongozi, wanaowakilishwa na Sasa na Mbura, hutumia rasilmali ya jamii kwa manufaa yao.

c) Toa mifano mingine minne ya mtindo huu katika hadithi nzima. (alama 4)

(i) Chakula kinawakilisha rasilmali ya nchi.

(ii) Kujirudiarudia kwenye foleni ya chakula inaashiria namna viongozi hukwamilia uongozini wakinuia kuendeleza umbilikizaji wa mali.

(iii) Kupakua mshahara kufanywao na mzee Mambo kunarejelea viongozi kujiamulia kiwango cha ujira wao, bila kuzingatia kazi iliyofanywa au pato la nchi.

(iv) Mbura anataarifiwa na mtu aliyempigia simu kuwa wanaonekana kwenye vyombo vya habari kwani sherehe inarushwa moja kwa moja. Ina maana umma umeng’amua viongozi wao wanatumia mamlaka yao kujitajirisha. Hawawajali wananchi, wanaowakilishwa na mpigaji simu.

(Kuna mifano mingine. Tafiti).

d) Ukiwarejelea wahusika wowote watatu kwenye hadithi, thibitisha namna viongozi wanafuja rasilmali ya umma. (alama 10)

(i) Mzee Mambo

Anapokea mshahara licha ya kuwa hana kazi maalumu. Anashikilia wadhifa wa waziri wa kivuli wa wizara zote, na kila wizara tayari ina mhusika wake ambaye anafahamika.

‘Anachota mshahara’- kujiamulia atakavyolipwa bila kujali kwamba hana mchango wowote katika ustawi wa uchumi wa jamii husika.

Magari ya serikali yanatumika kusafirisha wanaohudhuria sherehe na vitu vinavyotumika huko kama mapambo, maji na ikilazimika, watoto kuenda kuogeshwa.

Sherehe hii ya kuadhimisha mwanawe kifungua mimba kuingizwa nasari skuli na wa pili kuota meno inarushwa moja kwa moja kwenye televisheni ya taifa.

(ii) DJ

DJ anachota mabilioni ya fedha za serikali ili kutumbuiza kwenye sherehe hii, na yeye si mfanyikazi wa serikali.

Anamiliki duka kubwa la dawa ambalo mtaji wake ni bohari kuu ya dawa za serikali.

Halipii huduma za msingi kama wananchi wengine. Anapata maji, umeme, matibabu na huduma zote za msingi bure.

(iii) Sasa na Mbura

Wanapokea mshahara na wametelekeza wajibu wao kwani kinachothaminiwa ni kuenda kazi, sio kufanya kazi.

Wanapokuwa shereheni, wanarudia kupakua chakula mara tatu, ishara ya ulafi. Wanashiriki katika ubadhirifu wa mali kwani hawatosheki.

Wizara wanayosimamia, ya mipango na mipangilio, ndiyo muhimu kuliko wizara zote serikalini. Wanashinda wakipanga na kupangilia mambo bila utaratibu. Ina maana serikali haina mwelekeo, na inazidi kuwalipa licha ya kuwa hawana wafanyacho.

Maswali mengine yatajibiwa wiki ijayo.

Grace Ogoye

Kisumu Girls High School

You can share this post!

Matapeli wavuna vya haramu kupitia bandari ya Lamu

Hofu visa vya kaswende kwa wajawazito kuzidi

T L