NA VALENTINE OBARA
UCHAGUZI na uteuzi wa wanasiasa wa Kaunti ya Kilifi kwa nyadhifa kubwa bungeni huenda ukabadili pakubwa siasa za Pwani, kwa mujibu wa wachanganuzi wa siasa.
Kwa muda mrefu, Kaunti ya Mombasa ndiyo ilichukuliwa kuwa ngome kuu ya siasa za Pwani ambapo wanasiasa wa kaunti hiyo waliteka mioyo ya vigogo wa siasa za kitaifa.
Hata hivyo, wadadisi wanasema hatua ya vyama na miungano mikuu ya kisiasa kuwachagua wanasiasa wa Kilifi kwa viti vikubwa bungeni, ni ishara ya mabadiliko ya mawimbi ya kisiasa Pwani.
Huku aliyekuwa gavana wa Kilifi, Bw Amason Kingi akiwa tayari ashachaguliwa kuwa Spika wa Seneti, Chama cha UDA kilimteua Mbunge wa Kilifi Kaskazini, Bw Owen Baya, kuwa naibu kiongozi wa wengi katika bunge la taifa kuwakilisha Kenya Kwanza.
Bw Kingi aliteuliwa na Kenya Kwanza kuwa spika kupitia chama chake cha PAA alichotumia kumpigia debe Rais William Ruto, katika uchaguzi uliopita.
Kwa upande wake, ODM ilimteua Seneta wa Kilifi, Bw Stewart Madzayo, kuwa kiongozi wa wachache katika seneti. Bw Madzayo anatumikia kipindi chake cha tatu katika seneti.
Kulingana na mchanganuzi wa siasa, Bw Collins Ouma, hatua ya vyama vikuu kukabidhi wanasiasa wa Kilifi nyadhifa zilizo na ushawishi mkubwa kisiasa, huenda ikawa ni mbinu mpya ya kutaka kudhibiti siasa za Pwani kuelekea kwa Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Bw Ouma anasema kuwa, kwa upande mmoja, Kenya Kwanza itahitaji kujiongeza umaarufu katika kaunti hiyo iliyo ya pili kwa wingi wa idadi ya wapigakura Pwani, huku ODM ikitaka kudhibiti umaarufu wake.
“Inaonekana hii ni mikakati inayolenga siasa za siku za usoni. UDA haikufanya vyema kwa matokeo ya urais Kilifi na mbinu bora kubadili hali hii ni kwa kujenga urafiki. Kwa ODM, mpango wao ni kujikinga kutokana na makombora yanayorushwa na Kenya Kwanza ili isipoteze umaarufu wake,” akasema.
Kwa mujibu wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), Kaunti ya Mombasa ndiyo ina idadi kubwa ya wapigakura waliosajiliwa ambao ni 642,362 ikifuatwa na Kilifi iliyo na wapigakura 588,842, kisha Kwale 328,316.
Katika matokeo ya uchaguzi wa urais, kinara wa ODM, Bw Raila Odinga, aliongoza kwa idadi ya kura katika kaunti zote za Pwani ingawa waliachana na Dkt Ruto kwa asilimia 17 pekee za kura Mombasa.
Hata hivyo, ODM ilizoa viti vitano kati ya sita vya ubunge mbali na ugavana, useneta, uwakilishi wa wanawake na madiwani 23 kati ya 30.
Katika Kaunti ya Kilifi, Bw Odinga alimlemea Dkt Ruto kwa kura za urais walipoachana na asilimia 44.
Hata hivyo, ODM iliteleza kwa kupoteza baadhi ya viti vya ubunge na udiwani ilivyoshikilia katika mabunge yaliyopita, kufuatia kuingia kwa PAA ulingoni.
“Kenya Kwanza ikifanikiwa katika mpango huu wake wa kutaka kupenya zaidi Kilifi, itaathiri ODM katika ukanda wa Pwani,” akasema Bw Ouma.
Inasubiriwa kuonekana jinsi serikali ya Kenya Kwanza itakavyogawa nyadhifa nyingine zilizobaki ikiwemo za mawaziri na makatibu wa wizara.
Ishara za Kilifi kuwa ngome ya siasa za Pwani zilianza kuonekana wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa Agosti ambapo kampeni nyingi za wagombeaji wakuu wa urais zilielekezwa katika kaunti hiyo kuliko Mombasa.
Subscribe our newsletter to stay updated