Uncategorized

Sheria:Ndoa ni mkataba ambao lazima usajiliwe kwa mujibu wa Sheria

Na BENSON MATHEKA June 13th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

Ndoa nchini Kenya ni muungano wa hiari kati ya mwanamume na mwanamke, iwe ni katika uhusiano wa mke mmoja au wake wengi, uliosajiliwa chini ya Sheria ya Ndoa.

Ingawa ndoa huonekana kuwa jambo rahisi, inaongozwa na kanuni na taratibu nyingi ambazo mara nyingi hupuuzwa. Leo kwa ombi la wasomaji, tunafafanua vipengele vya kisheria na kitamaduni vya ndoa nchini Kenya.

Ndoa ni mkataba ambao lazima usajiliwe kwa mujibu wa Sheria ya Ndoa. Hivyo basi, wahusika wa ndoa wana haki na wajibu sawa wakati wa ndoa na hata wakati wa kuvunjika kwake.

Mkataba wa ndoa hutamatika pale talaka inapotolewa au kifo. Umri halali wa mtu kuingia kwenye mkataba kama huu ni miaka 18. Yeyote anayemuoa mtu ambaye hajafikisha miaka 18 anafanya kosa la jinai chini ya Sheria ya Makosa ya Kingono na Sheria ya Watoto. Hii huchukuliwa kuwa unyanyasaji wa watoto na ndoa ya mtoto.

Ili ndoa iwe halali, lazima ifanyike mbele ya mashahidi wawili waliokomaa kiakili na kimwili. Mashahidi hawa ni lazima wawe na umri wa angalau miaka 18, wawe na akili timamu, hawajalewa na wawe wanaelewa lugha inayotumika wakati wa sherehe ya ndoa, iwe kwa njia ya mkalimani au vinginevyo. Hata hivyo, wanandoa hawawezi kuwa mashahidi wa ndoa yao wenyewe.

Kuna aina tano za ndoa zinazotambuliwa kisheria nchini Kenya, ambazo ni:Ndoa za Kikristo  zinazofanywa kulingana na taratibu za imani ya Kikristo. Ndoa za kijamii  zinazofanywa na msajili wa ndoa wa serikali.

Ndoa za Kiislamu  kwa mujibu wa sheria na mila za Uislamu. Ndoa za kimila zinazofanywa kulingana na desturi za jamii mbalimbali za Kenya na Ndoa za Kihindu – kwa kufuata taratibu na ibada za Kihindu.

Ndoa inaweza kubadilishwa kutoka ndoa yenye uwezekano wa kuwa ya wake wengi hadi kuwa ya mke mmoja ikiwa  mume na mke watatangaza kwa hiari nia ya kufanya hivyo. Hata hivyo, ndoa ya wake wengi haiwezi kubadilishwa kuwa ya mke mmoja ikiwa wakati wa mabadiliko hayo mume ana wake zaidi ya mmoja.

Mabadiliko haya hufanywa kupitia tamko rasmi mbele ya afisa wa ndoa, na hurekodiwa kwa maandishi na kutiwa saini na pande zote. Msajili wa ndoa atatoa cheti cha kuthibitisha mabadiliko hayo kulingana na nia ya wahusika. Ndoa yenye uwezekano wa kuwa na wengi ni kama ya kitamaduni na Kiislamu.

Ni kinyume cha sheria na mila katika jamii nyingi kuoa au kuolewa na watu wafuatao: babu, nyanya, mzazi, mtoto, mjukuu, dada, kaka, binamu, shangazi, mjomba, mpwa wa kiume au wa kike. Pia ni marufuku kuoa au kuolewa na jamaa wa mwenzi wako kama vile: babu au nyanya yake, mzazi wake, mtoto wake, mjukuu wake, au wake/waume wa zamani wa mwenzi wako.