Habari za Kitaifa

Wakenya sasa kupata dawa za Ukimwi katika famasia za kijamii

Na ANGELA OKETCH August 3rd, 2024 1 min read

WAKENYA sasa wataweza kupata dawa za kupunguza hatari ya kuambukizwa Ukimwi (PrEP) kutoka kwa wanafamasia wa kijamii.

Hii ni baada ya utafiti kubaini kuwa kufanya hivyo kutaongeza kwa kiasi kikubwa matumizi ya dawa hizo nchini.

Utafiti ulibaini kuwa wanafamasia hao wa kijamii wataweza kutoa mwongozo mwafaka kwa watumiaji iwapo watapata mafunzo husika.

Utafiti huo pia ulitathmini jinsi maduka ya kuuza dawa yanavyotumiwa kusambaza PrEP katika kaunti sita zikijumuisha Kiambu, Kisumu, Migori, Homa Bay, Nairobi na Siaya na kuonyesha kuwa matumizi ya dawa hizo yameongezeka kutoka 10,000 mnamo 2016 hadi 438,003 katika mwaka wa 2023.

Ongezeko hilo lilitokana na mikakati kadhaa, ikiwemo kuanzishwa kwa famasia za kijamii.